March 28, 2014



Na Saleh Ally
UKIAMBIWA kazi ya ukocha wa soka katika nchi za Afrika inaweza kuwa moja kati ya kazi ngumu zaidi duniani, usikatae. Kuna mengi sana ya kuthibitisha hilo.

Hata kocha kama atakuwa na ujuzi kiasi gani, asilimia kubwa ya nchi za Afrika Mashariki, makocha wake wanafanya kazi bila ya kuwa na vifaa, makazi wala malipo mazuri.
FERGUSON

Wanaokuwa na ahueni ni makocha wa kigeni kwa kuwa tu, ugeni wao huwafanya wapate huduma kadhaa ambazo makocha wazalendo wamekuwa hawazipati hata kidogo.

Kuna kocha raia wa Brazil, Nielsen Elias alitua nchini kuinoa Simba miaka takribani sita iliyopita, mara baada ya kuonyeshwa uwanja wa mazoezi, akasisitiza kuwa kama hautabadilishwa ataondoka zake. Siku chache baadaye akasema wazi, Simba haikuwa hadhi yake, akaondoka.
 
WENGER
Kocha Ernie Brandts hadi anaondoka alikuwa hajatimiziwa ombi lake la kupewa magoli madogo aliyokuwa ameyaomba kwa uongozi wa Yanga ili kutoa mafunzo maalum. Lakini mwisho alionekana ameshindwa kuipandisha timu yake kiwango.
 
MOURINHO
Tatizo kwa viongozi wa soka nchini wanaonekana wanajua zaidi kuliko makocha, ndiyo maana timu kubwa kama Yanga na Simba, leo zaidi ya miaka 40, hazina hata viwanja vya mazoezi vyenye ubora.

Vitu vinavyoonekana ni vidogo, ndiyo vikubwa na timu nyingi kubwa maarufu duniani zinavithamini zikiwa njiani kupata maendeleo na zimefanikiwa.


PELLEGRINI

Malipo duni ya makocha, kutokuwa na makazi mazuri hadi wanapokuwa wageni au Wazungu lakini umewahi kusikia kuna klabu hapa nchini imetenga ofisi kwa ajili ya kocha wake?

Kila mmoja anaamini kocha kazi yake ni uwanjani pekee, lakini klabu zote kubwa duniani makocha wao wana ofisi zao.

Unaweza kusema Manchester United, Manchester City, Arsenal, Real Madrid na Barcelona ni kubwa sana. Je, timu za madaraja ya nchini katika nchi nyingine za Ulaya, makocha wao wanaofisi?

Ndiyo, mfano mzuri ni Gefle IF aliyowahi kuichezea Haruna Moshi ‘Boban’. Inashiriki daraja la kwanza na kocha wake, Perre Olsson ana ofisi yenye ubora ambao unaweza kulinganisha au zaidi ya ile ya meneja mkuu wa benki.

Hapa nyumbani inaweza kuonekana ni sawa na kichekesho cha karne kocha kuwa na ofisi kwa kuwa tu, hata makatibu au watendaji wa klabu na timu nyingine, angalau wamepata ofisi miaka michache iliyopita. Lakini kabla ya hapo mambo yaliendeshwa mfukoni au kwenye briefcase.

Kocha hana uwanja, hana vifaa na hana ofisi, makazi yake ni ya kubangaiza au ya kiwango duni lakini bado uongozi unachotaka ni ubingwa. Akishindwa, lawama zote na mwisho anatimuliwa, tena malipo yanakuwa shida.

Aliyekuwa Kocha Mkuu wa Manchester United, Alex Ferguson alikuwa akitumia muda wake kwa zaidi ya saa tano kila siku akiwa katika ofisi yake akipanga namna ya kufanya mikakati ya uendeshaji wa timu. Bado anakuwa na saa nyingine tatu hadi nne za mazoezi, mara mbili kwa siku.

Maana yake, Ferguson alikuwa akifanya kazi takribani saa 10 kwa siku kwa ajili ya Manchester United. Lazima atafanikiwa kwa kuwa anaipa nafasi kubwa zaidi kazi yake.

Kuna kiongozi yeyote wa Simba amewahi kufanya utafiti kwa nini makocha wawe na ofisini? Au nini umuhimu wake? Kazi ya soka inahitaji utulivu na utunzaji kumbukumbu kwa mpangilio.

Inawezekana akawa na mambo mengi sana ya kupanga kuliko Hans van Der Pluijm na Zdravko Logarusic wa Simba, lakini siku ya mwisho anachotaka ni mafanikio na hasa vikombe kama wanavyotaka makocha wa Yanga na Simba.

Kuiga maendeleo si vibaya, iko haja sasa timu za hapa nchini zikamuangalia kocha kama mwajiriwa anayeweza kufanya kazi zake klabuni na kupanga mambo mengi. Kuanzia watoto, vijana na timu kubwa.

Lakini si kocha kufanya kazi kipindi cha mazoezi pekee, haitoshi. Memba wa benchi la ufundi wanakutana wakati wa mazoezi pekee. Tofauti na Arsene Wenger anavyofanya na wenzake wa Arsenal au Manuel Pellegrini na wafanyakazi wenzake wa Manchester City.

Klabu za hapa nchini zinaweza kujifunza na zinaweza kubadilika, lakini hazipaswi kuwa na viongozi wanaozifanya ni ziada, njia ya kupita wapate majina au kujulikana zaidi au njia ya kulahisisha mambo ili wawanie ubunge kwenye majimbo yao!

Kujifunza ni sehemu ya hatua za maendeleo, ukikubali sehemu uliyokosea utaweza kupiga hatua. Makocha kuwa na ofisi ni sehemu ya mabadiliko na hatua za maendeleo.

Lakini bado ni muhimu kuwa klabu zetu ziwe na viwanja vya mazoezi, la sivyo ni sawa na kuwa na mtaji wa kuuza duka lakini hauna sehemu maalum ya kuuzia. “umachinga wa soka.”

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic