KAMA inavyojulikana, mashindano yote ya kimichezo,
ikiwemo Ligi Kuu Bara, yamesimamishwa kwa muda kupisha janga la Virusi vya
Corona, linaloendelea kuitesa dunia kwa kasi kubwa.
Tumeshuhudia
baadhi ya watu maarufu wa Tanzania wakibainika kuwa na Virusi vya Corona,
akiwemo msanii wa Bongo Fleva, Mwana FA na Meneja wa Diamond Platnumz, Sallam
SK.
Kipindi hiki
ambacho ligi imesimama, kama wachezaji wasipokuwa makini, wanaweza kurejea
uwanjani wakiwa na viwango duni.
Hiki siyo
kipindi cha wachezaji kujisahau. Na kama wakithubutu kufanya hivyo, basi
kutakuwa na anguko kubwa sana katika viwango vya soka mara ligi itakaporejea.
Wakati ligi
zikiwa mapumzikoni na timu nyingi zikiwa zimevunja kambi, kwa wachezaji
wanaojielewa, huu ni muda wa kufanya mazoezi ya binafsi kila siku ili kutunza
kiwango chao.
Huku wakiwa
wamejitenga kutokana na mlipuko wa virusi vya Corona na wakiepuka mikusanyiko,
huu ni wakati wa wachezaji kuendelea kujenga stamina zao na kuboresha zaidi
viwango vyao kwa mazoezi makini.
Shida ya
baadhi ya wachezaji wa Kibongo, hii kwao ndiyo fursa ya kujirusha na kusahau
kabisa mambo ya kimichezo, kama kuna mchezaji atafanya hivyo ajue kabisa
anajimaliza mwenyewe.
Mchezaji makini
hawezi kusahau mazoezi katika kipindi hiki.
Atahakikisha anafanya mazoezi kwa
nguvu zaidi kwa kuwa hakuna mechi ya kimashindano ya kucheza, na tunajua kwamba
kama hakuna mechi, maana yake inatakiwa zifanyike juhudi za ziada kulinda
kiwango.
Mchezaji
anapocheza ndiyo hulinda kiwango, lakini asipocheza, maana yake anatakiwa
afanye mazoezi ya ziada ya kulinda kiwango.
Mpira siyo
kama baiskeli kwamba ukishaelewa kuendesha, hata usipoendesha miaka 20, siku
ukiendesha hautaanguka.
Mpira ni
sayansi, ili uwe bora, unatakiwa kufanya mazoezi sana.
Hivyo ndivyo, tumekuwa
tukishuhudia kila siku kwa akina Lionel Messi na Cristiano Ronaldo, Mbwana
Samatta na wengine, wanapokuwa katika mapumziko, hawasahau mazoezi, licha ya
kuwa wana vipaji vikubwa.
Utaona mfano
kwa sasa Ronaldo amejitenga kwao Ureno akiwa na familia yake, lakini kila siku
amekuwa akijifua zaidi na zaidi.
Mchezaji
hauwezi kuwa bora kama hautafanya mazoezi, hata kama una kipaji cha namna gani.
Mazoezi ni lazima.
Wachezaji
wasipofanya mazoezi kipindi hiki, wakaishia kufanya anasa tu, ligi
itakaporejea, tutashuhudia wengi wao wakiwa chini ya viwango, maana yake
tutakosa soka la kuvutia katika ligi yetu.
Hatutaki hilo
litokee, tunataka kuona soka likichezwa kwa kiwango cha juu. Siri ni kutokulala
wakati huu wa mapumziko, ukilala ujue kuwa na soka lako litalala.
Corona isiwe
sababu ya kuua kipaji chako, kuna namna ya kufanya ili kukilinda kipaji
ulichonacho, ili kuendelea kuwa hazina kubwa kwa taifa.
0 COMMENTS:
Post a Comment