May 1, 2015


Na Saleh Ally
ALIYEWAHI kuwa mdhamini mkuu wa Coastal Union, Nassor Bin Slum, ametangaza kurejea tena na kuungana na viongozi wa klabu hiyo baada ya kukaa nje kwa miezi kadhaa.


Bin Slum alikaa nje ya klabu hiyo baada ya kutoelewana na viongozi wa klabu hiyo, hali iliyoanzisha mashambulizi kwenye vyombo vya habari, kila upande ukiulaumu mwingine.

Kurejea kwa Bin Slum kwa mara nyingine kumezua gumzo kubwa, wengine wakisema uongozi umekwama, ndiyo maana umeamua kumrejesha maana kikosi hicho kilikuwa kinateremka daraja.

Yeye anasema ameamua kurejea katika klabu hiyo kutokana na mapenzi yake na si kwamba sasa ni mdhamini tena. Katika mahojiano maalum na Championi Ijumaa, Bin anafunguka:

Kipi kimekufanya urejee Coastal, uliacha kitu labda?
Bin Slum: Kwanza nifafanue, nimerudi Coastal kama shabiki na mwanachama, si kama mdhamini kama ilivyokuwa awali. Nimekuwa nikiifuatilia timu, kipigo dhidi ya Prisons nyumbani, nikagundua inateremka daraja, maana naijua Coastal.

Unaweza kufafanua unaijuaje?
Bin Slum: Msimu uliopita, mechi tano za mwisho tulivurunda. Bahati nzuri tulikuwa tumefanya vizuri mwanzoni, ikatusaidia.
 
AKIINGIA MKATABA NA STAND UNITEDMsimu huu timu imeanza vibaya tangu mwanzo, sasa kama itafanya vibaya mwishoni, maana yake itateremka. Hesabu zilionyesha tofauti ya Coastal na timu iliyo mkiani ni pointi tatu tu, ikanitisha.

Kabla ya kurejea, ulifanya tathmini na kujua tatizo ni nini?
Bin Slum: Mchawi wa haya wanajua wachezaji na viongozi, ila viongozi wana tatizo zaidi pia. Wanakuwa wamejiwekea malengo ya kufanya vizuri, wanapofeli, huanza kutafuta mchawi na mzigo ni kwa wachezaji.

Nilirudi katika mechi dhidi ya Yanga. Msisitizo wangu ulikuwa ni kurudishwa kwa wachezaji. Niliomba warejeshwe ili kupambana na Yanga, lengo tusahau yaliyopita.

Coastal ilikuwa haina wachezaji wengi kama Mbwana Hamis ‘Kibacha’, Joseph Mahundi, Tumba Sued na Selemani Kibuta. Utasikia Julio alisema tumeshitukizwa, lakini ukweli waliocheza siku hiyo walikuwa vijana wengi, ni rahisi kupoteza dhidi ya Yanga iliyo sawa.
 
AKIINGIA MKATABA NA NDANDA...
Viongozi hawakulisikiliza hilo, tukafungwa nane. Ukawa wakati mzuri wa kuwakumbusha, nashukuru sana wakakubali kuwarudisha wachezaji wazoefu na kweli wakasaidia mechi iliyofuata dhidi ya JKT, tukashinda kwa mabao 2-0 kule Chamazi.

Unafikiri malengo ni tatizo pia?
Bin Slum: Malengo ni kitu kizuri, lakini viongozi wanakuwa na hofu ya kufeli. Hata mwaka huu, Coastal ilijiwekea malengo ya kuwa bingwa, mwisho mambo yamekwenda tofauti. Badala ya kulumbana, vema kukaa na kutathmini kwa pamoja.

Unakumbuka hata msimu walipofukuzwa akina Juma Nyosso na Crispine Odulla, Haruna Moshi ‘Boban’ akajitoa. Baada ya hapo, timu ikaanza kuyumba. Nafikiri kuliko kulaumiana, kurekebishana ni jambo bora zaidi.

Msimu huu, kipa mzoefu kama Shabani Kado pia hakuwa akipangwa. Kuna mambo mengi, lakini binadamu mnapokuwa pamoja lazima mkubali kuvumiliana, kurekebisha na kwenda pamoja.
 
BOBAN WAKATI AKIWA COASTAL...
Umerudi Coastal sababu ya mapenzi, ulikaa kando kwa sababu ya chuki?
Bin Slum: Sina chuki na Coastal, ila nina chuki na wale wanaofanya ifeli. Sina kinyongo nao, ndiyo maana wanapokosea ninasema bila ya woga. Mimi ni mwanachama wa Coastal, nina haki, niliamua kukaa kando kwa kuwa sipendi malumbano.

Uchaguzi unakaribia, unafikiri nini bora cha kufanya ili kutengeneza Coastal imara?
Bin Slum: Swali zuri sana, kwanza lazima viongozi wa makundi yote yanayokubaliana na yanayopingana wakutane pamoja. Wanaweza kumualika hata mkuu wa mkoa kama mlezi au mtu muhimu, wakazungumza na kukubaliana.

Wasahau yaliyopita, wapeane mikono na baada ya hapo wapendekeze viongozi wanaoamini wakigombea na kushinda wataisaidia timu na klabu kwa ujumla.

Vipi wewe kuhusu nafasi yoyote ya uongozi ili uisaidie timu na klabu?
Bin Slum: Sina mpango wa kugombea, wala sina mtu ninayemuunga mkono kwa maslahi binafsi. Nitawaunga mkono wote wenye lengo la kusaidia klabu. Tunahitaji viongozi imara kwa manufaa ya klabu yetu, hiyo ndiyo furaha ya kila mwana Coastal.

Coastal ikishinda mechi dhidi ya Stand United, itajiweka katika mazingira ya kukwepa kushuka. Wewe ni shabiki wa Coastal na mdhamini wa Stand, hapo vipi?
Bin Slum: (Tabasamu) Kweli mimi shabiki na mwanachama wa Coastal lakini Stand inadhaminiwa na Bin Slum Tyres Ltd kupitia bidhaa za Double Star. Hii ndiyo tofauti, ni vitu viwili tofauti kabisa.

Wana Kimanumanu African Sports wamepanda, nyie Coastal mmejiandaa kweli?
Bin Slum: Ndiyo maana tunapambana Coastal ibaki ili tuone Tanga derby ambayo hatujaishuhudia kwa miaka 23 sasa. Kumbuka familia ya Bin Slum ilipambana kuona Sports inarejea ligi kuu.


Lengo ni kurejesha ushindani na changamoto katika soka la Tanga. Ndiyo maana nilikuambia, utaipandisha Sports halafu uiache Coastal iteremke? Haiwezekani hata kidogo!

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic