May 18, 2013



 
Julio na Kiiza wakizozana, Saanya anaamua...
Simba itaivaa Yanga katika mechi ya Ligi Kuu Bara, kesho kwenye Uwanja wa Taifa. Awali vyanzo vilielezwa kuwa Israel Mujuni Nkongo ndiye angechezesha mechi hiyo. Baada ya gazeti hili kuweka wazi jambo hilo wiki iliyopita, inadaiwa wahusika wakabadilisha ratiba na kumpanga Martin Saanya wa Morogoro.

Kitendo cha kumbadili Nkongo kimezua malumbano makubwa hadi Simba kutishia kutaka kutocheza mechi hiyo ya kesho kwa madai kuna mpango wa ‘kuwamaliza’.
 
Mzozo unaendelea..
Inaonekana Nkongo ameondolewa baada ya Championi kujua kuhusu yeye na kuandika mapema suala la kwamba aliwahi kumpa kadi nyekundu Haruna Niyonzima wa Yanga na kuzua zogo kubwa katika mechi ambayo nusura ivunjike.
 
Mzozo umehamia kwa Kiggi..
Lakini hakuna anayejua vituko lukuki vya Saanya. Mwamuzi huyo mwembamba kwa umbo, ana mambo mengi ambayo amewahi kuyafanya katika michezo ya Ligi Kuu Bara aliyochezesha na unaweza kuita vituko au viburudisho.

Polisi Dodoma wamchapa makonde
Msimu uliopita alipata kipigo cha nguvu mara baada ya kuchezesha mechi ya Polisi Dodoma dhidi ya Azam kwenye Uwanja wa Jamhuri, Dodoma.

Ilielezwa ‘aliibeba’ Azam na kusababisha Polisi ifungwe bao 1-0, matokeo ambayo yalichangia timu hiyo ishuke daraja. Waliomtembezea kichapo walifanya hivyo wakati alipokuwa kwenye vyumba vya kubadilishia nguo uwanjani hapo.
 
Niyonzima anaamua kuingilia kupoza mambo...
Baadaye Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF) liliwafungia mechi tatu wachezaji waliompiga na faini ya shilingi milioni moja kwa kila mchezaji aliyehusika ambapo walikuwa tisa.


Kocha Azam amlalamikia
Saanya ndiye aliyechezesha mechi ya Ngao ya Hisani kati ya Azam na Simba mwanzoni mwa msimu huu, Simba ilishinda mabao 3-2, lakini aliyekuwa Kocha wa Azam, Bunjak Boris ‘Bocca’ alilalamika kuwa mwamuzi huyo ana uwezo mdogo wa kuchezesha soka.


Bocca alidai Saanya aliinyima Azam penalti mbili na kuipa Simba penalti isiyo halali na kudai kuwa aliichangia ‘kuiua’ timu yake.


Ajichanganya kutoa kadi
Saanya alimpa kadi ya njano kiungo wa Simba, Amri Kiemba, badala ya beki Said Nassor ‘Chollo’ katika mechi dhidi ya Coastal Union miezi mwili iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa ambapo Simba ilishinda kwa mabao 2-1.

Kiemba alimfuata na kumueleza kuwa siyo yeye aliyecheza rafu bali ni Chollo aliyemkwatua Twaha Hussein lakini Saanya hakutaka kumuelewa kabisaa!

Ugomvi wa Julio & Kiiza
Msimu uliopita Yanga ikiwa chini ya Kosta Papic ilisafiri kwenda kucheza Mkwakwani Tanga, Saanya ndiye alikuwa kati.

Mechi ilikuwa na upinzani mkubwa, wakati fulani Kocha wa Coastal Union, Jamhuri Kihwelo ‘Julio’, ambaye sasa ni kocha msaidizi wa Simba alizozana na wachezaji wa Yanga, Hamis Kiiza na Kiggi Makasi.

Saanya alilaumiwa kwa kupoteza muda, kwani badala ya kutumia filimbi, bila ya kujali ana mwili mdogo, alikuwa akilazimisha kuingia katikati ya Julio na Kiiza au Kiggi huku akitumia muda mwingi kuzungumza.

Yanga ilishinda bao 1-0 lililofungwa na Kiiza ambaye alikwenda kushangilia kwenye benchi la Coastal huku akionyesha ishara ya kumziba mdomo Julio. Baada ya mechi, Julio alilalamika kuwa Saanya alichangia kuharibika kwa mchezo huo kwa kuwa aliona matendo mengi ya wachezaji wa Yanga ambayo si ya kiungwana lakini hakuchukua uamuzi.

Coastal v Yanga tena
Pamoja na kwamba ndiye alichezesha mechi kati ya Yanga na Coastal msimu uliopita, TFF ilimpa mechi ya timu hizo mjini Tanga msimu huu tena! Safari hii, Yanga ilishinda kwa mabao 2-1 na Coastal Union wakalalamika kwamba Saanya amekuwa akiwaua kila mechi hasa zile wanazokutana na  vijana hao wa Jangwani.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic