April 10, 2015


SHIRIKISHO la Soka Afrika (Caf) limetoa makundi na ratiba ya kuwania kucheza Kombe la Mataifa Afrika mwaka 2017.


Katika ratiba ya makundi iliyotolewa na Caf, Tanzania imetupwa Kundi G, ikiwa na vigogo wawili wa Afrika, Nigeria na Misri. Timu ni nyingine ni Chad.

Kitendo cha Tanzania, Taifa Stars kupangwa na Nigeria na Misri, tayari hofu imetawala miongoni mwa Watanzania wengi.

Katika mijadala niliyoisikia kuanzia katika mitandao, makundi ya wadau wa soka na michezo mingine na wale niliojadiliana nao wanafikiriaje, wengi wanaona hadithi ya Tanzania kuendelea kuiona michuano ya Afcon kwenye ‘kideo’ itaendelea kama kawaida!

Wengi wanaamini hilo halina mjadala, wakiamini ni ndoto Tanzania kuzipindua Misri na Nigeria na kuchukua nafasi ya kucheza Kombe la Mataifa Afrika. Msisitizo wao, hadithi ya “kichwa cha mwendawazimu” inaonekana kukosa mwisho.

Hofu hiyo inaonyesha dhahiri Watanzania hawaiamini Taifa Stars inayoongozwa na Kocha Mholanzi, Mart Nooij. Kwa nini hawaiamini? Jibu mwendo wake hata katika mechi za kirafiki umekuwa ni wa kusuasua sana.

Pamoja na mwendo kuwa wa kusuasua, bado Stars imekuwa ni ileile, isiyokuwa na mabadiliko huku Nooij mwenyewe akionyesha kufurahia tu.

Tangu ameichukua timu hiyo kwangu nimekuwa sioni tofauti ya Mholanzi huyo na Mdenishi Kim Poulsen ambaye angalau alionyesha imani kwa wachezaji vijana ambao leo wamekuwa tegemeo katika ngazi za klabu na hata timu ya taifa.

Unakumbuka alichokifanya kwa akina Simon Msuva na Frank Domayo. Unakumbuka alivyowaamini akina Ramadhani Singano na hata Jonas Mkude. Sasa ni tegemeo katika klabu mbalimbali na Stars pia.

Nooij amekuwa na mfumo wa “watu wazima” tena katika mechi za kirafiki na bado timu yake imekuwa haina matokeo mazuri kwamba unaweza kusema alimchagua Amri Kiemba badala ya Ibrahim Ajibu kwa kuwa alisaidia sana timu ishinde mabao mengi kujiweka vizuri katika msimamo wa Fifa.

Bora ya sare ndani ukiwa na Ajibu kuliko Kiemba, bora kupoteza ndani ukiwa unamtumia Salim Mbonde kuliko Aggrey Morris. Hawa watakwenda baada ya muda kwa kuwa umri nao unawalazimisha.

Tanzania sasa inawahitaji vijana waje kufanya mabadiliko. Uwezo wanao na wanahitaji kuanza kutumika sasa si kipindi tunaingia katika mashindano dhidi ya Misri, Nigeria ndiyo wanapewa nafasi katika kikosi cha timu ya taifa, haiwezi kuwa sawa.

Hofu kubwa inayowakuta wengi ni kwa kuwa hawaoni kama kuna maandalizi kwa ajili ya kikosi cha baadaye au vijana wachache wenye mwanga wa kusaidia hata baada ya akina Kiemba, Cannavaro na wengine kuondoka.

Tanzania itaendelea kuzihofia timu nyingine hadi lini? Cape Verde, Rwanda na timu nyingine zimewahi kufuzu licha ya kuwa katika kundi moja na timu ngumu kama Cameroon na nyinginezo.

Unapokuwa na jeshi bora, hakika hauwezi kuhofia vita. Sisi tumekuwa waoga kwa kuwa tunaliona jeshi letu kwamba si imara namna ile na hata ujengwaji wake umekuwa na walakini wa juu. Vipi watu watakuwa wana imani ya kuona linakwenda vitani kupambana wasiwe na hofu?

Hofu isipotutoka Watanzania maana yake hatuwezi kushinda kwa kuwa hatuwezi kuwa na uhakika wa asilimia mia kuzikwepa timu za Afrika Magharibi na Kaskazini katika makundi.

Kufanikiwa ni lazima kukubali lazima tukutane nazo na baada ya hapo ni kujiandaa vema, kujipanga sahihi ili kushinda dhidi yao.

Ukitaja timu bora kabisa za Afrika, hauwezi kuiacha Algeria lakini usisahau kikosi cha Stars chini ya Kim Poulsen kiliionyesha kazi ya kuitwanga kwa mabao 3-1 pale Taifa jijini Dar tena kikiwa na vijana walioonekana kama wasingeweza.


Hata Cameroon, Misri, Nigeria wakikutana na Algeria wanajua si kazi rahisi. Stars iliitungua. Hiyo ni picha kuonyesha kuwa inawezekana lakini kwa maandalizi yanayoendelea sasa inatia shaka.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic