Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) limeahirisha uchaguzi
wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kutokana na mkanganyiko
uliojitokeza katika mchakato wa uchaguzi huo.
Akizungumza na Waandishi wa Habari katika ofisi za TFF
jijini Dar es Salaam leo mchana (Februari 19 mwaka huu), Rais wa TFF, Leodegar
Tenga amesema Fifa imetuma barua ikiagiza mchakato wa uchaguzi usimame baada ya
kupata malalamiko.
Amesema kutokana na mkanganyiko huo, Fifa katika barua yake
ya leo (Februari 19) imeagiza mkutano wa uchaguzi wa TFF ambao awali ulipangwa
kufanyika Februari 24 mwaka huu uahirishwe hadi hapo itakapotuma ujumbe wake
nchini.
Ujumbe huo wa FIFA unatarajiwa kufika nchini katikati ya
mwezi ujao (Machi) ambapo utafanya tathimini ya hali hivyo, kutuma ripoti yake
katika shirikisho hilo na baadaye kutoa mwongozo wa nini kifanyike.
Tenga amewaomba
radhi wajumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF kwa usumbufu uliojitokeza kutokana na
uamuzi huo wa Fifa, hivyo kwa sasa hakutakuwa tena na mkutano huo mpaka hapo
watakapopewa taarifa nyingi.
“Nia yetu ni kuona
watu wanatendewa haki, na nia ya Fifa ni kutafuta ukweli. Hivyo wahusika
(waathirika) wajiandae, watumie wakati huu kuandaa hoja zao ili Fifa wakifika
wawasikilize, wapate maelezo ya kina kuhusu utaratibu na malalamiko
yaliyotolewa,” alisema Tenga.
Tenga amesema timu hiyo ya Fifa itakapofika yenyewe ndiyo
itakayopanga izungumze na nani kwa wakati gani, hivyo ni vizuri waathirika na
vyombo vyote vilivyohusika na mchakato wa uchaguzi wakajiandaa.
“Nataka tubakie kama tulivyokuwa. Malumbano yaishe. Pangeni
hoja, wakija hao waheshimiwa (FIFA) muwaambie. FIFA ni chombo cha juu, nafurahi
wamekubali kuingia katika hili, kwani wana shughuli nyingi wangeweza kukataa,”
amesema.
Kuhusu fursa ya kufanya marejeo (review) kwenye Kamati ya
Rufani ya Uchaguzi inayoongozwa na Idd Mtiginjola ambayo aliielezea Jumamosi,
Rais Tenga amesema kwa vile hicho ndicho chombo cha mwisho nchini katika
masuala ya uchaguzi alishauriwa kuwa kingeweza kufanya review.
“Kwa vile hakuna chombo kingine, nikashauriwa kuwa kinaweza
kufanya review. Katika utaratibu wa kutoa haki, uamuzi ni lazima uwe wa wazi
kwa kutoa sababu. Nilidhani hilo linawezekana, kwani Mahakama Kuu hufanya
hivyo. Kwa hili uamuzi wa Mtiginjola ni sahihi,” amesema Rais Tenga.
Kamati ya Mtiginjola iliyokutana jana (Februari 18 mwaka
huu) ilitupa maombi ya review yaliyowasilishwa mbele yake na waombaji uongozi
watano kwa vile hakuna kipengele chochote kwenye Katiba ya TFF na Kanuni za
Uchaguzi kinachotoa fursa hiyo.
Waombaji hao walikuwa Jamal Emil Malinzi aliyeenguliwa
kugombea urais wa TFF na Hamad Yahya aliyeondolewa kwenye kinyang’anyiro cha
kuwania uenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board).
Wengine ni walioomba kuwania ujumbe wa Kamati ya Utendaji ya
TFF na Kanda zao kwenye mabano; Eliud Peter Mvella (Iringa na Mbeya), Farid
Salim Nahdi (Morogoro na Pwani) na Mbasha Matutu (Shinyanga na Simiyu).
0 COMMENTS:
Post a Comment