April 17, 2013




Na Saleh Ally
MUULIZE mchezaji yoyote anayekipiga sasa kuhusiana na suala la ushirikina na bangi kama ni sehemu ya maisha ya soka ya Tanzania, hatakubali kuelezea kwa kuwa anaona kama atakuwa anatoa siri za ‘familia’.
Jiulize wewe mwenyewe, kwa nini viongozi na wachezaji ambao wako katika mchezo wa soka katika kipindi hiki hawataki kuelezea kuhusiana na mambo hayo mawili wakati wanajua ni tatizo na yanawaathiri.

Majibu yanaweza kuwa mengi, lakini jibu la uhakika ni kwamba, wachezaji na viongozi wengi wa soka wanaabudu ushirikina pamoja na uvutaji wa bangi, maarufu kama sigara kubwa.
Lunyamila na Saleh Ally

Waache waabudu, swali la mwisho je, inawasaidia kufikia mafanikio? Kama inawasaidia wao, Ulaya na kwingine soka ilikopiga hatua wanatumia ushirikina, au wanavuta bangi ili kucheza vizuri? Jibu litakuwa hapana! Hakika inashangaza sana.

Kuna matukio mengi ambayo yamekuwa yakijitokeza hadi kufikia hata wadau hao au viongozi kwenda kukodisha maiti kwenye hospitali kubwa jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kufanya mambo ya ushirikina ili timu ishinde.
Lakini Tanzania imewahi kuwa na wachezaji hodari wengi ambao hauwezi kusema walitengenezwa na bangi au ushirikina, lakini walijulikana kutokana na uwezo wao kama kipaji au mazoezi ya kutosha.


Angalia Edibily Lunyamila, Bakari Malima ‘Jembe Ulaya’, Hussein Marsha, Athuman China, marehemu Said Mwamba ‘Kizota’ na Ramadhani Lenny, Sekiloji Chambua, Mohammed Hussein, nahodha wa zamani wa Simba, Selemani Matola, Mohammed Mwameja.


Wako wengi sana, lakini huwezi kusema uwezo wao ulitokana na ushirikina au bangi, baadhi yao waliofanya mahojiano na Championi Jumatatu wamekiri hilo lipo, lakini hawakutaka kwenda ndani zaidi.

“Kweli ni mambo yanayotokea, imekuwa ni kitu cha kawaida na inatokana na watu kuamini tu. Lakini siamini kama ni msaada, kikubwa ni mazoezi na kujilinda kiafya. Ingekuwa uchawi ndiyo kila kitu, basi lazima Afrika ndiyo ingekuwa inatoa mabingwa wa Kombe la Dunia kila wakati,” anasema Matola aliyeiongoza Simba yenye mafanikio.

“Wakati nacheza, wachezaji wengi waliokuwa wanavuta bangi walikuwa wale wavivu. Hivyo wanavuta bangi kujipa nguvu, wanadai wanaondoa uoga. Lakini mimi nilicheza bila ya kuvuta wala ushirikina na sikuwa muoga,” anasema beki wa zamani wa Yanga na Simba, Malima maarufu kama Jembe Ulaya.

“Ilifikia wakati watu wakaamini navuta kwa kuwa ni jasiri, lakini mimi naona ujasiri ni asili ya mtu. Halafu nilikuwa najiamini sana kutokana na kuwa, nilikuwa nafanya sana mazoezini. Ndiyo maana wachezaji wengi wakienda Ulaya au Uarabuni wanashindwa kutokana na kutokuwa na bangi ya kutosha huko walipo, hivyo wanacheza chini ya kiwango.”

 Matola na Malima ni kati ya wanasoka wa miaka ya 1990 na 2000 mwanzoni waliofanya vizuri sana katika maisha yao ya zamani. Lakini kuna vituko ambavyo msomaji unapaswa kuvijua. Championi Jumatatu lilifanya mahojiano na wachezaji kadhaa wa zamani ambao wanasimulia.
Mmoja ni beki pembeni wa zamani wa Yanga, yeye anaeleza namna walivyowahi kukesha usiku kucha wakifanya masuala ya ushirikina klabu kwao.
“Kulikuwa na lawama kati yetu, wachezaji walilalamika ‘kupigana misumari’, suala hilo likafika kwa uongozi na siku chache baadaye uongozi ukatuita na kusema siku hiyo tutakula na kulala klabuni, jioni wakaja wazee.

“Wale wazee wakasema usiku wana tambiko wanataka kufanya, basi tutakubali na kuanzia kama saa moja usiku akaletwa kondoo. Yule kondoo akawekwa katikati yetu, wakaanza kusoma hadi saa sita usiku. Baada ya hapo tukamwagiwa maji fulani hivi.

“Dakika chache yule kondoo akafa huku tunaona. Usiku saa saba tutashuka kule karibu na uwanja, likachimbwa shimo tunashuhudia na yule kondoo akazikwa. Baada ya hapo tukaanza kumruka na tukaelezwa hilo ndilo tambiko.”

Huyo ni beki huyo wa pembeni wa zamani wa Yanga, lakini mshambuliaji wa zamani wa Simba naye anakiri hivyo kwamba kweli, bangi na ushirikina ndiyo rafiki mkubwa wa timu karibu zote zinazoshiriki Ligi Kuu, Ligi Daraja la kwanza na hata zile za mchangani.
“Sisi tulikuwa tumeweka kambi kule Bamba Beach, makamu mwenyekiti wakati huo akaja na kuku we mganga, aliagizwa atamchinja wakati tukipanda kwenye gari na kila mtu amruke. Hivyo kuku akafungwa kamba akalala pale hotelini.

“Siku iliyofuata, wakati tunakaribia kupanda kwenye gari, alipotafutwa kuku akakutwa amekufa. Dah ilikuwa mshikemshike lakini mwisho mechi hiyo ilikuwa dhidi ya Yanga, nakumbuka fainali ya Kombe la Tusker, tukashinda bao 4-1.”

Wakati mshambuliaji huyo anasimulia, beki mwingine wa kati wa zamnai wa Simba anasema waliwaji kupelekwa kwa mganga mkoani Mwanza.
“Kuna mdau mmoja wa Mwanza ndiye alikuwa antupokea, tulipofika tu alitupokea na kusema ameambiwa timu imechezewa, tukachukuliwa na kupelekwa kwa mganga kijijini sana. Nakumbuka anaitwa Mzee Nyumbani. Kila mchezaji alikuwa ana godoro lake na usiku akatupeleka kwenye jiwa refu.

“Mfano kama mbao zinazotumika kurukia kwenye swimming pool. Basi pale wachezaji tukawa tunaserereka nabaadaye akaimba na kuomba mambo yake lakini siku ya mechi dhidi ya Kahama United mjini Kahama, matokeo yakawa suluhu na mechi ilikuwa ngumu.”

Achana na huyo, kuna mchezaji mwingine ameomba jina na timu yake ifichwe gazetini anaeleza yalifanyika mambo ya kishirikina hadi wakatokwa na machozi.

“Huwezi kuamini, mganga alisoma mambo yake hadi kondoo akapoteza nguvu. Baadaye akafungwa sanda kama maiti ingawa alikuwa mzima, usiku huo tukaambiwa kwenda makaburini. Mganga alitaka kaburi jipya, yaani mtu kazikwa siku ile au siku mbili zilizopita.

“Tulipofika kule, akachimba lile kaburi usawa wa kiuno na kumzika yule kondoo, pamoja na kufukia tulimsikia akiendelea kulia. Baadhi yetu wakaanza kutoa machozi, ilikuwa inaumiza sana. Wakati huo mganga alikuwa na paka wake mweusi amemfunga kama kama vile mbwa.”

Inaonekana kuna mambo mengi sana, lakini jiulize kama vitu hivi vina msaada katika soka ya Tanzania. Badala yake inaonekana ni miradi ya wachache ambao hata ikiguswa wanakuwa wakali sana wakihofia riziki zao zinaweza kutoweka. 

Kweli wao wanafaidika, kwani hata wauza bangi wanaingiza mamilioni kupitia wanasoka kama ilivyo kwa waganga wa kienyeji na mwisho wachezaji wa Tanzania, safari yao mwisho inakuwa ni Dar es Salaam.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic