September 19, 2014


Mshambuliaji mpya wa Yanga, Geilson Santos ‘Jaja’, amempiku kwa mara nyingine mshambuliaji mpya wa Simba, Emmanuel Okwi, safari hii ikiwa ni katika mshahara wa mwezi.


Siku chache zilizopita, Jaja amekuwa ndiye mchezaji gumzo zaidi hasa baada ya kufunga mabao mawili wakati Yanga ilipoivaa Azam FC na kuitwanga kwa mabao 3-0 kwenye mechi ya Ngao ya Jamii.

Umaarufu huo wa Jaja ulifanya amfunike Okwi huku mashabiki wa Yanga wakiona wamepata mbadala wa kuwapoza baada ya Okwi kurejea Simba, ghafla.

Kwa mara nyingine, Jaja amezidi kung’ara baada ya mshahara wake anaochota kwa mwezi Yanga kuwa unazidi ule wa Okwi kwa dola 100 (Sh 168,000).

Simba inamlipa Okwi dola 2,500 (Sh milioni 4.2) na imeelezwa inaweza kumuongeza wakati wa kuingia mkataba mpya.

Yanga inatoa dola 2,600 (Sh milioni 4.4) kwa Jaja ambaye mshahara wake unaendana na ule wa Andrey Coutinho.

Mnyarwanda, Haruna Niyonzima ndiye mchezaji anayeongoza kwa mshahara ‘rundo’ kwa wachezaji wote wa Yanga na Simba kwa kuwa kwa mwezi analamba dola 3,000 (Sh milioni 5).

Wageni wengine ni Hamis Kiiza anayechukua dola 2,500, sawa na Mbuyu Twite, mwenye uraia wa Rwanda lakini akiwa na asili ya DR Congo.

Kwa upande wa Simba, Okwi ndiye anaongoza kwa mshahara huo wa dola 2,500 akifuatiwa na nahodha Joseph Owino anayepokea dola 2,000 (Sh milioni 3.4), anafuatiwa na Paul Kiongera (dola 1,500), halafu Amissi Tambwe na Pierre Kwizera wote raia wa Burundi ambao kila mmoja analamba dola 1,000 (Sh milioni 1.7).

Mishahara ya wachezaji wa Yanga imeonekana kuwa juu zaidi kuliko wale wa Simba na inaonekana Simba ambayo imepata uongozi mpya, inaanza kujipanga.

Kabla ya kuingia kwa uongozi mpya, wachezaji wa Simba walikuwa wakipokea mishahara ya chini zaidi lakini tayari wameanza kujitutumua.

Yanga walianza kuboresha mishahara ya wachezaji wao mapema na wamekuwa wakisisitiza wataendelea kufanya hivyo.

Timu hizo kongwe mbili na Azam FC ndizo zinaonekana kuwa na mishahara mikubwa kwa wachezaji wake wa kigeni na angalau wale wa nyumbani.


MISHAHARA YA WAGENI 10:

YANGA:
1. Jaja               dola 2,600
2. Coutinho        dola 2,600
3. Niyonzima        dola 3,000
4. Twite                dola 2,400
5. Kiiza                dola 2,600

SIMBA:
1. Okwi               dola 2,500
2. Owino               dola 2,000
3. Kiongera        dola 1,500
4. Tambwe        dola 1,000
5. Kwizera               dola 1,000


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic