February 20, 2015



Kocha Mkuu wa Simba, Goran Kopunovic, ameingizwa mjini baada ya kuibiwa kiasi cha dola 300 (Sh 510,000) pamoja na fedha za Kitanzania ambazo hazikufahamika ni kiasi gani akiwa katika hoteli yenye hadhi kubwa mkoani Morogoro.


Kocha huyo amekumbwa na tukio hilo alipokuwa mkoani humo wakati timu yake ilipokuwa mkoani humo maalum kwa ajili ya mechi dhidi ya Polisi Morogoro iliyochezwa, Jumapili iliyopita.

Filamu ya tukio hilo ipo hivi; alipofika mkoani hapo alifikia katika hoteli (jina kapuni), Jumanne asubuhi kocha huyo alihamishiwa katika hoteli nyingine kwa sababu za kile kilichoelezwa usalama.

Baada ya hapo, mizigo ya Kopunovic ikatangulizwa kwenye hoteli hiyo kubwa na kisha michakato yote ikafanyika, baada ya kocha huyo kufika hotelini hapo na kuingia ndani jioni ya siku hiyo, ndipo alipogundua kuwa kulikuwa na upungufu wa kiasi hicho cha fedha na kuamua kuripoti suala hilo kwa uongozi wa hoteli.

Baada ya kocha huyo kuripoti, uongozi wa hoteli ukaitisha kikao cha dharura na kukubaliana kumlipa fidia ya shilingi 540,000 licha ya kudai kuwa hoteli hiyo haihusiki katika upotevu huo, lakini umeamua kufanya hivyo ili kulinda heshima ya wateja wao na hoteli hiyo kwa jumla.

Chanzo kutoka katika hoteli hiyo kilisema kuwa, ulifanyika upekuzi juu ya yeyote aliyehusika kuingia kwenye chumba cha kocha huyo kupitia kamera zilizopo hotelini hapo lakini hakukuwa na jibu la uhakika la kilichotokea kwenye kamera hizo.

Alipotafutwa Ofisa Habari wa Simba, Humphrey Nyasio juu ya suala hilo alikanusha vikali kuwepo kwa taarifa hizo na kusema: “Hakuna kitu kama hicho, kama kungekuwa na suala kama hilo lazima kocha angeniambia tu.”

Upande wa uongozi wa hoteli hiyo haukuwa tayari kufunguka wakati Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Simba, Kassim Dewji alikiri kuwepo kwa suala hilo na akalitolea ufafanuzi.

“Hilo suala la wizi ni kweli limetokea na ni kwamba kocha alitoka chumbani kwake, aliporejea akakuta fedha zake zimepungua, kulikuwa na dola 600 lakini akakuta zimebaki 300.


“Ni ajali imetokea na sisi kama uongozi tumesikitishwa na kusononeshwa kwa wizi huo ingawa kocha hakutakiwa kuacha fedha chumbani. Kuhusu kulipwa taarifa hizo sijazipata ila kama amelipwa tayari au mtu amejitolea kuzilipa, basi ni suala zuri,” alisema Dewji.

SOURCE: CHAMPIONI

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic