September 19, 2014


UKIZUNGUMZIA suala la uwezo uwanjani kwa mshambuliaji wa Simba, Emmanuel Okwi, haliwezi kuwa suala lenye maswali mengi kwa kuwa jibu lake litapatikana kwa urahisi sana.


Okwi ana uwezo mkubwa, achana na zile taarifa za kwamba amekwisha, Okwi wa mwaka jana si wa mwaka huu au vinginevyo. Mchezaji anaweza kuamua awe katika kiwango kipi na wakati upi.

Inajulikana vitu vipi vinavyoweza kumfanya mchezaji awe bora, hili pia litakuwa linamhusu Okwi na hakika haliwezi kuwa jambo geni kwake, kwamba amelisikia jana.

Lazima mchezaji afanye mazoezi ya kutosha ambayo yamepangiliwa kitaalamu, ndiyo maana klabu zinaajiri makocha bora kwa ajili ya timu zao.

Baada ya kazi ya kocha, mchezaji ndiye anatakiwa kujilinda ili kuhifadhi mazoezi aliyopewa na mwalimu au walimu wake. Kuna mambo anatakiwa asifanye ili aendelee kubaki fiti.

Suala la starehe hakuna haja ya kuficha, ngono, uvutaji sigara, ulevi kupindukia na kutojipatia muda wa kutosha wa kupumzika ni tatizo.

Iwapo mchezaji hatafanya mazoezi halafu atake kung’ara ni kichekesho au afanye mazoezi halafu ashindwe kujitunza ni kichekesho kingine.

Hivyo, Okwi pamoja na kwamba ana kipaji, lakini lazima ajue kuwa anatakiwa kuwa makini na hayo niliyoyaeleza na hakuna ubishi akifikia hivyo na kwa kipaji alichonacho, basi ana uwezo wa kusumbua hapa nchini na nje ya mipaka.

Maana ya kueleza haya ni kwamba, suala la kusema Okwi amekwisha ni lake, anaweza kuamua asiwe hivyo au awe hivyo. Yeye ndiye mwenye uamuzi wa mwisho.

Kilichonivuta kuandika Hoja Yangu leo ni suala la mashabiki. Wale wa Yanga ambao wana hasira naye kwa kuwa ana mgogoro na klabu yao, wamekuwa wakimbeza lakini kitu kizuri hakuna anayemtupia kashfa zaidi ya ule utani wa watani wa jadi.

Msemo wa “Okwi mwisho Chalinze, mjini kila mtu Jaja” umezagaa kwa kasi ya kimondo katika mitandao mbalimbali hadi vyombo vingine vya habari, hali iliyosababisha Okwi naye kujibu mapigo kupitia Mtandao wa Kijamii wa Facebook.

Okwi ameapa kwamba wanaomdharau, siku itafika na watafuta msemo huo. Ni jambo zuri kwa kuwa analenga kufanya vizuri, lakini kuna mambo muhimu ya kuangalia kwake.

Wachezaji hawawezi kufurahi kucheza mechi bila ya mashabiki na timu haina maana kama itakuwa inacheza na mashabiki wake tu uwanjani. Ndiyo maana nataka kumsisitizia Okwi kuwa, atambue kuwa mashabiki wapo nao ni familia ya mpira.

Wanasema nini kuhusu wachezaji au yeye, hilo ni suala jingine ila wana haki ya kuanika hisia zao na mfumo wao unapishana na mfumo wa wachezaji lakini mwisho vyote viko ndani ya mpira.



Mashabiki watakuwepo tu na Okwi hapaswi kupania kucheza vizuri zaidi kwa ajili yao. Kuna mawili, anaweza kufanikiwa au kufeli na kauli yake ya kwenye Facebook inajenga dalili zote kwamba ‘amepaniki’.

Akiendelea hivyo, itazidi kumfanya ‘apaniki’, badala yake anatakiwa kuonyesha kweli yeye ni ‘professional’, aelekeze nguvu zake uwanjani badala ya jukwaani. Kwani kama masikio yake yatakuwa jukwaani badala ya uwanjani, atafeli.

Wachezaji walioweka nguvu zao nyingi kwenye ushindi uwanjani, huwa hawana habari na mashabiki, hawahitaji kuzungumza kuhusu wao na badala yake ni vitendo tu.

Kutoa hisia ni jambo zuri, unaweza pia kusema alichokifanya Okwi si kibaya sana. Lakini pia anatakiwa kutotupia nguvu nyingi walipo mashabiki na badala yake nguvu uwanjani na malengo ya kufanikiwa.

Bado Okwi ana nafasi ya kufanya vema kuliko wengine wanavyoamini. Haina ubishi, kuwa makini zaidi na malengo ya mafanikio, ndivyo vitakavyomfanya ashinde vita dhidi ya wanaotaka afeli.





0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic