February 5, 2014



CHANGA (ALIYESIMAMA)

Mshambuliaji Omary Changa aliyefariki dunia Jumapili iliyopita na Championi likawa gazeti la kwanza kuandika, amezikwa juzi kwenye makaburi ya Mwinyi Mkuu yaliyopo Magomeni, Dar, katika msiba uliohudhuriwa na mamia ya wadau wa soka nchini.

Kifo cha mchezaji huyo wa zamani wa Yanga na JKT Ruvu ambaye mara ya mwisho alikuwa akiichezea Moro United ya Ligi Daraja la Pili, kimepokelewa kwa huzuni na masikitiko makubwa na baadhi ya wadau waliojitokeza kwenye msiba huo.

Baadhi ya watu maarufu waliojitokeza msibani hapo ni pamoja na nahodha wa zamani wa Yanga, Ally Mayay, aliyeonekana kusikitishwa na msiba huo ambapo alieleza huzuni aliyokuwa nayo kwa marehemu.

“Kwa kweli tumehuzunika sana sisi familia ya soka ukizingatia ni mmoja kati ya watu wachache waliokuwa wana uwezo mkubwa wa kucheza mpira hapa nchini, yaani pengo lake halitaweza kuzibika milele, alikuwa ni mtu wa pekee sana kwenye safu ya ushambuliaji,” alisema Mayay.

Kocha Mkuu wa Moro United, Salum Kumbala, naye pia alionyesha kusikitishwa: “Alikuwa msaada mkubwa kwa timu yetu akiwa uwanjani lakini pia alikuwa akiwapa sana ushauri wenzake jinsi ya kufanikiwa katika mpira, tumeondokewa na mtu muhimu sana.” 

Kwa upande wake beki wa Azam FC, Aggrey Morris, ambaye alikuwa msibani hapo, alisema: “Huyu ni mmoja wa wachezaji niliokuwa nawakubali sana ili ndiyo hivyo ametutoka na hakuna atakayekuja kufanya alivyokuwa anavifanya Changa na hiki ni moja kati ya mapengo makubwa kuwahi kutokea kwenye soka hapa Tanzania.”

Pamoja na hayo, kiungo wa Yanga, Nizar Khalfan, pia alielezea hisia zake: “Tumeumia sisi kama wachezaji kwa kumpoteza mwenzetu aliyekuwa na kipaji chenye kuleta dira nzuri tu kwa soka la Tanzania, tutammisi sana.”

Mashabiki, wadau, wachezaji  na makocha walijitokeza kwa wingi kwenye msiba wa mchezaji huyo ambaye mwili wake ulikutwa umetupwa Jangwani jijini Dar es Salaam, wikiendi iliyopita.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic