Mshambuliaji mpya wa Yanga, Geilson Santos ‘Jaja’,
amempiku kwa mara nyingine mshambuliaji mpya wa Simba, Emmanuel Okwi, safari
hii ikiwa ni katika mshahara wa mwezi.
Siku chache zilizopita, Jaja amekuwa ndiye mchezaji
gumzo zaidi hasa baada ya kufunga mabao mawili wakati Yanga ilipoivaa Azam FC
na kuitwanga kwa mabao 3-0 kwenye mechi ya Ngao ya Jamii.
Umaarufu huo wa Jaja ulifanya amfunike Okwi huku
mashabiki wa Yanga wakiona wamepata mbadala wa kuwapoza baada ya Okwi kurejea
Simba, ghafla.
Kwa mara nyingine, Jaja amezidi kung’ara baada ya mshahara
wake anaochota kwa mwezi Yanga kuwa unazidi ule wa Okwi kwa dola 100 (Sh
168,000).
Simba inamlipa Okwi dola 2,500 (Sh milioni 4.2) na
imeelezwa inaweza kumuongeza wakati wa kuingia mkataba mpya.
Yanga inatoa dola 2,600 (Sh milioni 4.4) kwa Jaja ambaye
mshahara wake unaendana na ule wa Andrey Coutinho.
Mnyarwanda, Haruna Niyonzima ndiye mchezaji anayeongoza kwa
mshahara ‘rundo’ kwa wachezaji wote wa Yanga na Simba kwa kuwa kwa mwezi
analamba dola 3,000 (Sh milioni 5).
Wageni wengine ni Hamis Kiiza anayechukua dola 2,500, sawa
na Mbuyu Twite, mwenye uraia wa Rwanda lakini akiwa na asili ya DR Congo.
Kwa upande wa Simba, Okwi ndiye anaongoza kwa mshahara
huo wa dola 2,500 akifuatiwa na nahodha Joseph Owino anayepokea dola 2,000 (Sh milioni
3.4), anafuatiwa na Paul Kiongera (dola 1,500), halafu Amissi Tambwe na Pierre
Kwizera wote raia wa Burundi ambao kila mmoja analamba dola 1,000 (Sh milioni 1.7).
Mishahara ya wachezaji wa Yanga imeonekana kuwa juu
zaidi kuliko wale wa Simba na inaonekana Simba ambayo imepata uongozi mpya,
inaanza kujipanga.
Kabla ya kuingia kwa uongozi mpya, wachezaji wa Simba
walikuwa wakipokea mishahara ya chini zaidi lakini tayari wameanza kujitutumua.
Yanga walianza kuboresha mishahara ya wachezaji wao mapema
na wamekuwa wakisisitiza wataendelea kufanya hivyo.
Timu hizo kongwe mbili na Azam FC ndizo zinaonekana kuwa
na mishahara mikubwa kwa wachezaji wake wa kigeni na angalau wale wa nyumbani.
MISHAHARA YA WAGENI 10:
YANGA:
1. Jaja dola 2,600
2. Coutinho dola 2,600
3. Niyonzima dola 3,000
4. Twite dola 2,400
5. Kiiza dola 2,600
SIMBA:
1. Okwi dola 2,500
2. Owino dola 2,000
3. Kiongera dola 1,500
4. Tambwe dola 1,000
5. Kwizera dola 1,000
0 COMMENTS:
Post a Comment