July 22, 2015


 Na Saleh Ally
MWAKA 2003, Denis Oliech akiwa na umri wa miaka 17 tu, aliingia katika kipindi cha pili katika mechi dhidi ya Tanzania Bara ‘Kilimanjaro Stars’ na kuisaidia Kenya ‘Harambee Stars’ kubeba ubingwa wa Kombe la Cecafa kwa kuishinda Kilimanjaro Stars.


 Kocha Mkuu wa Tanzania, James Siang’a ambaye ni raia wa Kenya, alijua kabisa kwamba kuna hatari ya Oliech. Lakini aliwaamini mabeki wake wa kati, Boniface Pawasa na Lubigisa Lubigisa ambao walikimbizwa na Oliech kuanzia katikati ya uwanja pale CCM Kirumba kabla hajamchambua Juma Kaseja na kuandika bao la tatu na kuifanya Kenya iibuke na ushindi wa mabao 3-2.

 Kipindi hicho, Kenya ilikuwa chini ya kocha kijana, huyu ni Jacob ‘Ghost’ Mulee ambaye anajulikana kwa kazi nzuri.
 Ushindi ule, uliwafanya Watanzania waliojazana kwa wingi Kirumba waanze kutoka taratibu. Habari ikaisha, kila mmoja wetu, waandishi na mashabiki wa kawaida, tulikubali iko siku Oliech atacheza soka Ulaya. Kweli, sasa anakipiga nchini Ufaransa.

 Michuano ya Kombe la Kagame inaendelea katika jiji la Dar es Salaam na gumzo kubwa sasa ni mshambuliaji Michael Olunga wa Gor Mahia ambao ni mabingwa wa Kenya.

 Olunga raia wa Kenya pia, sasa ana umri wa miaka 21 na ameonyesha uwezo mkubwa ingawa haujawa wa kutosha kupita kiasi.
 
AKIHOJIWA NA SUPER SPORT...
Lakini kwa kuwa Tanzania haina mshambuliaji hata mmoja katika timu zake tatu ambaye ameonyesha ni hatari kweli au zaidi ya Olunga, maana yake lazima yeye awe gumzo na mjadala mkuu.

 Olunga amecheza mechi mbili, moja dhidi ya Yanga na nyingine dhidi ya KMKM ya Zanzibar. Katika mechi hizo amefanikiwa kupachika mabao matatu.

Nakukumbusha katika mechi hizo mbili alizofunga mabao matatu ni dhidi ya ngome za timu za Tanzania yaani Yanga aliyoifunga bao moja na KMKM mabao mawili.

 Amezinyanyasa timu mbili za Tanzania, kupitia safu mbili za ulinzi zinazoongozwa na Watanzania kwa asilimia 90. Ndiyo maana Olunga kawa gumzo na vyombo vya habari vya Tanzania na nchi jirani, viko ‘busy’ kuhusiana naye.

 Vyombo vya habari vimekuwa ‘busy’ naye kwa kuwa Watanzania wengi wanataka kujua kuhusiana naye. Sasa ni gumzo, kwamba atakwenda Yanga au Simba, maana Azam FC nao imeelezwa kwamba wanammezea mate.

 Stori yake ndiyo ile ya Oliech ambaye kipindi kile ilielezwa angesajiliwa na Simba, hata hivyo ikashindikana kwa kuwa ilikuwa na watu kama kina Athumani Machuppa na Oliech mwenyewe alionyesha msimamo kwa kuwa ndoto yake ilikuwa ni kucheza Ulaya.

 Olunga ambaye ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Ufundi nchini Kenya, tayari amesema yu tayari kucheza kokote lakini anachoangalia ni maslahi, ingawa zaidi angependa kucheza Ulaya.
KIKOSI CHA GOR MAHIA, OLUNGA WA PILI KUTOKA KUSHOTO WALIOSIMAMA.
 Tayari aliwahi kukataa kujiunga na Super Sport United ya Afrika Kusini kwa sababu moja tu. Ilishindwa kumpatia nafasi ya kujiendeleza kimasomo kwa kuwa alitaka kucheza soka huku akisoma.

Tangu Kenya walipompeleka Oliech Ulaya baada ya kuwa ameibukia hapa nyumbani kwetu kwa kuipa nchi yake Kombe la Cecafa. Leo ni miaka 13, Tanzania haina mchezaji yeyote anayecheza Ulaya hasa katika ligi tano kubwa za England, Hispania, Ujerumani, Italia na Ufaransa.

 Katika miaka hiyo 13, Tanzania imeendelea kuendeleza maneno, yaani fitna, watu wasiopendana katika mpira hadi tumeibukia kwa Olunga na sasa amekuwa gumzo, hakuna ubishi kama ataendelea hivyo, basi iko siku atacheza Ulaya.

 Mulee ambaye sasa ni mchambulizi katika runinga ya SuperSport, kipindi hicho alikuwa kocha na mlezi wa Oliech kisoka. Sasa Mulee ndiye mlezi wa Olunga na hawezi kwenda timu yoyote bila ya kuhusishwa kwa kuwa alianza kuchipukia kisoka katika kituo chake cha malezi ya wanasoka vijana, pia ile michuano ya Airtel Rising Stars ambayo mara moja ameibuka kuwa mchezaji bora.

 Tokea kwa Oliech hadi kwa Olunga, hapa nyumbani kuna nini ambacho kinaweza kuelezwa ni sehemu ya mpira kupiga hatua?

 Kumezea mate si jambo baya, lakini katika soka kuendeleza watu wako ni jambo jema. Simba, Yanga na Azam zinazommezea mate mshambuliaji huyo zimefanya nini kwa vijana wa Tanzania?

 Huu ndiyo msimu wa kwanza kwa Olunga kutamba kwenye Ligi Kuu Kenya. Kama umaarufu zaidi, atakuwa ameupata kwenye Kagame, michuano inayofanyika Dar es Salaam.
Inafanyika katika ardhi yenye waoga wengi, wasiopendana wengi na wenye uwezo mkubwa wa kutamani na kusifia vya wenzao huku wakijivunia maendeleo ya wenzao.

 Sioni kama kuna ubaya kumpa Olunga sifa zake kwa kuwa anafanya vizuri. Lakini kama ni sahihi kuendelea kuwa washangiliaji, wasindikizaji na watoa fursa kwa wageni kung’ara na kuigeuza nchi ya Tanzania sehemu ya watu kupitia kwenda kwenye mafanikio makubwa. Zindukeni, furahieni vya wenzenu lakini nafsi ziwaume, mtengeneze na vyenu na wanaotengenezwa nao wajitume. Mwe!




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic