July 28, 2014



Na Saleh Ally
WATANZANIA wanaweza kuwa mashuhuda si kwa kuangalia kwenye ‘kideo’ badala yake wataeleza umahiri alionao mshambuliaji, Didier Drogba kwa kuwa amewahi kuzitikisa nyavu za Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.


Drogba alifunga bao pekee wakati Taifa Stars ilipolala kwa bao 1-0 katika mechi ya kirafiki iliyopigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar.

Ufundi wa bao lile, aliwahi kuhadithia beki kisiki nchini, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ aliyeeleza wepesi wa Drogba na akili ya haraka linapofikia suala la kufunga.

Drogba sasa ana umri wa miaka 36, lakini kocha Jose Mourinho wa Chelsea, ameshindwa kuficha anachokiamini ndani ya moyo wake, ameamua kumrudisha mkali huyo kundini.


Drogba amesaini kuichezea Chelsea kwa mwaka mmoja akitokea Galatasaray ya Uturuki, hali ambayo imewafanya wengi wajiulize maswali, kila mmoja akiwa na upande wake.

Wapo wanaohoji kama kweli Drogba atakuwa na makali kama yale alipoichezea Chelsea kuanzia mwaka 2004 hadi 2012 alipoamua kuondoka. Wengine wanahoji kuhusu Mourinho kuamua kujaribu patapotea hiyo na kama itakuwa na msaada kwake.

Kuna mambo mengi aliyonayo Drogba ambayo yangeweza kumshawishi kocha yeyote makini na kuamini kweli atafanya vizuri na kufanikiwa akiwa na Drogba.


Mourinho si mgeni kwa Drogba na hakuna shaka anajua anachokitaka na ‘Tembo’ huyo anaijua kazi yake kwa kuwa kuanzia akiwa na umri mdogo hadi ‘uzeeni’ bado ameendelea kuthibitisha kuwa ni kiwembe.

Ukiwembe wa Drogba si wa maneno, unadhihirishwa na takwimu ya timu zote alizopita na ligi alizozichezea kwamba si mtu wa kuchezea, silaha yake kubwa ni kazi ya ukweli.

Kwa msimu mmoja akiwa na Chelsea, bado ana nafasi ya kutoa msaada na vizuri atakuwa na ‘ticha’ anayejua afanye nini akiwa naye. Yaliyomvuta Mourinho ni mengi na inawezekana asifanye vizuri lakini kufanya vizuri zaidi ni asilimia nyingi. Angalia baadhi ya haya.


 Mabao 100:
Hadi anaondoka Chelsea, Drogba aliweka rekodi ya kuwa Mwafrika wa kwanza kufunga mabao 100 katika Ligi Kuu England, maarufu kama Premiership.

Drogba aliondoka na mabao 100 kamili baada ya kuichezea Chelsea mechi 226. Amekuwa mchezaji wa 22 kufunga mabao 100 katika ligi hiyo. Kocha yeyote angeweza kuvutiwa naye.

Kila timu:
Wastani wa mabao aliyofunga kwa kila timu aliyoichezea kuanzia mwaka 1998, inaonyesha ni mshambuliaji mwenye uwezo wa juu sana. Angalia jedwali.

 MWAKA             TIMU        MECHI/MABAO

1998–2002             Le Mans         64(12)

2002–2003           Guingamp        45(20)

2003–2004            Marseille          35(19)

2004–2012            Chelsea            226(100)

2012–2013            Shanghai           11(8)

2013–2014            Galatasaray       37(15)

2014–            Chelsea               ?(?)

Eto’o:
Ilionekana Samuel Eto’o ndiye angeziba pengo na kuwasahaulisha Chelsea kuhusiana na Drogba. Lakini inaonekana imeshindikana na sasa amerejea.

Bado atakuwa na mtihani mkubwa wa kuonyesha Mourinho hakukosea, lakini pia kufanya kazi nzuri zaidi ya ile iliyofanywa na ‘shemeji’ yake Eto’o akiwa na Chelsea kwa msimu mmoja. (Mke wa Eto’o ni raia wa Ivory Coast).

 Makombe:
Kwa misimu miwili aliyocheza Uturuki akiwa Galatasaray, Drogba amefanikiwa kutwaa makombe matatu ya ligi kuu (2012–13), Super Cup (2013) na Kombe la Uturuki (2014).

Sasa kumbuka kipindi cha Chelsea wakati akiwa na Mourinho na hata baada ya hapo, Drogba amekuwa akibeba tu makombe.

Hadi anaondoka Chelsea, amefanikiwa kubeba jumla ya makombe 10 ya Ligi Kuu England, Kombe la FA na Kombe la Ligi. Pia amebeba ngao mbili za jamii.

Maana yake anaporudi leo Chelsea, inaonekana Mourinho ana haki ya kujaribu tena kama almasi aliyojipamba nayo miaka kadhaa iliyopita, kweli bado inaweza kung’ara?

Ikishindikana, basi hakuna anayeweza kumcheka kwa kuwa hata kama kweli ni masharti na vigezo, amezingatia na kazi ya Drogba ndiyo iliyomtia wazimu. Kikubwa sasa ni kusubiri, Drogba ataweza? Kwa kuwa mpira unachezwa hadharani, acha Premier League ianze.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic