September 1, 2017


KIUNGO wa zamani wa Yanga, Abdi Kassim Babi au Ballack wa Unguja ni mmoja kati ya wachezaji wenye heshima katika medani ya soka Tanzania kutokana na kutengeneza rekodi nyingi alipokuwa akitamba kwenye timu mbalimbali. 
Babi ambaye ni nyota wa zamani wa Taifa Stars na Zanzibar Heroes, anakumbukwa kwa kuandika rekodi ya kuwa mchezaji wa kwanza kufunga bao kwenye Uwanja wa Taifa wakati ukifunguliwa mwaka 2007. 

Kiungo huyo alifunga bao hilo akiwa umbali wa mita 35 katika mchezo wa kirafiki dhidi ya timu ya taifa ya Uganda ambao uliopigwa Septemba Mosi, 2007 na Taifa Stars kushinda 1-0. 
Mbali na rekodi hiyo, kiungo huyo anakumbukwa na mashabiki wa Azam FC kwa rekodi yake ya kufunga bao la kwanza kwa timu hiyo katika mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Al Nasri ya Sudan uliopigwa Februari, 2013 kwenye Uwanja wa Taifa. 

Mpaka sasa kiungo huyo mwenye uwezo wa kupiga mashuti makali nje ya eneo la 18 ameshazitumikia timu tofauti ambapo alianzia kwao alipozaliwa kisiwani Pemba katika timu ya Vikokotoni mwaka 1995 hadi 1999 kabla ya kuhamia Mlandege FC msimu wa 2002/03, mwaka 2004 alijiunga na Mtibwa Sugar ya Morogoro. 

Mtibwa alidumu mpaka 2007 kabla ya kujiunga na mabingwa wa msimu uliopita, Yanga kuanzia mwaka huo hadi 2010, mwaka 2011 aliondoka nchini na kutimkia Vietnam katika timu ya Don Tam long An ambayo hakuweza kudumu nayo kwani mwaka huohuo alirejea nchini na kutua Azam FC, kisha KMKM na baadaye UitM FC ya Malaysia. 
Babi ambaye kwa sasa yupo Zanzibar akiichezea timu ya mtaani kwao, Jang’ombe Boys, amefanya mahojiano maalum na Championi Ijumaa kuhusiana na usajili wa vikosi vya timu za Simba na Yanga kwa ajili ya msimu huu. 

Kiungo huyo ameanza kwa kusema kuwa hategemei kuona Simba ikifanya makubwa katika ligi ya msimu huu kutokana na kujaza mastaa kibao ambao kila mmoja amekuwa na majivuno kwa mwenzake tofauti na wapinzani wao waliosajili timu ya kazi ambayo haijabeba majina makubwa. 
“Kwanza kabisa Yanga nimecheza kwa muda mrefu na bahati nzuri, wakati wanaenda Pemba kuweka kambi kabla ya kucheza na Simba, walipita hapa Unguja na nikacheza nao nikiwa na Mlandege ambao waliniomba kuwasaidia.

“Unajua hizi timu kwanza kinapofika kipindi cha usajili wanakuwa na presha kubwa kwa sababu kila mtu anataka kujua mwenzake amesajili wachezaji gani na baada ya hapo huwa kunakuwa na vikao vya propaganda kwa kuangalia itikadi za wachezaji hao.
“Sasa ukiangalia Yanga, wao wanatakiwa kuwa makini sana katika kutengeneza timu yao icheze kitimu kwa sababu wachezaji wao wengi hawana uzoefu wa mechi kubwa kwa maana ya kucheza ligi ya Bara kwa muda mrefu.

“Lakini ukiangalia Simba ina wachezaji wazoefu, mchezaji kama John Bocco, Haruna Niyonzima, Emmanuel Okwi wote hao ni wazoefu ambao wanaweza kuwa msaada kama watajitambua.
“Mchezaji kama Bocco tayari ameshakuwa mkubwa na ana jina na hata hao waliobaki pia wapo hivyo kutokana na sehemu walizokuwa wakicheza awali.

“Najua watu wengi wamekuwa wakiamini kwamba Simba msimu huu itafanya vizuri kwa kuwa wachezaji wake wengi ni wakubwa, pia wanaielewa ligi ya hapa.

“Binafsi hayo ni mawazo na mitazamo yao hakuna anayeweza kuwakatalia lakini ukiangalia kwa upana zaidi Simba ipo katika wakati mgumu zaidi tofauti na huko nyuma.

“Naamini wachezaji wao hawatakuwa wanajituma kwa sababu kikosi chao ni kikubwa, hilo siyo tatizo kubwa sana, ila tatizo zaidi ni wao kushindwa kufanya kile ambacho mashabiki wanakifiria na ndiyo maana nasema kwamba Yanga wana asilimia kubwa ya kufanya vizuri kwa sababu wachezaji watakuwa wanang’ang’ania namba.


KIVIPI WAKATI SIMBA INA WACHEZAJI WAZOEFU?
“Unajua wachezaji wa Yanga mpaka sasa hakuna mchezaji mwenye uhakika wa namba ya kudumu ndani ya kikosi chao tofauti na Simba ambao wachezaji wao hawatakuwa na mpango wa kung’ang’ania namba kwa sababu wengi wao wanatambua wamekuja kucheza kwa maana wana uhakika wa namba.
“Hiki kitu utakuja kukiona baadaye siyo sasa, timu itashindwa kujimudu kwa sababu tayari ina wachezaji wafalme tangu walipotoka, sasa kila moja atahitaji acheze mwenyewe na siyo kitimu, angalia Bocco, Niyonzima na Okwi sehemu walizotoka walikuwa kwenye daraja gani.
“Ukiangalia kitakwimu hilo lipo wazi kuwa Simba ina safari ndefu katika msimu huu tofauti na Yanga ambayo imesajili wachezaji wa kawaida na wanaweza kufanya maajabu makubwa msimu huu,” anasema Babi.

5 COMMENTS:

  1. Kassim uchambuzi wako ni wakishabiki Sana.Simba inachotafuta ni combination ya mastrikers Tu Nani apangwe na Nani wafunge magoli mengi.Yanga ya Leo itakosa morali Kwa wachezaji upande wa kiuchumi,Manji alikua ndio kilakitu pale.sasa hayupo tena.Mpira wa leo ni mkwanja Kaka.Usajili si ishu Sana Simba ishu nikua na uhakika wa huduma Kwa kila mchezaji Kwa wakati na Muda sahihi.

    ReplyDelete
  2. Kassim uchambuzi wako ni wakishabiki Sana.Simba inachotafuta ni combination ya mastrikers Tu Nani apangwe na Nani wafunge magoli mengi.Yanga ya Leo itakosa morali Kwa wachezaji upande wa kiuchumi,Manji alikua ndio kilakitu pale.sasa hayupo tena.Mpira wa leo ni mkwanja Kaka.Usajili si ishu Sana Simba ishu nikua na uhakika wa huduma Kwa kila mchezaji Kwa wakati na Muda sahihi.

    ReplyDelete
  3. We kweli bado sasa yanga Kwan c klabu mbona unaongea bila logic ?ooh nan hayupo wakat mwingine huwa napata hofu na wa2 wanaotoa coment!!

    ReplyDelete
  4. Simba hakuna kugombania NAMBA , yeyote atakayepangwa kati ya waliosajiliwa NI mtambo

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic