October 24, 2015

KIKOSI HIKI CHA TOTO AFRICAN KINA VIJANA SITA KUTOKA SIMBA B, MMOJA AKIWA ALIWAHI KUCHEZA SIMBA KUBWA.

Na Saleh Ally
SIMBA ni moja ya timu inayojitahidi sana katika suala la ukuzaji wa wachezaji vijana. Ndiyo maana timu yake ya vijana ilikuwa maarufu sana.


Simba B ilikuwa ikifanya vema katika michuano mingi miaka mitatu iliyopita na ikaendelea kuwa gumzo kubwa baada ya kufanikiwa kutwaa ubingwa wa Kombe la Banc ABC.

Michuano hiyo, Simba pekee iliamua kupeleka timu ya vijana huku timu nyingine kama Azam FC na Mtibwa Sugar zikiwa na vikosi vikubwa lakini vikaambulia vipigo, Simba B ikawa bingwa.

Unaweza kushangazwa na namna ambavyo Simba imekuwa ikisumbuka kipindi hiki kusajili wachezaji kama Pape N’daw kutoka Senegal ambaye badala ya kucheza soka, amechukua umaarufu katika masuala ya ushirikina.

N’daw hadi sasa hajapiga hata shuti moja kali kwenye lango la timu pinzani lakini Simba imetoa lundo la fedha, zaidi ya Sh milioni 50 hadi kukamilisha kila kitu cha N’daw.

Timu ya watoto ya Simba, pia imepoteza mwelekeo na ajabu zaidi, utaona wachezaji wengi wa Simba ambao walikuwa katika timu yake ya vijana ndiyo wanaofanya vizuri katika timu nyingine za Ligi Kuu Bara.

Achana na kwamba Simba imekuwa ikiwaacha wachezaji wanaonekana wazuri, kila wanapotoka Simba wanafanya vizuri sana. Wachezaji wawili, Amissi Tambwe aliyekwenda Yanga na Elius Maguli ambaye sasa anakipiga Stand United na ndiye anaongoza kwa kufunga mabao.

Simba imekuwa na mwanzo mzuri kwa timu zake za vijana lakini mwendelezo ni hovyo kwa kuwa viongozi wanaonekana kuwa ni wenye papara sana.

Ndiyo maana wachezaji wengi ambao huenda wangekuwa msaada mkubwa kwa Simba, wanakwenda katika timu nyingine na huenda hapo baadaye Simba italazimika kuwanunua kwa fedha nyingi kuwarudisha nyumbani.

Kuna wachezaji wachache ambao Simba ilifanikiwa kuwabakiza, mfano Jonas Mkude, Said Ndemla na Ramadhan Singano ‘Messi’ ambaye aliamua kuhamia Azam na kuachana na Simba.

Bado Simba ingeweza kuwakuza zaidi wachezaji waliokuwa katika kizazi cha Ndemla ambao nina uhakika misimu miwili ijayo, Simba italazimika kuwatafuta na kuwanunua kwa fedha nyingi.

Ukienda Majimaji utakuta zaidi ya vijana wanne, wengine wapo kwenye kikosi cha Toto Africans kilichofungwa na Yanga kwa mabao 4-1 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, kilionyesha soka safi sana na kuwapa Yanga wakati mgumu.

Tatizo kubwa likaonyesha wachezaji wake hawakuwa na uzoefu. Kikosi chake cha kwanza kilikuwa na wachezaji sita kutoka Simba B ambao msimu uliopita waliamua kuondoka baada ya kuona Simba B haieleweki au hakukuwa na mpango wa kuwapa nafasi ya kupanda.

Wachezaji hao Japhet Makaray ‘Balotelli’, Carlos Protus, Miraji Madenge ‘Sheva Go’, Abdallah Seseme, Hassan Khatibu na Edward Christopher ‘Edo’ walionekana kuwa msaada mkubwa kwa Toto ambao wako katika nafasi ya 10, utaona safu yake ya ulinzi inaongozwa na Protus na imefungwa mabao saba, mshambuliaji Sheva Go, pia ni tishio na uliona alivyokuwa akiwahangaisha akina Kelvin Yondani na Vincent Bossou.

Kiungo Seseme ambaye ndiye alikuwa anashika nafasi ya pili kupiga pasi ndefu baada ya Athumani Iddi ‘Chuji’ pia alikuwa moto kwa Yanga.

Si rahisi timu imtumie kila mchezaji iliyemkuza lakini Simba inatumia asilimia 9 tu ya wachezaji inaowakuza na mwisho hawaifaidishi kwa lolote kwa kuwa hakuna mipango ya muda mrefu ya mwendelezo wa wachezaji hao.

Hata kama watakuwa wanaondoka, suala la Simba imefaidika vipi lina maswali mengi. Inaonekana wazi haiwezekani kabisa kwani wanaondoka zao tu wanavyotaka au wasivyotaka kutokana na kuona mambo hayaendi vizuri, lakini Simba haifaidiki.

Simba ni timu inayojitahidi kuwa na timu ya vijana, lakini suala la timu hiyo linaonekana si mpango wenye malengo ya mwendelezo wa kibiashara na kupata faida. Ndiyo maana inaweza kuwaacha wachezaji waende na baadaye kuwanunua.

Angalia mshambuliaji kama Madenge ‘Sheva Go’, Simba ilihitaji kuwa naye kwa maana ya kumpa uzoefu. Baadaye awe tegemeo, lakini kesho utasikia ametua Yanga au Azam halafu anakwenda kuwa tishio Simba ambayo iliona hana lolote jambo ambalo uongozi unapaswa kulitupia macho ya kitaalamu na si kufanya mambo kama ni sehemu ya kujifurahisha tu.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic