March 24, 2014





Na Saleh Ally
SIKU chache zimepita tangu makala iliyokuwa ikieleza namna ambavyo wachezaji wa Yanga imefikia nao wawajibike au kujifanyia tathmini kuhusiana na suala la kutokuwa makini, itoke.


Maelezo ya makala yale yalifafanua namna ambavyo Yanga imekuwa na uwezo mkubwa wa kutengeneza nafasi, lakini ikishindwa kuzimalizia, hivyo kubakia na maneno mengi kuwa ilibaki kidogo tu.

Halafu baada ya hapo, mzigo wamekuwa wakiangushiwa walimu kwamba hawana uwezo lakini wakati mwingine wanakuwa si wao tu, badala yake tatizo ni la wachezaji ingawa ni vigumu sana kuonekana kwa upande huo wa pili.

Ukifanya tathmini, utagundua Yanga ndiyo kikosi kilichotengeneza nafasi nyingi sana za kufunga katika Ligi Kuu Bara, lakini ndiyo walioshindwa kuzitumia nafasi hizo isipokuwa katika mechi chache.

Lakini timu kama Azam FC, imejitahidi kutumia nafasi nyingi sana ilizozipata na wachezaji wake hasa Kipre Tchetche amekuwa kama msumari kila anapopata nafasi hizo.

Anayeonekana ni bora zaidi katika utumiaji nafasi hizo bila ya kujali ni mchezaji wa kigeni au mzalendo ni Amissi Tambwe wa Simba ambaye amekuwa makini zaidi anapofika langoni, unaweza kusema si mtu wa mchezo.

Lakini Hamisi Kiiza na Didier Kavumbagu wa Yanga, wamekuwa na tatizo kubwa la utumiaji nafasi. Huenda ni papara au woga kuwa mashabiki watasema imekuwa ni hali inayowatoa mchezoni, ndiyo makala hayo yalisisitiza ni lazima wawe makini au walimu wachukue uamuzi mgumu.

Yanga ilionyesha ugonjwa huo kwa kiasi kikubwa katika mechi yake ya kwanza wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al Ahly ya Misri. Baada ya hapo ikafanya hivyohivyo katika mechi ya pili jijini Alexandria na mwishoni ikang’olewa kwa penalti katika mechi iliyoonekana kuwa ‘yao’ kabisa.

Iliporejea nyumbani kwenye Ligi Kuu Bara, ilicheza mechi mbili ikianza na Mtibwa Sugar halafu Azam FC na ikapoteza nafasi nyingi kabla ya kujilaumu kwa kuambulia sare hizo mbili.

Kocha Hans van Der Pluijm aliendelea kuwatumia Kiiza na Kavumbagu bila ya kuwapa nafasi Jerry Tegete na Hussein Javu ambao alikuwa akiwaingiza muda ukiwa umeyoyoma sana.

Lakini mambo yamebadilika wakiwa Tabora wakati Yanga ikiivaa Rhino, amewapa nafasi na wote wamempa majibu kwamba wanazihitaji nafasi hizo, ndiyo maana kila mmoja akafunga bao moja.

Tegete alifunga bao la kwanza na kusababisha la pili baada ya shuti lake kuwababatiza mabeki. Javu alifunga la pili na kuongeza idadi ya mabao kwa Yanga ambayo ilishinda kwa mabao 3-0.

Kumbe Tegete na Javu bado wazima! Wanaweza kufunga na wameonyesha kwa vitendo na huenda walichokifanya kitakuwa changamoto kwa wageni pamoja na benchi zima la ufundi la Yanga kwamba kuna sababu ya kutoa nafasi kwa wengine.

Kusiwe na woga wa kuwapa nafasi wazalendo au isiwe staili kwamba ni lazima wageni ndiyo waanze katika kikosi cha kwanza. Kama kweli mtu anafanya vizuri bila ya kujali ni mzalendo au mgeni basi apewe nafasi.

Lengo si kuwabana Kiiza na Kavumbagu, lakini hali halisi inaonyesha kila kinachoelezwa. Basi hakuna haja ya kuwa na woga, kwani kama wanafanya vizuri hakuna haja ya kuwabania.

Kikubwa mwendo wa upangaji vikosi uangalie ubora wa kazi uwanjani na si huyu ni mchezaji mgeni ndiye anakuwa na nafasi kubwa ya kucheza hata kama haonyeshi kiwango cha juu. Kwa mshambuliaji, ubora wake kuwa juu ni kufunga tu, hilo halina mjadala.

Hii si kwa Yanga pekee, hata timu nyingine kwamba kama mgeni anaboronga basi abaki benchi ikiwa kama ni sehemu ya changamoto kwake na ikiwezekana ajiulize kwamba imekuwaje.

Hakuna sababu ya kuwaacha wanaoweza kufunga kwa hofu kuwa ni wazalendo, lakini si sahihi kuwaacha wachezaji bila ya kuwa na changamoto ya vitendo kama waliyoionyesha Tegete na Javu.

Wameonyesha wanaweza, basi wapewe nafasi tena na ikiwezekana Kiiza na Kavumbagu wakiwa benchi, basi waone kuwa kutozitumia nafasi ni kujiongezea ugumu wa kupata nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza na si kuwa na uhakika hata kama watavurunda.

Makocha wengi wenye timu zinazojumuisha wageni wamekuwa wagumu kuwaweka nje, hivyo hilo la Tegete na Javu, basi liwe kwa mabenchi yote ya ufundi yaliyolala yakajisahau sababu ya ugeni, lakini iwe changamoto pia kwa wanaoshindwa kufanya vizuri kwamba wakikosea, kuna wengine walio benchi wanaweza.

Kama ni uzalendo, Tanzania inahitaji washambuliaji bora, pia ni vizuri kuona vijana wa nyumbani wanacheza na hasa kama wana uwezo sawa na ule wa wageni, basi kipaumbele kiwe kwao. Wapeni nafasi vijana bana!

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic