December 13, 2013




Na Saleh Ally
Kumekuwa na maswali mengi sana kuhusiana na timu zetu za taifa, kwani kila mashindano tumekuwa tunajivunia suala la afadhali na inaonekana wengi tumeridhika nalo.


Wakati timu ya Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars, inakwenda Kenya kushiriki Michuano ya Kombe la Chalenji, hakika nilikuwa nina asilimia 90 kwamba ndiyo yenye nafasi ya kutwaa kombe hilo, nitakupa sababu.

Katika timu zote zilizoshiriki michuano hiyo ambayo imefikia tamati jijini Nairobi, Kili Stars ndiyo ilikuwa na kikosi bora zaidi kuliko nyingine, takwimu zinasema hivyo kwa maana ya vikosi.


Zambia ambao walikuwa wageni, kikosi chao ambacho hushiriki michuano iliyo chini ya Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) na lile la Afrika (Caf), kilikuwa kimevunjwavunjwa. Yaani waliotumika, wengi ni wageni.

Sudan pia ilifanya hivyo na hata wenyeji Kenya pia ilikuwa hivyo. Mfano ingekuwa ni michuano ya kuwania kufuzu kucheza Kombe la Dunia au Mataifa Afrika, basi asilimia 80 ya wachezaji walioshiriki Kombe la Chalenji isingekuwepo.


Badala yake wachezaji kama akina McDonald Mariga, Victor Wanyama, Denis Oliech, Jamal Mohamed na wengine wanaocheza nje ya Kenya, ndiyo wangechukua nafasi.

Kadhalika Uganda, kocha wao, Sredojevic Milutin ‘Micho’, aliamua kuwaita wachezaji wanaocheza Uganda tu huku akichukua wawili kutoka nje ambao ni Hamis Kiiza wa Yanga na Dan Sserunkuma wa Gor Mahia ya Kenya.

Micho aliacha rundo la wachezaji wa nje kwa kuwa anataka kuboresha kikosi cha Chan mwakani huko Afrika Kusini. Ethiopia pia waliamua kuchukua wachezaji wengi vijana kwa lengo la kutengeneza kikosi chao upya. Waliokwenda na vikosi vyao kamili ni Somalia, Kili Stars na Zanzibar Heroes.

Hapa kitu cha kujiuliza ni hiki, kama Kili Stars ilikwenda na kikosi kwa asilimia 95 ambacho kinaunda timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, vipi kimeshindwa kufurukuta dhidi ya vikosi vya pili au vya vijana vya wenzetu?

Taifa Stars imekuwa ikizitoa jasho na ikiwezekana kuzifunga Zambia, Uganda, Kenya tena zikiwa na wachezaji wake wa kikosi cha kwanza ambao wengi hawakuwepo Nairobi.

Kama ni tathmini, kikosi cha Kili Stars ndiyo kilikuwa bora zaidi kuliko vingine, lakini mwisho kimeishia nusu fainali na kufungwa na wenyeji ambao walikuwa na wachezaji wengi ambao hawana nafasi kama akina Mariga wakiwa wameitwa kujiunga na timu hiyo.

Hata ukiangalia au ukapima mchezaji mmoja-mmoja na rekodi za mashindano makubwa, yaani yale ya klabu na timu za taifa chini ya Caf, basi hakuna timu iliyokuwa na wachezaji wenye uwezo kama wale wa Kili Stars.

Ninaona kuna tatizo na linaweza likatokea katika moja ya pande hizi mbili, kwa wachezaji au Kocha Kim Poulsen ambaye nafikiri huu ndiyo ulikuwa wakati mwafaka kwake kufunguka, maana Tanzania kuendelea kubahatisha sasa imekuwa ‘too much’.

Najua Poulsen na wenzake wanalipwa kwa ajili ya kuitumikia Taifa Stars, hakuna kati yao anayeweza kusema anafanya kazi ya kujitolea. Kikubwa kinachotakiwa ni mafanikio na hakuna zaidi ya makombe au kufuzu kucheza michuano mikubwa kama Kombe la Dunia au Mataifa Afrika, ikiwezekana hata Chan.

“Mambo ya ilibaki kidogo tu”, sasa basi. Kama itaendelea basi wakati wa kufunguka na kumhoji Poulsen bila ya woga utafika na hakutakuwa na breki wala woga, muhimu zaidi, maslahi ya taifa mbele.

Ndiyo maana nasema umefika wakati kwa Poulsen kufunguka, kama anaona kuna tatizo, kuna wachezaji wavivu, wasiomsikia, wasiotaka kujituma kwa ajili ya taifa lao, basi awe wazi na afunguke mara moja.

Inawezekana kuna mambo yanaendelea chinichini, labda kuna mgomo baridi, au kuna wachezaji viburi waliovimba vichwa, basi Poulsen aseme na mara moja washughulikiwe ili wajue maana ya utaifa na umuhimu wa kuichezea timu ya taifa.

Lakini kama atathibitisha hakuna tatizo, basi yeye ndiye atakuwa na tatizo na kama ameshindwa kulitatua, basi mara moja Mtanzania mimi nitaanza kulitatua na kutaka mabadiliko.

Kama wapo wanaoona ni sahihi timu kila siku kubakiza kidogo tu kufuzu au kuchukua kombe na wanaacha mambo hayo yaendelee, basi sasa wakati umebadilika na umekwisha, maneno na visingizio sasa basi, tunataka mafanikio.

FIN.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic