May 1, 2015


KIKOSI cha Yanga kimewasili nchini Tunisia kwa ajili ya mechi ya pili ya Kombe la Shirikisho dhidi ya wenyeji wake, Etoile du Sahel.


Mechi ya kwanza mjini Dar es Salaam, timu hizo mbili zilitoshana nguvu kwa sare ya bao 1-1, Waarabu hao wa Tunisia wakisawazisha kipindi cha pili.

Yanga wanatakiwa kushinda au sare ya aina yoyote ile kuanzia 2-2 ili kuweza kusonga mbele. Wote tunajua haitakuwa kazi rahisi hata kidogo kwa Yanga kuuvuka mlima wa Waarabu hao.

Nawaita mlima kutokana na kazi ngumu wanayotakiwa kuifanya Yanga. Wapande vipi, nguvu yao ikoje na wapinzani wanaokutana nao wako vipi.

Kazi hiyo inatakiwa ifanyike kesho, Etoile wamejiandaa na wameonyesha kwamba mambo yao wanayafanya kwa tahadhari kubwa wakiamini Yanga si timu ya kubeza.

Wote tuliona timu yao si ya kubahatisha, ni washindani hasa kwa Yanga na wana wachezaji wengi wa viwango vya juu kuliko hata wale wa Yanga, hakuna haja ya kuficha.

 Tuliona wakiwa ugenini kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, walionyesha soka safi, soka la mipango na walionekana ni watu walioiva kwa ajili ya michuano ya kimataifa. Haitakuwa kazi rahisi kwa Yanga, lakini si kazi isiyowezekana kwa asilimia mia.

Kweli mpira una maajabu yake, lakini Yanga hawawezi kukaa, wakasinzia halafu maajabu yakafanya kazi yenyewe. Lazima wapambane kweli wakijua kazi waliyonayo ni ngumu zaidi ya ile waliyokutana nayo jijini Dar es Salaam.

Baada ya sare, asilimia 50 ya watu wa Yanga wakiwemo mashabiki walikata tamaa kabisa. Nilizungumza na baadhi ya wachezaji wa Yanga, ingawa mazungumzo yao yalionyesha wanaweza kufanya maajabu na watapambana, lakini hakukuwa na mwendo mmoja kati ya macho na matamshi yao.

Hata wao walionekana kuwa na hofu, jambo ambalo ninaamini ni baya zaidi kwa Yanga kwa kuwa kama watakwenda na hofu kwamba jamaa hawawezekani, basi ni rahisi sana kufungwa hata bao tano au saba.

Watu wa mpira, tano wanaita mkono na saba ni wiki. Kweli kabisa, kama Yanga wataamini hawawawezi Etoile kabla ya kuingia uwanjani, lazima wajue wanajitengenezea chumba cha kupigwa mabao mengi na kuingia katika aibu. Badala yake wanapaswa kujua wao sasa ni wawakilishi wa Yanga na taifa pia.

Hivyo lazima wapambane mwanzo mwisho na kwa juhudi na ufundi wa juu na hapo ndiyo soka linaweza likaleta maajabu yanayoweza kutokea na kufanya kazi yake.

Waungwana, kweli Etoile wana uwezo mkubwa. Tukubali hata Al Ahly nao ni wakubwa, tena kuzidi timu hiyo ya Tunisia, lakini tuliona walivyopata kazi kubwa kwa Yanga hadi kuwatoa kwa mikwaju ya penalti, tena Yanga wakiwa na nafasi kubwa zaidi ya kusonga mbele.

Timu za Waarabu ni bora kuliko zetu kutokana na mazingira na hali halisi lakini katika soka mara nyingi umeona timu iliyoonekana haiwezi kushinda, ikifanya hivyo kwa kuwa watu walijiandaa na walipambana kiume.

Hata kama wanawake wanacheza, soka ni mchezo wa kiume. Wanaume jasiri hawarudi nyuma, badala yake wanapambana hadi tone la mwisho. Yanga inaweza kupambana na kufanya vizuri dhidi ya Etoile.

Yanga haikuwa na mchezo mzuri katika mechi ya kwanza jijini Dar es Salaam. Inaweza ikawa na mchezo mzuri ugenini huku Etoile nao wakiwa hawana mchezo mzuri nyumbani. Hayo yote ni mambo ya mpira na yanatokea. Yanga hawapaswi kuangalia uzuri au ubaya wa mchezo, muhimu kupambana wakiwa na malengo.


Kitu cha kwanza ni kukubali ni mechi ngumu, pili ni maandalizi ambayo yamefanyika, tatu ni kufuata maelekezo ya mwalimu, nne ni kuamini inawezekana na tano ni kupambana hadi kieleweke. Kila la kheri.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic