February 28, 2015


Wawakilishi wa Tanzania katika Ligi ya Mabingwa Afrika, Azam FC leo Jumamosi wanacheza mechi ya marudiano dhidi ya El Merreikh ya Sudan nchini hapa ikiwa na kumbukumbu ya kushinda mabao 2-0 wiki mbili zilizopita.


Ili kuvuka hatua hii ya awali, Azam inatakiwa itoke sare au ifungwe si zaidi ya idadi ya bao 1-0 au kufungwa kokote kunakofanana na huko na ikishinda itakuwa vizuri zaidi. Mchezo huo utakaochezwa na mwamuzi Wellington Kaoma wa Zambia utachezwa hapa jijini Khartoum, Sudan.

Katika mchezo wa kwanza ni wazi El Merreikh ilikumbana na kitu ambacho haikukitarajia kwani kipigo cha mabao 2-0, kiliwashutua hivyo sasa wana kazi moja ya kuhakikisha hawafanyi makosa kama ilivyotokea katika mchezo wa awali.

Maandalizi ya El Merreikh yameonekana kuegemea zaidi katika safu yao ya ulinzi na Kocha Diego Garzitto ameonekana kuchanganywa na kipigo cha ugenini hivyo anataka kuthibitisha thamani yake katika mchezo wa leo.

Tangu kupoteza mechi yake ya kwanza na Azam, mashabiki wa El Merreikh wamekuwa na shahuku ya kufahamu ubora wa Azam na sababu kubwa ni ipi hadi timu yao ikapoteza mechi hiyo jijini Dar es Salaam kwa mabao 2-0.

USHINDI AU KAZI BASI
Baadhi ya maofisa wa El Merreikh wamelithibitishia gazeti hili kwamba endapo Azam itafanikiwa kusonga mbele na wao kutolewa kuna uwezekano mkubwa, Garzitto akapoteza kazi yake kwani inaonekana uwezo wake utakuwa umeishia hapo katika kuwasaidia.

Katika mazoezi yake kujiandaa na mechi dhidi ya Azam, Garzitto ameonekana akiwasisitiza washambuliaji wake kuwa makini katika eneo la hatari ili kupata mabao mengi ya mapema ili kuidhohofisha Azam itakayokuwa chini ya beki wa kati, Pascal Wawa aliyewahi kuichezea El Merreikh.

“Hatuhitaji mambo mengi sana uwanjani zaidi ya kufanya vizuri na kusonga mbele, kocha ameshaambiwa nini tunachokihitaji kutoka kwake hapo mwanzo hatukuifikiria Azam kama ingeweza kupata ushindi wa aina hii.

“Ni zamani sana sisi kuishia hatua ya awali kwenye michuano hii mikubwa Afrika, ni jukumu la benchi la ufundi kuhakikisha hatufanyi vibaya nyumbani mbele ya mashabiki wetu lukuki, kuna kitu kibaya kinaweza kutokea endapo tutapoteza mchezo huu,” alisema mmoja wa maofisa wa El Merreikh.

Kwa mujibu wa ofisa huyo, Garzitto anaonekana kuyafanyia kazi maneno aliyoambiwa na muda mwingi amekuwa akitoa maelekezo yake kwa washambuliaji wake, Allan Wanga na Mohamed Traore ili waweze kufanya vizuri.

Inaonekana tegemeo pekee la kocha huyo ni Wanga na Traore ambao walikutana kipindi cha pili katika mechi dhidi ya Azam jijini Dar es Salaam na kudhibitiwa vikali na Wawa raia wa Ivory Coast.

WANGA, TRAORE KUANZA
Kwa mujibu wa maofisa wa El Merreikh, Garzitto amepanga kuanza na washambuliaji Wanga na Traore kwa pamoja ili kupata ushindi wa mapema na kumchanganya beki Wawa aliyeonekana kuwa kikwazo kwao katika mchezo wa awali.

“Lilikuwa kosa kumuingiza Traore kipindi cha pili katika mchezo ule wa awali, hapa tatizo lilikuwa kocha kutoifahamu vizuri Azam hasa kuongezeka kwa Wawa kwenye kikosi chao kwani tulipocheza nao kwenye Kombe la Kagame, Wawa tulikuwa naye huku.

“Hakuijua vizuri safu ya ulinzi ya Azam lakini sasa ana kitu cha kufanyia kazi na amesisitiza kumtumia Traore mapema ili kuidhoofisha timu pinzani, kocha anapambana sana kuhakikisha kikosi chake kinafanya vizuri,” anasema ofisa huyo.

Ofisa huyo anasema anafahamu Azam ina faida ya Wawa ambaye si kwamba anawafahamu washambuliaji wa El Merreikh bali ni mzoefu wa soka la Afrika ndiyo maana aliwamudu jijini Dar es Salaam. “Wote wataanza na hata kama Wawa atawazuia, atachoka tu kwani uwezo wake si sawa na wa wenzake katika safu ya ulinzi,” anasema. 

KAZI YA AZAM
Tangu ilipowasili Azam inaonekana kufanyia kazi zaidi ulinzi huku Wawa akionekana kuwa msaada mkubwa wa kutoa baadhi ya maelekezo kwa wenzake kwenye Uwanja wa Jeshi waliofanyia mazoezi jijini Khartoum.

Kitu kimoja muhimu kwa Azam ni kutokubali kuruhusu icheze kwa kujilinda ikiamini mabao mawili iliyopata awali ni mengi na yanayoweza kuwavusha katika hatua ya awali.

“Lengo ni kucheza kwa kujilinda zaidi ili timu isonge mbele na kutopata madhara ugenini hivyo ni lazima tujilinde, lakini kwa akili sana siyo kila mara kwani tunahitaji ushindi pia kuweza kujihakikishia nafasi ya kusonga mbele,” anasema kocha wa Azam, Joseph Omog.

Katika mazoezi ya siku tangu jana ilipowasili hapa, wachezaji wa Azam wameonekana kuwa na furaha muda wote wakiishi kwa kushirikiana kwa kila kitu.

Mchezo huu umekuwa gumzo jijini Khartoum na kila mdau wa soka anataka kuitazama Azam ni timu ya aina gani hadi iweze kuifunga El Merreikh mabao 2-0 nyumbani. Tusubiri dakika 90.

Vikosi vinavyotarajiwa kuanza leo;

Azam; Aishi Manula, Shomari Kapombe, Erasto Nyoni, Aggrey Morris, Pascal Wawa, Michael Bolou, Salum Aboubakari ‘Sure Boy’, Frank Domayo, Didier Kavumbagu, Kipre Tchetche na Brian Majwega.

El Merreikh; Magoola Salim, Kamal Amir, Gafar Ali, Alrayah Maki, Babeker Bakri, Okrah Augustine, Mussa Mussab, Hado Alaa, Traore, Shareif Ramadhan na Wanga.

Fin…

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic