June 1, 2021

 

LIGI Kuu Tanzania Bara kwa msimu wa 2020/21 inaelekea ukingoni, ambapo kufikia sasa timu nyingi tayari zimefanikiwa kucheza michezo 29 au 30 na chache zikiwa na michezo michache ya hiyo.

 

Hivyo kwa idadi hiyo ya mechi, timu nyingi zinasaliwa na michezo minne au mitano tu kutamatisha ligi ya msimu huu.

 

Katika hali kama hii, tayari viongozi wa timu mbalimbali wameanza kuweka nguvu katika mipango ya kuboresha vikosi vyao kupitia dirisha kubwa la usajili, ambalo linatarajiwa kufunguliwa mara baada ya kuisha kwa msimu huu.

 

Kwa kawaida usajili wa dirisha kubwa huwa mkubwa kwa ajili ya kujenga upya au kuboresha vikosi vya timu mbalimbali, tofauti na ule wa dirisha dogo ambao ni mahususi kwa ajili ya kuzisaidia klabu kufanya maboresho ya vikosi vyao, kutokana na tathimini ya mapungufu ambayo yameonekana katika michezo ya mwanzoni mwa msimu.

 

Dirisha hili halilengi kuwasaidia wale tu ambao wamepitia katika kipindi kigumu kwa msimu huu wa 2020/21, bali hata zile timu ambazo zinakuwa na mpango wa kutwaa ubingwa kwa msimu ujao wa 2021/22, na hata kuanza maandalizi ya michuano ya kimataifa kwa msimu ujao ambapo tunatarajia kuwa na wawakilishi wanne.

 

Kwa umuhimu huu, ni wazi kwamba hakuna anayepaswa kufanya masikhara na kuuchukulia usajili huu kama kichaka cha mchezo wa bahati nasibu ‘kubeti’, kwani kwa kufanya hivyo watakuwa wanajiweka katika hatari kubwa ya kupoteana kwenye michuano ya msimu ujao.

 

Mifano mingi kuhusu jambo hili ipo, kwa uchache tu nawakumbusha kuihusu klabu ya Coastal Union, ambao licha ya kuwa na kikosi kizuri na mafanikio makubwa msimu uliopita, msimu huu hali yao imekuwa dhoofu na isiyotabirika.

 

Hii ni kutokana na ukweli kuwa Coastal waliruhusu kuondokewa na wachezaji muhimu, na waliowapa mafanikio msimu uliopita kama vile aliyekuwa nahodha wao, Bakari Mwamnyeto (Yanga), Ayoub Lyanga (Azam) na Ibrahim Ame (Simba), huku wakishindwa kufanya usajili mkubwa wa kuziba mapengo yao.

 

Coastal hawakuwa pekeyao katika makosa haya, lakini nimewataja kama mfano ili kuzikumbusha klabu nyingine funzo hili linalopaswa kuchukuliwa na klabu zote zitakazoshiriki Ligi Kuu msimu ujao.

 

Kama kuna timu inajiandaa kufanya usajili ndani ya kipindi hiki cha dirisha kubwa, inapaswa kwanza wajiridhishe juu ya tathimini ya mapungufu ya kikosi chao, na pia kukusanya taarifa za kutosha kuhusiana na nyota wapya wanaotaka kuwasajili ‘scouting’.

 

Usajili haupaswi kuendeshwa kwa mihemko kama ambavyo imekuwa ikifanywa mara nyingi na klabu zetu hasa zile zilizobadilishiwa majina na kuitwa klabu kubwa, ambao imefika wakati husajili mchezaji eti kwa sababu alitajwa kuwa na uelekeo wa mpinzani wake.

 

Hali hii humpa wakati mgumu kocha kutokana na kuwa na rundo la wachezaji ambao hakuwapendekeza, na ambao hawakidhi matakwa yake kiasi cha kuwasotesha benchi.

 

Kama ni kweli tunahitaji maendeleo basi ni lazima tuhakikishe tunaondokana na tabia za kufanya mambo kwa kubahatisha kwani mtazamo huu hauna afya chanya kwa soka letu.


Uchambuzi wa Edibily Lunyamila, unaweza kuusoma uchambuzi huu kupitia gazeti la michezo la Championi Jumatatu, linalotoka kila Jumatatu.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic