March 23, 2015


INAWEZEKANA leo itakuwa ni zaidi ya mara tatu naandika kuhusiana na usalama kuwa hovyo, uliozorota na hatari kwa wanamichezo ndani ya Uwanja wa Mkwakwani mjini Tanga.


Katika misimu mitatu, nilifanikiwa kuhudhuria mechi mbili katika uwanja huo na kushangazwa na mambo mengi sana huenda si lahisi kuyaona katika viwanja vingi vya soka au michezo hapa nchini.

Kwanza ni mashabiki wake kupenda ugomvi kupindukia, tena ugomvi usiokuwa na sababu za msingi. Yaani ni sehemu ambayo mashabiki wao wanaamini ubabe ndiyo ujanja, ugomvi usiokuwa na sababu.

Mwaka juzi wakati Yanga ikipambana na Coastal Union iliyokuwa chini ya Jamhuti KIhwelo ‘Julio’ na kuishinda kwa bao 1-0 lililofungwa na Mganda Hamis Kiiza. 

Mashabiki walifanya vurugu za kupindukia hadi kwa waandishi wa habari waliokuwa wakiripoti mchezo huo.
Mashabiki hao walianza kuwashambulia waandishi wakati wakimshutumu mwamuzi aliipendelea Yanga.

Chupa za maji na matusi yakaanza kuwaangukia waandishi waliokuwa wametulia tuli wakiripoti. Binafsi nilishangazwa kushuhudia sura nyingi za ninaoweza kuwaita watu wazima au wakuu wa familia wakifanya upuuzi huo. Nilifanya juhudi kuu kuwapiga picha ili niwaanike, wakajificha.

Kujificha kwao kulinifanya niamini kuwa walichafua hali ya amani kwa makusudi huku wakijua waziwazi walichokifanya hakikuwa kitu cha kiungwana na si cha kistaarabu. Sasa vipi wanafanya hivyo!

Tokea hapo nimekuwa nikiendelea kushuhudia vurugu karibu kila mechi ya Yanga au Simba zinapocheza kwenye uwanja huo. Wakati mwingine hata timu hizo za Coastal Union na Mgambo zinapokutana. Hawa watu wa Tanga vipi, wanajua sana ngumi? Sasa kwa nini wengi wao wasicheze judo au Kung Fu wakaachana na soka ambayo haitaki “Yan kibadachi!”

Juzi umeona tena, mara tu baada ya mechi kati ya Mgambo dhidi ya Yanga kumalizika, mashabiki hao waliruka uzio na kuvamia uwanjani na kuanza kuwabeba wachezaji wa Yanga, hasa Simon Msuva.

Hawa walikuwa mashabiki wa Yanga, jiulize vipi wamekuwa na tabia hizo za kizamani ambazo sasa ni nadra kuona zinajitokeza katika mechi za Ligi Kuu Bara katika viwanja mbalimbali. Bado ninaamini ni mashabiki wa Yanga wa mkoani Tanga ambao wamezoea kutofuata utaratibu.

Kama wangekuwa Yanga wa Dar es Salaam, mbona hawafanyi hivyo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar. Msisitizo kama ni wa Dar es Salaam walifanya hivyo, basi hata Polisi wanaosimamia ulinzi Mkwakwani nao watakuwa ni wazembe na wanastahili kubadilika.

Vipi mashabiki wavuke uwanja na kuingia ndani mara tu baada ya mechi. Waliokuwa wamembeba Msuva, tuna uhakika vipi wote wanampenda. Wangemchoma kisu, tena tunajua siku chache zilizopita, mashabiki wa Yanga wamekuwa wakimtafuta na kutaka kumpiga!

Msimu ujao, mji wa Tanga utakuwa na timu tatu zinazoshiriki Ligi Kuu Bara ambazo ni Coastal Union na Mgambo ambazo hazina ugeni tena wa ligi hiyo. 
Usisahau wakongwe wengine African Sports nao wamerejea baada ya kushika nafasi ya pili wka ubora baada ya Mwadui FC ya Shinyanga.

Upinzani wa African Sports dhidi ya Coastal Union unajulikana kwa kuwa ni kati ya timu kongwe kabisa za soka nchini. Lazima kutakuwa na vurugu katika kila mechi inayozihusisha hata kabla hazijakutana zenyewe.

Pia kutakuwa na vurugu katika kila mechi inayokutanisha Coastal na Simba Yanga au African Sports dhidi ya Yanga au Simba. Unaweza kusema wigo wa vurugu na upana wa matatizo utaongezeka katika uwanja huo wa Mkwakwani. Swali, walinzi wa uwanja huo wanaoonekana kutokuwa tayari katika misimu mitatu au zaidi sasa, watakuwa tayari kudhibiti hali hiyo ya hovyo msimu ujao?



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic