September 9, 2020

 


KWA kasi ya msimu wa 2020/21 ilivyoanza nina amini kwamba tutashuhudia mambo mengi sana hasa ndani ya uwanja.

Inapendeza kuona namna ambavyo timu zinafanya vizuri ndani ya uwanja katika kutafuta matokeo. Kwa namna ambavyo Ligi Kuu Tanzania Bara imeanza inavutia.

Itakuwa vizuri ushindani huu ukiendelea mpaka mwisho wa msimu. Sio kwa kuwa ni mwanzo basi timu zikakamia mwanzo kisha mwisho zikajisahau haitapendeza.

Muda uliopo sasa ni kila timu kupambana na kuendelea kujiandaa kwa mechi ambazo ipo nazo mbele kwani safari ndo kwanza inaanza.

Ninaona kwamba mashabiki nao pia wapo mbele kwa kujitokeza ndani ya uwanja. Hakika mnastahili pongezi hapahapo mliposhika endeleeni wala msirudi nyuma.

Septemba 6 na 7 baada ya mechi 9 kuchezwa kukamilisha mzunguko wa kwanza tumeshuhudia mashabiki wakijitokeza kushangilia timu zao wanazozipenda.

Dakika 90 ni muda sahihi uwanjani na unatatosha kuwapa burudani mashabiki na kushuhudia uwezo wa wachezaji wao ambao wapo baadhi ni wapya baada ya dirisha la usajili kupita.

Ukiachana na mashabiki kujitokeza kuwaona wachezaji wao pia wanahitaji ile ladha ya soka iwe endelevu yaani tamu mwanzo mwisho bila kuharibiwa na maamuzi ya waamuzi.

Ili waamuzi wasiweze kuboronga katika kutoa ile ladha kazi yao iwe moja tu ndani ya uwanja, kufuata sheria 17 za mpira.

Kwa kufanya hivyo mashabiki wetu ninawatambua linapokuja suala la haki wanaelewa sana na wanapenda kuona timu zao zinashinda kwa uhalali kabisa.

Nakumbuka kuna shabiki aliwahi kuniambia kwamba ni kheri timu yake ikafungwa kwa uwezo ama ikashinda kwa uwezo ila sio kwa mabao ya kuonyesha kwamba wamebebwa huwa inamnyima usingizi.

Kweli maamuzi ya waamuzi wakati mwingine huwa yanakuwa tofauti ndio maana tunaona msimu uliopita wapo ambao waliadhibiwa kwa kufungiwa mechi kadhaa na wengine walipewa onyo.

Kwa msimu huu mpya, yale yaliyopita kwa waamuzi kufungiwa ama kupewa adhabu hatuhitaji kuskia tunataka kuona mwamuzi baada ya mchezo naye awe anapewa pongezi.

Tunahitaji kuona kwamba kila mchezaji anatoka ndani ya uwanja akiamini kwamba amepoteza kutokana na makosa ya timu ambayo yamewagharimu na sio kumbebesha lawama mwamuzi.

Kwenye mechi za ufunguzi kelele za hapa na pale huwa hazikosekani lakini zifungue mwanga kwa waamuzi waweze kuangalia pale ambapo wanakosea ili wajifunze zaidi.

Makosa yapo kwa kila mmoja kuanzia wachezaji, waamuzi, mashabiki mpaka wale waokota mipira nao wana makosa yao lakini haitapaswa yawe endelevu lazima yafanyiwe kazi.

Kwa kufanya hivyo na kujifunza zaidi kwa waamuzi kufuata sheria 17. Ikiwa hivyo tutakuwa na ligi bora mfano wake hakuna hata bingwa atakayepatikana atafurahiwa na dunia nzima kwa kuwa kila kitu kiliendeshwa kwa haki.

Ujumbe wangu kwa timu ambazo zimepanda daraja kwa msimu wa 2019/20 zikiwa na uhakika wa kushiriki Ligi Kuu Bara msimu wa 2020/21 zina kazi ya kupambana.

Gwambina FC na Ihefu zimeanza kwa kupoteza bado zina nafasi ya kurekebisha makosa na kufanya vema kwenye mechi zao zinazofuata.

  Dodoma Jiji hawa wameanza kwa ushindi mbele ya Mwadui FC wanapaswa pongezi hata wale waliopoteza pia wanapaswa pongezi kwani wameonyesha ushindani wa kweli.

 Ishu ya kushuka daraja bado ipo hivyo ni muhimu kulitambua hilo wakati ligi ikiwa imeanza kusonga mbele taratibu.

Singida United,Lipuli FC,Ndanda FC,Alliance na Mbao zipo kwenye ulimwengu mwingine wa Ligi Daraja la Kwanza zikijiandaa kurejea tena huku kwenye  ligi.

Jambo la msingi ni kwa kila timu kuweza kutimiza majukumu yake vizuri ndani ya uwanja. Maandalizi mazuri katika kila mchezo yatawapa matokeo chanya.

Kila timu kwa sasa inaweza kupata matokeo chanya hata ikiwa ugenini licha ya kwamba na zenyewe ni ngeni cha msingi ni kukubali kwamba mmeshapanda na mnahitaji ushindi.

Imani yangu ni kwamba baada ya kila timu kucheza mchezo mmoja kuna kitu ambacho kitakwenda kufanyiwa maboresho.

Katika maboresho hayo msisahau kwamba wapo ndugu zenu pale Ligi Daraja la Kwanza nao wanahitaji nafasi hivyo kwa kulitambua hilo nina amini kutawapa nguvu ya kupambana zaidi.

Maisha ya Ligi Daraja la Kwanza tayari kwenu muda wake umeisha kwa sasa pambaneni kuweka rekodi mpya. Iweni kama Namungo namna ilivyoleta ushindani na ilimaliza ndani ya tano bora.

Polisi Tanzania pia nao walifanya vizuri kwa kumaliza ndani ya tano bora ikiwa ina maana kwamba hata nyinyi mnaweza pia. Jifunzeni kwa wale ambao wameweza kufikia hatua ambazo mnazihitaji.

Wachezaji ndani ya uwanja ni muhimu kupambana kwa hali na mali kusaka ushindi ili kuwapa wanachostahili mashabiki wenu.

Kwa kufanya kwenu vizuri ndani ya uwanja kunawapa nguvu mashabiki kuendelea kujitokeza ndani ya uwanja kila iitwapo leo na inapendeza kuona kwamba wameanza kujitokeza kwa wingi.

Sapoti ya mashabiki ndani ya uwanja ni kubwa na ina umuhimu hivyo ili waendelee kujitokeza kwa wingi uwanjani ni lazima matokeo yawe mazuri.

Ikishindikana kwa matokeo ndani ya uwanja basi wachezaji chezeni kwa kuonyesha viwango bora ndani ya uwanja hili pia ni jambo la kuzingatia.

Furaha ya mashabiki inabebwa na ushindi pamoja na kushuhudia ule udambwiudambwi ndani ya uwanja kwa wachezaji kuonyesha uwezo mwanzo mwisho.

Matumaini yangu kutakuwa na ushindani mkubwa kwa timu zote ndani ya ligi pamoja na mashabiki kuendelea kujitokeza kwa wingi.

 

1 COMMENTS:

  1. Mwamuzi atafuataje sheria 17 wakati sheria nyingine hazimhusu mwamuzi kama suala la hali na vipimo vya uwanja?

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic