Kumekuwa na mjadala mkubwa kuhusiana na
suala la mapato yaliyopatikana katika mechi ya Nani Mtani Jembe.
Mechi hiyo huwakutanisha Yanga na Simba, kwa
mara ya pili Yanga imepoteza, Simba wakishinda mechi ya kwanza kwa mabao 3-1,
halafu 2-0 katika mechi ya mwaka huu.
Mechi zote mbili fedha zilizopatikana
hazikutangazwa, mgawo wake ulikuwaje, haukutanagzwa pia!
Blogu hii imekuwa ikilivalia njuga suala
hilo, ingawa linaonekana kuwakera baadhi ambao huenda walifaidika.
Wako waliohoji kwamba blog inafaidika nini
au mwandishi anapata kipi? Lakini ukweli fedha za Yanga au Simba ni mali ya
jamii, hilo halina ubishi kwa kuwa timu hizo zinamilikiwa na Watanzania na si
mtu mmoja au wawili au viongozi walio madarakani.
Blogu hii inahoji kwa kuwa ni chombo cha
habari, itaendelea kuhoji kwa nia njema ili kupata ufumbuzi wa suala hilo
ambalo linauuhusu mpira wa Watanzania.
Walioandaa hiyo mechi ni Kampuni ya Bia
Tanzania (TBL) kupitia bia yake ya Kilimanjaro ambao ni wadhamini wa Yanga na
Simba.
Hongera kwa kuzidhamini timu hizo na kila
kitu kiko wazi kuhusiana na udhamini. Lakini suala la mechi ni kitu kingine na
kiko wazi.
Hoja kadhaa za msingi ambazo nimekuwa
nikihoji ni kiasi gani kilichopatikana ili kujua Yanga na Simba waliingiza
kiasi gani na wamefaidika nini.
Pili, TBL au Kilimanjaro walichukua kiasi
gani na kwa sababu ipi ya msingi, ni suala la muhimu sana kulijua kwa manufaa
ya mpira wa Tanzania.
TBL kama wamechukua fedha ni kwa sababu
gani? Maana wao ni wadhamini na kazi yao ni kuuza bia na si kuandaa mechi za mpira.
Kama hawajachukua, basi tuelezwe nani kachukua.
Pamoja na upande wa TBL, Simba na Yanga
walipata? Kama ni hivyo, kiasi
gani, mgawo wake ukoje?
Pia, vizuri tujue baada ya mgawo kama kweli
Yanga na Simba, pia TBL walipata. Wengine waliochukua ni akina nani na kwa
sababu gani?
Yako mengi yanaweza kuulizwa, vizuri kwa TBL
au Kilimanjaro kusimama na kutoa ufafanuzi katika suala hilo.
Wasomaji wengi wameanza kuhoji, wametaka
kujua, nini kilichotokea na kwa nini fedha hizo haziwekwi hadharani!.
Hoja ya msingi hapa ni kueleza kuhusiana na
mgawanyo wa fedha hizo si kukaa kimya au kununa kwa kuwa ni maswali yanayoweza
kuelezeka na lengo ni zuri tu kusaidia mpira wa Tanzania.
Pia kukaa kimya hakuwezi kuwa dawa, kwa maswali
yataendelea hadi majibu yatakapopatikana na kwa kuwa TBL ni kampuni
inayoheshimika. Basi si vema
ikaingia kwenye jambo ambalo linaweza kuichafua wakati huenda ikawa
haijahusika.
Ndugu yangu wewe ni Mwandishi, una haki ya kwenda ofisi yoyote na kuuliza chochote ambacho utataka ufafanuzi. Kwa Kuanzia nenda TFF watakupa majibu, uridhike/usiridhike na majibu yao nenda Simba na nenda Yanga pia na mwisho kabisa malizia na TBL baadaye tuletee ulichokipata kwenye blog yako sisi wasomaji wako lakini kama utaendelea kuuliza kwenye blog kama unavyofanya sasa hivi hutapata cha maana kwa sababu hakuna yeyote anayeona yuko responsible kujibu maswali yako.
ReplyDelete