March 24, 2014




Na Saleh Ally
HAKUNA ubishi, umaarufu wa Ligi Kuu England unatokana na namna ushindani unavyokua kuanzia mwanzo hadi mwisho wa ligi hiyo bila kujali timu ni zipi.


Vipigo vya ‘kufa mtu’ vya juzi huku vikihusisha vigogo kama Arsenal, vimeonyesha kuwa Ligi Kuu England, maarufu kama Premiership, haitaki lelemama na wala si ligi ya kubahatisha.

Timu zilizo kileleni au zinazopambana kuwania ubingwa, yaani Chelsea, Liverpool na Manchester City kila moja imeshinda kuanzia mabao matano kwenda mbele.

Chelsea iliishindilia Arsenal kwa mabao 6-0 na kuacha gumzo ambalo litaendelea kudumu kwa siku kadhaa, Manchester City wakawaminya Fulham na kuzidi kuwadidimiza kwa mabao 5-0 huku Liverpool wakiwatanguliza SAS (Suarez na Sturridge) wakailipua Cardiff kwa 6-3.

Arsenal ndiyo timu pekee iliyo katika nne bora katika msimamo wa ligi hiyo ambayo ilikutana na kipigo cha mabao hayo sita.

Hiyo ni dalili tosha kuwa timu hizo hazina mchezo katika mechi hizo za mwisho, pia ni dalili tosha kwamba kadiri ligi inavyokwenda ukingoni, basi kutakuwa na mambo mengi sana ya kushangaza.


Pamoja na yote hayo, timu tatu tu tayari zimejichuja kuwa ndiyo zinazowania ubingwa wa Ligi Kuu England ambazo ni Chelsea, Liverpool na Manchester City.

Kimahesabu inaonekana Manchester City inaongoza kutokana na asilimia kubwa, ikifuatiwa na Chelsea, Liverpool na Arsenal ambao hata hivyo wamezidi kupoteza mwelekeo tofauti na walivyoanza.

Mchezo wa soka unapendwa kuliko yote duniani kwa kuwa hautabiriki, ukiamini vile wenyewe unaibuka na matokeo tofauti kabisa. Lakini kuna wakati unafikia, lazima mambo yawe hivyo.

Pamoja na kwamba hesabu zinaonyesha Manchester City ina nafasi kubwa zaidi lakini lazima ishinde, hali kadhalika kwa Chelsea na Liverpool, atakayeteleza basi ajue amekwenda na maji.

Kingine ambacho kina ugumu ni hivi, kwamba katika baadhi ya mechi, timu hizo nne zinazowania ubingwa, zitakutana zenyewe kwa zenyewe. Maana yake ugumu wa hesabu utakuwa katika mechi hizo, atakayepoteza, basi anapotea zaidi.

Man City:
Hawa wana nafasi zaidi kutokana na kuwa na michezo mingi zaidi mkononi, wanayo kumi, maana yake inategemea watazicheza vipi karata zao kuhakikisha wanapasi au la.

Hadi sasa wamecheza mechi 28, wamekusanya pointi 63 na wako kwenye nafasi ya tatu. Iwapo watashinda zote kumi, watafikisha pointi 93 ambazo zitakuwa ni za juu zaidi na haziwezi kufikiwa na timu nyingine yoyote.

Kwa pointi hizo, hakutakuwa na timu ya kuwazuia kuwa mabingwa wa England kwa mara ya pili katika kipindi cha misimu mitatu.

Ugumu kwao ni mechi mbili; watakutana na timu mbili kati ya hizo zilizo katika nafasi nne za juu katika msimamo huo; Machi 29 watawavaa Arsenal wakiwa ugenini na Aprili 13 watakaribishwa kwenye Dimba la Anfield kwao Liverpool. Wakivuka hapo, basi wao wanaume wa shoka.

Chelsea:
Kimahesabu wana nafasi ya pili kwa kutwaa ubingwa maana wamecheza mechi 31, wana pointi 69 kileleni mwa ligi, wanachojivunia ni kuwa na pointi nyingi na si michezo mingi.

Wamebakiza mechi saba, wakishinda zote watakuwa na pointi 90 ambazo ni za pili kwa wingi ukilinganisha na Man City wakishinda zote.

Mechi ya vigogo walio katika nne bora, itakuwa Aprili 7 dhidi ya Liverpool kwenye Uwanja wa Afield, wakipita hapo wana nafasi kubwa. Wakipoteza, kutakuwa na walakini na ugumu kwao.

Liverpool:
Wana pointi 65 baada ya kucheza mechi 30 za Ligi Kuu England na wako katika nafasi ya pili kwenye msimamo. Lakini kama ni kutwaa ubingwa, inaonekana wanaweza kufanya hivyo bado.

Unaweza kuwapa nafasi ya ubingwa kwa kuwa katika mechi 30 walizocheza, maana yake wamebakiza nane na wakishinda zote, tayari wana uwezo wa kufikisha pointi 89.

Lakini wana ugumu zaidi kwa kuwa wana mechi mbili dhidi ya vigogo wanaowania ubingwa. Aprili 13 watakuwa nyumbani dhidi ya Man City, hicho ni kimbembe. Halafu Aprili 27 wana Chelsea na ndiyo zinazopewa nafasi kubwa ya kutwaa ubingwa.

Inawezekana Liverpool ikajitengenezea nafasi bora kwa kuwa iko nyumbani na ikizifunga timu hizo mbili, itatibua hesabu zao na asilimia zao za ubingwa, kujitengenezea nafasi bora zaidi badala ya kuonekana kucheza nao ni tatizo kwao.

Arsenal:
Tofauti na ilivyoanza, kasi yake kama kawaida inapungua mwishoni na taratibu wanaanza kupiga ‘rivasi’. Tayari wameyumba ingawa ndiyo timu inayopewa nafasi ya nne kati ya nne zinazowania ubingwa.

Imecheza mechi 30 na kukusanya pointi 62 ikiwa katika nafasi ya nne kwenye msimamo na iwapo itashinda zote nane zilizobaki itakusanya pointi 86.

Ugumu kwake katika mechi nane zilizobaki, moja ni tatizo kwa kuwa watakutana na Man City, Aprili 29. Ndiyo watakuwa nyumbani, lakini wanalazimika kufanya kazi ya kweli kupunguza kasi ya ‘mziki’ wa jamaa hao wa Jiji la Manchester.

Timu yoyote katika ya hizo, ukianza na yenye nafasi ya kwanza hadi ya nne kutwaa ubingwa huo inaweza kuwa bingwa, kinachotegemewa ni umakini na hesabu za uhakika za kumaliza mechi zilizobaki.

Karibu kila timu itakutana na timu nyingine zinazoonekana ni ndogo lakini pia zitakuwa zinapambana kuepuka kushuka daraja. Hivyo, ugumu utakuwa mwanzo mwisho na timu ikifungwa mechi mbili kati ya ilizobakiza, ubingwa isahau.

MSIMAMO WA NAFASI YA UBINGWA:
                  MECHI        POINTI       WAKISHINDA ZOTE POINTI
Chelsea        31               69            (mechi 7) +21                   90  
Liverpool     30               65             (mechi 8) +24                  89
Man City      28               63             (mechi 10) +30               93     
Arsenal         30               62             (mechi 8)   +24          86
  
Premier
                        P      W    D     L      GF   GA   Pts
1. Chelsea      31   21   6      4      62   23   69
2. Liverpool   30   20   5      5      82   38   65
3. Man City   28   20   3      5      76   27   63
4. Arsenal      30   19   5      6      53   34   62

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic