March 28, 2014




Na Saleh Ally
KIPIGO cha mabao 2-1 walichokipata Real Madrid kutoka kwa Sevilla, usiku wa kuamkia jana, ni jibu tosha kwamba wameingia kwenye kipindi kigumu cha matatizo na wakizubaa kidogo, majanga!

Kwa mtazamo wa haraka kama baadhi ya mashabiki wa Madrid walivyoandika kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter kwamba mambo mazuri yanakuja na wasijute na kupoteza, inaweza kuonekana kama ni jambo la kawaida.
Lakini mambo yakiwekwa kwenye mahesabu inaonekana kuwa kuna kila dalili Barcelona inaweza kubeba ubingwa wa La Liga na hasa kama Madrid watashindwa kuliona na kuliamini hilo kuwa linaweza kutokea.
Tofauti au balaa kwa Madrid limeanza baada ya kupoteza pointi sita ndani ya siku tano tu, halafu Barcelona wakaongeza idadi hiyo ya pointi kwa kipindi hicho.
Madrid wamepoteza mechi mbili mfululizo, dhidi ya Barcelona kwa kufungwa mabao 4-3 wakiwa nyumbani kwao, halafu wakafungwa 2-1 na Sevilla wakiwa ugenini. Barcelona wao wakaongeza pointi kuwa sita kwa kuwaadhibu Celta Vigo 3-0.
Kutokana na matokeo hayo, Barcelona wamepanda hadi nafasi ya pili wakiwa na pointi 72, wakati Madrid waliokuwa vinara wameteremka hadi nafasi ya tatu wakiwa na pointi 72 na Atletico Madrid ndiyo vinara wakiwa na 73.
Hesabu za kuangalia ni mwenendo wa timu hizo, namna Madrid wanavyokwenda ni balaa kwa kuwa Barcelona wamewazidi kwenye vitu vingi wakati ndiyo wako katika hatua za mwisho.

GD:
Kasi ya ufungaji mabao kwenye safu ya Barcelona imezidi kuwa juu na hasa tangu kurejea kwa Messi na hiyo inafanya tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa (GD) ya Barcelona kuwa juu. Barca imefunga mabao 88 na kufungwa 25 tu, hivyo GD yake ni 63.
Madrid imefunga 81 na kufungwa 32, GD yake ni 49. Hivyo ikitokea imelingana na Barcelona, basi itakuwa katika wakati mgumu kuwa juu yake.

Kanuni:
Kanuni za La Liga kuhusu timu kuwa juu ya msimamo, zinaonyesha kwanza timu inaangaliwa kuwa ina pointi ngapi, pili zimewahi kukutana mara ngapi na nani alifanya vizuri (head-to-head). Halafu vinafuata vigezo vingine.
Barcelona na Madrid zimekutana mara mbili kwenye La Liga, Barca imeshinda zote. Hivyo yenyewe iko katika nafasi nzuri zaidi.

Ushindi:
Ushindi mfululizo unazidi kujenga hali ya kujiamini ya Barcelona ambayo awali ilionekana iko taabani. Lakini kupoteza kunazidi kuidhoofisha Madrid ambayo ilijiona iko katika nafasi nzuri ya kutwaa ubingwa kabla ya kuboronga mechi mbili mfululizo.

Messi:
Messi ndiye amekuwa chachu ya mabadiliko ya Barcelona ambayo imekuwa na kiwango cha juu zaidi baada ya kurejea kwake.
Hali nzuri ya kuelewana kimchezo kati yake na watu wawili, Iniesta na Neymar imeongeza makali ya Barcelona katika kupata ushindi.

Mechi:
Baada ya mechi 30, kila timu imebakiza mechi nane tu. Katika kila mechi nane zilizobaki kwa timu hizo, inaonyesha zina ugumu wake kwa kuwa zitacheza na timu kama Espanyol, Getafe, Villareal na Atletico Madrid ambazo bila ya kujali ziko nafasi ipi lakini zimekuwa na upinzani mkubwa dhidi ya timu hizo.

Barcelona:
Espanyol, Real Betis, Granada, Villareal, Getafe, Athletic Bilbao, Elche na Atletico Madrid.

Madrid:
Rayo Vallecano, Real Sociedad, Almeria, Osasuna, Valencia, Valladolid, Celta Vigo na Espanyol.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic