April 21, 2014




MARA kadhaa kumekuwa na matatizo makubwa sana kuhusiana na suala la waamuzi wa soka nchini kuboronga katika mechi mbalimbali za Ligi Kuu Bara.

Waamuzi hao wamekuwa wakifanya madudu kila kukicha na kusababisha vurugu kila mara na baadhi yao wakionyesha waziwazi kwamba wamepania kuisaidia timu fulani.
Kwa kuwa suala la rushwa ni siri kubwa, kila mmoja anaweza kukanusha na kusema kivyake, lakini lazima tukubali kwamba kuna hilo tatizo.
Viongozi wengi wa soka wamekuwa hawapambani na rushwa, sitaki kusema wanahusika pia au la, lakini ukweli wako wanaoshiriki hata kudhoofisha nguvu ya kupambana na rushwa.
Lakini juzi, Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi, alikiri kwamba wapo wanaofanya mchezo huo mchafu na kwamba baada ya muda itafikia siku atamkamata mmoja wao na atakuwa mfano kwa wengine.
Malinzi ameyasema hayo wakati anafanyiwa mahojiano na kipindi cha michezo cha Radio One, huku akionyesha kwamba anakerwa na hali hiyo ambayo hakuna ubishi inazorotesha michezo nchini.
Mara ngapi kuna wale ambao wanataka hali hiyo kwisha wamekuwa wakipambana lakini badala yake wanaonekana ni sawa na maadui wakubwa kwa kusema ukweli?
Kitendo cha Malinzi kusema hadharani na kuonyesha anakerwa na jambo hilo, ndiyo wakati mzuri na mwafaka wa kuanza kufunga safari ya kupambana nalo na ikiwezekana na kulimaliza ili matokeo ya ligi kuu na ligi nyingine yawe ni yale yanayopatikana kwa uwezo na si ujanjaujanja.
Kuna timu hadi zimeunda vitengo vya fitna, kuna watu wanalipwa fedha ili kuhakikisha wanawahonga waamuzi ili kufanya mambo yaende vizuri kwao licha ya kuwa wana wachezaji na makocha wa kimataifa wanaolipwa fedha nyingi.
Waamuzi wanajua kuwa wao ni tatizo ingawa si wote, wako wanaowajua wenzao kwa majina kwamba wanashiriki mchezo huo mchafu ambao kadiri siku zinavyosonga, wanataka kuufanya halali na hauna tatizo.
Lakini kama Malinzi ambaye ndiye kiongozi wa juu zaidi katika soka ameona upuuzi huo, uchafu huo, basi kiwe kipindi mwafaka cha kumaliza kila kitu na kukifanya kiende vizuri, inawezekana na vizuri vita hii ianzie kwa waamuzi wenyewe na chama chao.
Si waamuzi wote wanaochukua rushwa, lakini wako wachache wanaoharibu sifa ya waamuzi wenzao na wao wote kutokana na tabia ya tamaa inayowaongoza. Tunajua huo ni ugonjwa wa dunia nzima kwa kuwa hata Ulaya, Marekani na kwingineko kuna waamuzi wenye tabia hizo.
Lakini si sahihi kuiga mfano mbaya na kuufanya ndiyo mwenendo wa maisha hata kama tumekuwa tukikopi mengi kutoka kwa wenzetu kutokana na wao kupiga hatua. Badala yake tuyatumie makosa yao kama sehemu ya kujifunza na kufanya kilicho bora, maana ifikie siku nao waje waige kwetu, inawezekana.
Hakuna haja ya woga, kweli kuna waamuzi mnachukua mlungula na mnajuana. Wenyewe pia mnajua tamaa zenu zinavyoathiri mpira wa Tanzania ambao kila siku haukui.
Hata kama kuna makosa ya viongozi au uzembe wa wachezaji, lakini waamuzi ni sehemu kubwa ya kuzorotesha mchezo wa soka na mmegeuza rushwa ni haki yenu kwa kuwa tu ni vigumu kuwa na ushahidi mnavyochukua kwa vile wanaotoa pia wanaficha siri.
Bosi wenu sasa anajua, huenda tamaa inazidi kuwaongoza. Lakini kama imefikia hadi anayewaongoza amekubali, basi kidogo anzeni kuona hata aibu ili muusaidie mpira wa Tanzania.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic