October 9, 2015


Na Saleh Ally
TAIFA Stars imeamsha matumaini upya kwa Watanzania kwa kuitandika Malawi mabao 2-0 katika mechi ya kuwania kucheza Kombe la Dunia nchini Urusi mwaka 2018.


Moja ya mambo ambayo yamekuwa magumu katika timu yetu ya taifa kwa miaka nenda rudi ni kucheza michuano miwili mikubwa, Afcon na Kombe la Dunia.

Kila Mtanzania mpenda soka au michezo kwa ujumla atakuwa anatamani kuiona hiyo hali tukiifikia. Kwamba Taifa Stars inakwenda kushiriki Afcon au ikiwezekana Kombe la Dunia, dah! Acha ifike.

Hata hivyo siku hiyo, haiwezi kufika kwa ndoto tukiwa tumelala. Lazima kupambana na kuwa na mipango endelevu ambayo inaangalia mbele angalau kwa uchache wa miaka 10 mbele yetu.

Miaka 10 mbele, haiwezi kuwa mipango yenye wigo finyu ambayo unaangalia vitu vichache. Lazima watu wafungue vichwa vyao kweli na kujua kipi wanakitaka na kukisimamia kwa miaka yote tena kukiwa na mipango na maendeleo.


Mipango inaanzia kwa vijana kwenda mbele. Lazima watu waachane na mambo ya kuripua, wakiamini ushindi wa leo ndiyo kila kitu.

Tumekaa kando muda mwingi sana, huu ndiyo wakati wa vitendo na baada ya Taifa Stars kuitwanga Malawi kwa mabao 2-0 angalau kunainuka matumaini upya kwamba kuna uwezekano wa kufanya jambo Fulani.

Hiyo ni habari njema au dalili ya kuonyesha tunaanza kwenda ingawa Watanzania lazima waweke vichwani mwao kwamba kwa kuwa Stars inashiriki mechi za soka, kupoteza siku yoyote inawezekana pia ni jambo la kawaida na wasianze kelele kwa kupoteza mechi moja. 


Katika soka kuna kuteleza na kuinuka na uwezekano wa kufanya hivyo kabla ya kuanguka upo.

Lakini lazima tukubali, Stars haikucheza vema kama ilivyokuwa katika mechi dhidi ya Nigeria. Hii ni changamoto pia inayoonyesha bado safari ni ndefu na hakuna haja ya kuridhika.

Wakati nikishuhudia mechi ya Stars dhidi ya Malawi ambayo mabao mawili ya mechi ya yalifungwa na Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu, nilianza kufikiri kuhusiana na washambuliaji hao wawili wa TP Mazembe.



Samatta na Ulimwengu sasa ni lulu ambayo Watanzania ambao wanajivunia. Swali likawa hivi, hivi bila ya hawa wapiganaji wawili? Tunakwenda vip?

Nakumbuka mechi zote ambazo wanakosekana, mara nyingi John Bocco amekuwa mkombozi. Lakini kweli tuna watu ambao tunaamini kweli ndiyo sahihi wanaweza kushika mikoba ya Samatta na Ulimwengu?

Lazima tukubali wao ni binadamu, wanaweza kuwa wanaumwa au majeruhi na Tanzania ina mechi muhimu sana ambayo inatakiwa kushinda. Ndani ya 11 hayumo Samatta na Ulimwengu, kweli tunaweza kuwa na kikosi kitakachopambana mwanzo mwisho na kusababisha ufungaji wa mabao.

Achana na hawa wawili, nguvu ya kule mbele kwa Taifa Stars pia inaongezwa na Mrishi Ngassa. Watakaokuwa wanamsahau basi wanafanya makosa sana, ana msaada mkubwa ingawa namba yake ya pembeni angalau utasema kuna watu mbadala kama Simon Msuva au Farid Mussa.

Lakini kwa Ulimwengu na Samatta ambao ni washambuliaji wenye uwezo wa mengi wasiyoweza wengi. Mfano kuingia na mpira wakiwa wamezongwa na mabeki hadi watatu, kutoa pasi zinazozaa mabao au kufunga kwa uwezo binafsi. Nani mwingine wa hapa nyumbani?

Ninaweza nikawa nawauliza mashabiki, lakini kwa wachezaji wenyewe wakiwa na timu zao chini ya klabu, wanaona kazi ya kina Ulimwengu na Samatta na kweli wanajifunza kwamba wako tayari kuwa washindani?

Inawezekana kabisa mchezaji akawa anacheza nyumbani na kuonekana ni mshindani wa yule anayecheza nje ya nyumbani. Mfano mzuri Ahemd Musa wa Nigeria, alianza kupata namba akiwa anacheza nyumbani licha ya Super Eagles kuwa na nyota wengi wanaocheza nje ya Afrika. Sasa yuko CSKA Moscow na tegemeo la nchi yake.

Nani anathubutu kuwa mpinzani wa Samatta na Ulimwengu hapa nyumbani. Ikiwezekana siku moja apate timu nje lakini hata kama bado, ndiye aonekane mbadala wa wawili hao na siku moja wakija wakae benchi huku yeye akiisaidia Stars kupata ushindi.

Hili ni jambo ambalo hata Kocha wa Taifa Stars, Charles Boniface Mkwasa na msaidizi wake, Hemed Morocco wanapaswa kuliangalia kwa maana ya kuwa na kikosi kipana zaidi chenye kulenga kupambana kwa muda mrefu.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic