February 21, 2015


Na Saleh Ally
KAMA ulishuhudia mechi kati ya Liverpool dhidi ya Besiktas ya Uturuki unaweza kujifunza mambo mengi sana kuhusiana na mshambuliaji Mario Balotelli.
Balotelli raia wa Italia mwenye asili ya Ghana, huenda ndiye binadamu ‘asiyejali’ zaidi kuliko wote duniani.
Muitaliano huyo, pia anaweza kuingia kwenye kundi la watu wanaosahau matatizo au kero haraka kuliko mwingine yeyote.


Balotelli amefanya kituko cha aina yake katika mechi hiyo ya Michuano ya Europa baada ya kumpokonya mpira nahodha wa timu hiyo, Jordan Herdeson na kwenda kupiga penalti.

Wakati anampokonya mpira huo, mshambuliaji mwingine tegemeo, Danny Sturridge alikuwa akitamani apige yeye, akamsisitiza nahodha wake ampokonye mpira Balotelli, haikuwezekana.

Akionekana kujiamini, alitembea na mpira mkononi ikiwa dakika ya 84. Akauweka eneo maalum la kupiga na kuupiga kwa ufundi mkubwa. Mwisho Liverpool ikashinda kwa bao 1-0 dhidi ya Waturuki hao.

Ukiliangalia suala la Balotelli lina sura mbili, kwanza ni utukutu kama ilivyozoeleka na hata amekuwa akionekana kama ni kituko.

Balotelli hajali, akiamua kufanya jambo bila hata kuangalia madhara yatakuwa nini, basi yeye anafanya na hajali kama inawezekana au la.

Kwa kuwa ni majeruhi, nahodha wa Liverpool, Steven Gerrard alikuwa jukwaani akifanya kazi ya uchambuzi kupitia runinga ya ITV.

Gerrard alimsifia Balotelli kufunga, lakini akasisitiza suala la kugombea mkwaju wa penalti kwamba halikuwa jema na si picha nzuri. Hilo kweli.

Kujiamini:
Utukutu wa Balotelli ni sehemu ya kuonyesha yeye ni kiburudisho kweli, maana anaamini anachokifanya hata kama si sahihi.

Lakini kujiamini kwake ni kwa hali ya juu sana. Huenda wachezaji saba kati ya 10 walio uwanjani ukitoa kipa, wangeweza kukimbia kupiga mkwaju katika dakika ya 85 wakijua ni lawama kama wangekosa.

Kwa Balotelli lawama si jambo kubwa sana kwake. Alijiamini na kuchukua ule mpira, akijua wazi kama angekosa, basi angekuwa katika matatizo makubwa.

Kwani tangu ametua England, amefunga katika mechi moja tu ya Ligi Kuu England. Amekuwa na presha kubwa hadi alipofunga bao hilo, sasa jiulize angeipoteza penalti hiyo ingekuwaje?

Lakini kwa kuwa Balotellia anajiamini, hakuona shida. Akagombea mpira, akapiga na kufunga. Mwisho yeye ndiye shujaa hata kama itaonekana amekosea, alichokosea kinafutika.

Maisha ya Balotelli ni zaidi ya hadithi, amezaliwa katika familia ya Kiafrika ya Barwuah na kulelewa na familia ya Kizungu ya Balotelli. Huenda hilo ni tatizo kwake pia kwa kuwa haelewani kabisa na baba yake mzazi lakini amekuwa akiendelea kutoa huduma katika familia yake.
Kelele kubwa ya vyombo vya habari vya England ni Balotelli kutokuwa msaada kwa Liverpool kutokana na kutofunga mabao, anaonekana ni hasara.

Safari hii amegeuza uelekeo, kwanza amefunga bao la ushindi katika Ligi Kuu England wakati Liverpool ilipoishinda Tottenham Hotspurs kwa mabao 3-2. Sasa amefunga bao lake muhimu na kuibeba Liverpool.
Mabao mawili yaliyopeleka pointi tatu na nafasi nzuri ya kusaidia kusonga mbele katika Ligi ya Europa. Unawezaje kumkosoa Balotelli kwa kusema hajui? Hakika itakuwa vigumu.

Kujiamini kupindukia:
Karibu kila mmoja anajua Balotelli anaathirika kwa kujiamini kupindukia. Si mwoga na asiyejipima alipo ni sehemu sahihi ya kufanya anachotaka au la.
Akiwa Man City alizichapa na Jerome Boateng, akazozana na Yaya Toure, Micah Richard na Kocha Roberto Mancini. Liverpool tayari ameishazua mzozo na Sturridge.

Kuna mengi ya kujifunza kwa Balotelli. Kwanza kabisa si kumhukumu kwa makosa yake, iko haja ya kuangalia pia ubora wake kama ambavyo leo Wazungu wamekuwa wakiangalia ubora wa Balotelli.

Kama ingekuwa ni kuangalia ubora tu, hakuna atakayetaka kuendelea kufanya naye kazi leo hii. Lakini kwa wachezaji, pia wakati mwingine wajifunze, kujiamini ni sehemu bora hasa kama unachokifanya unaamini ni bora ingawa kukubali ushauri kama unaona ni sahihi pia ni bora zaidi.


Kweli Balotelli ni mtukutu, lakini angekuwa hajiamini ingekuwa rahisi kuyumbishwa na huenda leo angekuwa anakipiga katika timu ya daraja la pili.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic