July 10, 2013



 
WANYAMA KAZINI...
 Na Saleh Ally
KIUNGO nyota wa Kenya, McDonald Mariga Wanyama hadi sasa ameweka rekodi ya mchezaji kutoka Afrika Mashariki kucheza ligi kubwa mbili na michuano mikubwa zaidi kwa klabu Ulaya.

Amecheza Italia ‘Serie A’ akiwa na Inter Milan na Parma, halafu Real Sociedad ya Hispania ‘La Liga. Lakini kumbuka alitwaa ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya akiwa na Inter chini ya Jose Mourinho.
 
MARIGA MAZOEZINI NA SJINEIDER WAKATI WAKO INTER..
Mdogo wake, Victor Wanyama, anakipiga katika kikosi cha Celtic ya Scotland. Tayari amekuwa gumzo kwani pamoja na klabu hiyo kumnunua kwa pauni 900,000 tu kutoka Ubelgiji, iliwaambia Man United na Arsenal kwamba inahitaji pauni milioni 25 kumuachia.

Kweli Mariga anatokea katika familia ya mpira, maana baba yake, Noah Wanyama alikuwa winga hatari wa AFC Leopards, wadogo zake wawili Thomas na Sylvester wanacheza Sofapaka na Sony Sugar katika Ligi Kuu ya Kenya. Dada yao mdogo, Mercy ni nyota wa mpira wa kikapu.
 
OLIOECH KAZINI UFARANSA..
Ukiona hivyo, maana yake Mariga na Wanyama wanatokea katika familia ya wanamichezo hasa, ingawa mwisho wanachofanya wanaing’arisha nchi yao.

Kenya sasa ina wachezaji wa kiwango cha kina Mariga, wanaweza kucheza timu moja na wale wa Manchester United, Arsenal, Real Madrid, Barcelona na wanafundishwa na makocha hadi wenye hadhi ya Mourinho!

Tanzania haina mchezaji kabisa ambaye inaweza kujivunia. Awali lilionekana ni tatizo la Afrika Mashariki lakini sasa limebaki na kuwa tatizo Tanzania tu.

Uganda wana wachezaji zaidi ya 20 walio nje ya nchi yao, kati ya hao wapo wanaocheza Ulaya na anayecheza Heart of Midlothian ya Scotland, huyo ni kiungo David Obua.

Tanzania yuko nani, anacheza wapi na kwa sababu gani inakuwa vigumu? Mtu gani ni tatizo au nchi yetu?

Mwaka 2002, Kenya iliifunga Kilimanjaro Stars katika fainali ya Kombe la Chalenji na kubeba kombe mbele ya mashabiki kibao kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza. Kinda Denis Oliech akafunga bao la tatu la ushindi, matokeo yalikuwa 3-2.

Jiulize wachezaji wa Tanzania Bara waliocheza na Oliech wakati ule wako wapi, vipi hata mmoja hakufanikiwa? Lakini Mariga alikuja nchini miaka miwili iliyopita akiiongoza Harambee Stars ambayo ilipata sare ya bao 1-1 dhidi ya Stars.
 MFANO: ANGALIA WANYAMA AKIWA NYUMBANI KWAKE SCOTLAND..



Ukimuangalia uchezaji wake, halafu angalia uchezaji wa viungo wetu wengi, bado utaona wapo wengi wenye uwezo kama wake au zaidi.
Nani anaumia kutaka kujua wapi tunakwama halafu aanzishe safari ya kutafuta suluhisho zaidi ya ukimya?

Viongozi:
Matatizo yanaweza kuwa mengi sana, lakini uwezo wa viongozi pia ni tatizo. Si wale wanaoangalia mbele au wanaokubali mafanikio kwa wengine.

Kwanza hawapo tayari kuzipatia klabu zao maendeleo na kuangalia mfumo wa kukuza vijana. Pia wapo tayari kumuondoa mchezaji anayefanya majaribio au kumzuia asiende ili acheze mechi ya Simba dhidi ya Yanga hata kama tayari bingwa kapatikana.


Mfumo:
Mfumo ni tatizo, hauwaonyeshi wachezaji kwamba wanaweza kwenda mbali zaidi ya kucheza Yanga au Simba ambako wengi wanaamini ndiyo ‘mwisho wa mbingu’.
Bado hawajiamini, hata waliopata nafasi ya kwenda kufanya majaribio UIaya na kufanikiwa, wanaona Simba na Yanga zinatosha au bora wakacheze Uarabuni!

Wachezaji:
Hata wao ni tatizo, kwanza hawana wivu wa maendeleo na hawaumii na kufeli. Asilimia kubwa bado wanaona soka kama sehemu ya kujifurahisha.
Asilimia kubwa hawana tamaa ya kuvuka kutoka walipo na kwenda mbali, ajabu zaidi wengine wanasisitiza siyo kitu kibaya kwao. Inawezekana kwa kuwa hakuna aliyelipia kipaji chake kwa Mwenyezi Mungu, hivyo haoni hasara yoyote.

Inawezekana kabisa hata kwa kuangalia, Mariga na Wanyama si wachezaji bora kuliko wa kwetu, lakini tamaa ya mafanikio na kutaka kutimiza ndoto imewafikisha walipo.

Ukiangalia kwa kina sababu ni nyingi sana. Mfano wa Mariga na Wanyama unakuwa mzuri kwa kuwa Kenya hatuna tofauti nao na wakati mwingine ligi yetu ni bora kuliko yao. Vipi wao wanafanikiwa nasi hakuna kitu!

Lazima kuwe na tabia ya kujipima, hasa kwa kuangalia jirani au mtu wa karibu yako anavyofanikiwa. Basi tuumie na tuamini Tanzania ina wachezaji wa kulipwa wenye uwezo wa kucheza katika nchi zilizofanikiwa kisoka, tujue hiyo ni sehemu ya kuinua soka nchini. Tafakari..!!!






0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic