April 30, 2014

MWOMBEKI AKIPAMBANA NA MABEKI WA PRISONS

Mshambuliaji wa Simba, Betram Mwombeki, amesema kwamba yupo tayari kuvunja mkataba na klabu hiyo endapo ataendelea kusota benchi na kukosa amani kwenye kikosi hicho msimu ujao.

Mwombeki aliyesajiliwa na Simba iliyokuwa chini ya Abdallah Kibadeni msimu uliopita, alikuwa shujaa wa timu hiyo kwenye mechi kadhaa hasa ile dhidi ya watani wao, Yanga, pale alipofunga bao na kuisaidia timu hiyo kutoka nyuma na kuilazimisha Yanga sare ya mabao 3-3 kwenye ligi kuu msimu uliopita.
Lakini baada ya muda mfupi mambo yalimbadilikia straika huyo na kuanza kusugua benchi huku mara kwa mara akikosekana kwenye mazoezi ya timu hiyo baada ya kutua kwa utawala wa Mcroatia, Zdravko Logarusic.

Mwombeki alisema huwa hafurahii maisha aliyonayo Simba kwa sasa, hivyo endapo msimu mpya utaanza na mambo yatakuwa ni yaleyale, basi atakuwa hana budi kuachana na timu hiyo na kuangalia maisha mengine.

Mwombeki amebakiza mkataba wa mwaka mmoja klabuni hapo unaoisha mwishoni mwa msimu wa 2014/15.
“Haina haja ya kukuelezea sana kwamba nilikuwa naishi maisha gani Simba, kila mtu aliyekuwa anafuatilia soka alikuwa anaona kilichokuwa kinaendelea, lakini kama itatokea mambo haya yataendelea msimu ujao basi nitavunja mkataba na kuangalia mambo yangu mengine.
“Naweza nikatafuta timu nikacheza au nikaangalia maisha yangu mengine na nikatulia kwanza kuhusu soka.
“Siwezi kusema kwamba Loga ndiyo chanzo kwa sababu yeye amekuja na mfumo wake mpya na kila kocha anakuwa na mipangilio yake katika timu, lakini kuna vitu vingi muda mwingine huwa vinaendelea na mimi huwa siridhishwi navyo.
“Ishu kubwa ni kwamba mimi nacheza mpira, sasa kama mtu unacheza soka ni lazima watu wakuone uwanjani na si kukaa benchi tu, hii inakuwa haipendezi, soka ni mchezo wa kuonekana, sasa kama mtu unakuwa hupewi nafasi ina faida gani sasa?” alihoji Mwombeki.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic