March 28, 2014





Mshambuliaji nyota wa Simba, Amissi Tambwe huenda akavunja mkataba wake na klabu hiyo na kuondoka zake mara baada ya kumalizika kwa msimu huu, ikiwa timu hiyo haitapata nafasi ya kuwakilisha taifa kwenye mashindano ya kimataifa.


Tambwe ambaye ndiye kinara wa mabao katika Ligi Kuu Bara akiwa na mabao 19, amesema kuwa matarajio yake wakati anajiunga na klabu hiyo yalikuwa ni kuiona ikishiriki mashindano ya kimataifa, hivyo kukosa kushiriki michuano hiyo kutamtibulia mipango yake na ametamka wazi anafikiria kuondoka klabuni hapo.

Simba ipo katika nafasi ya nne na haina matumaini ya kushika nafasi ya kwanza wala ya pili kwa kuwa imesaliwa na michezo minne, ambapo imezidiwa pointi 10 na Yanga inayoshika nafasi ya pili.

Tambwe, raia wa Burundi amesema hatma yake ya kuendelea kubakia Simba itajulikana baada ya kumalizika kwa ligi ya msimu huu ambayo ipo katika hatua za lala salama.

Alisema anaweza kuondoka au asiondoke Simba lakini alisisitiza kuwa kila kitu kitajulikana baada ya Aprili 19 ambapo ligi itakuwa inafikia tamati.

“Wakati najiunga Simba, matarajio yangu yalikuwa ni kushiriki mashindano ya kimataifa, lakini ndoto hizo zinaonekana kugonga mwamba kutokana kwa kuwa hivi sasa timu yetu ipo kwenye nafasi mbaya ambayo haitupi kabisa matumaini ya kumaliza ligi tukiwa kwenye nafasi mbili za juu ambazo kwa sasa zinashikiliwa na Azam na Yanga.

“Kusema kweli hali hiyo inasikitisha na inaniumiza sana kwani natamani kushiriki mashindano ya kimataifa kama walivyo wachezaji wote wanaotaka mafanikio katika mchezo wa soka.

“Hata hivyo kwa sasa siwezi kuzungumza lolote kama nitaendelea kubakia Simba au la ila hilo litajulikana baadaye baada ya kumalizika kwa ligi kuu, lakini nafikiri juu ya hilo,” alisema Tambwe.

Simba ina pointi 36 nyuma ya Mbeya City yenye pointi 42, Yanga yenye ponti 46 na Azam inayoongoza msimamo ikiwa na pointi 50.

Wakati huohuo, Tambwe amesema kama atapata nafasi ya kucheza kwenye mechi dhidi ya Azam katika ligi kuu keshokutwa kwenye Uwanja wa Taifa, atapambana ili kuhakikisha Azam inafungika.

“Azam ni timu tu kama timu nyingine, naiheshimu kutokana na ubora wake, tutahakikisha tunaivunja rekodi yao ya kutofungwa msimu huu,” alisema Tambwe.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic