July 26, 2014



Kocha mkuu wa timu ya Yanga Mbrazili, Marcio Maximo ni kama vile sasa ameamua kuwatolea uvivu wachezaji wake wa kimataifa wa Uganda Emmanuel Okwi na Hamis Kiiza kutokana na kile alichosema juu ya aina ya wachezaji anaowahitaji katika kikosi chake na yupo tayari kuwatema.

Kwa sasa ndani ya klabu ya Yanga kuna mchako wa kupunguza mchezaji mmoja wa kimataifa ili kupata nafasi ya kumuongeza katika usajili wao Mbrazil Genilison Santos ‘Jaja’ aliyeingia mkataba wa miaka miwili.
Sheria ya soka la Tanzania inaitaka kila klabu inayoshiriki Ligi Kuu Bara kuwa na wachezaji watano wa kimataifa, lakini Yanga mpaka sasa ina wachezaji sita, Kiiza, Okwi, Jaja, Andrey Coutinho, Mbuyu Twite, Haruna Niyonzima.
Maximo amefunguka kuwa kamwe hatakubali kufanyakazi na mchezaji mbinafsi na mwenye chuki kwenye kikosi chake na yupo tayari kumtema hata kama atakuwa na kiwango gani.
Kauli hiyo, ni kama inawagusa viungo Okwi na Kiiza ambao wenyewe kila mara wamekuwa wakilalamikiwa na vitendo hivyo na viongozi wa juu wa timu hiyo.
Katika msimu uliopita wa ligi kuu, Okwi alidaiwa kugomea kucheza mechi sita mfululizo ambazo zote zilikuwa muhimu ikiwemo dhidi ya Simba na Azam FC.
Wakati Okwi akifanya tukio hilo, Kiiza mwenyewe alionyesha utovu wa nidhamu kwa kuondoka kwenye vyumba vya kubadilishia nguo na kwenda kukaa jukwaani mara baada ya kutolewa nje na aliyekuwa Kocha Mkuu wa timu hiyo, Hans Pluijm timu hiyo ilikuwa ikivaana na Ruvu Shooting.
Mbali na hayo Kiiza kuna kipindi aligoma kucheza Yanga, kutokana na madai kuwa amepata timu na Yanga wanambania kwenda huku akishutumiwa kwa ujeuri, huku Okwi usumbufu wake ulianzia alipokuwa katika timu ya Simba ambapo mara kwa mara alikuwa akikorofishana na viongozi wake.
Akizungumza na Championi Jumamosi, Maximo alisema kuwa kila mchezaji kwake ni sehemu ya ushindi, hivyo hatakubali kuona makundi yakitengenezwa kwenye kikosi chake ambayo yatasababisha mgawanyiko.
Maximo alisema, amekubali kuifundisha Yanga kwa ajili ya kuibadilisha na kuipa mafanikio makubwa ikiwemo timu kushinda na kuchukua mataji ya ubingwa mbalimbali.
Aliongeza kuwa, pia katika kikosi chake hatampanga mchezaji kutokana na ukubwa wa jina, atampa mchezaji nafasi ya kucheza yule anayejituma na anayetambua majukumu yake ndani ya uwanja katika kupata ushindi.
“Mchezaji mbinafsi na mwenye chuki, kamwe sitampa nafasi ya kucheza kwenye kikosi changu, kikubwa ninachoangalia ni uwajibajika wa mchezaji ndani ya uwanja, lakini wale wenye utovu wa nidhamu nitaachana nao.
“Silaha kubwa ya ushindi katika timu ni amani na upendo, hivyo ili timu ipate ushindi na ichukue makombe basi umoja lazima uwepo na siyo kuwepo na ubinafs na chuki huku wengine wakijiona wao ndio kila kitu.
“Hivyo kama nikimgundua au nikiwagundua wachezaji wenye tabia hizo, basi nitaondoa kwenye kikosi change haraka sana, bado nawafatilia wote na nasubili hao wengine waje ndiyo nitatoa msimamo wangu wa mwisho, ni vyema wachezaji wangu wote wakalifahamu hilo,”alisema Maximo.
Maximo ni kati ya kocha anayetambulika kusimamia nidhamu ya hali ya juu katika kila timu anayofundisha, anakumbukwa kwa jinsi alivyowatema mastaa kama Juma Kaseja, Athuman Iddy ‘Chuji’ na Haruna Moshi ‘Boban’ alipokuwa kocha wa Taifa Stars miaka sita iliyopita.
Wakati huohuo uongozi wa Yanga umeamua kukaa kando kuhusu kupunguzwa kwa mchezaji mmoja wa kimataifa klabuni hapo na sasa umemakabidhi rasmi suala hilo Maximo aamue moja kati ya Okwi na Kiiza.
Kutokana na kauliza Maximo, Championi Jumamosi lilizungumza na Katibu Mkuu wa Yanga, Beno Njovu na kufafanua kuwa hiyo ishu ya kiufundi zaidi na kwamba wao kama uongozi hauwezi kuiingilia badala yake wamemwachia Maximo ndiyo atakayekuwa na maamuzi ya mwisho kuhusiana na hilo.
“Unajua haya ni mambo ya kiufundi zaidi kuhusu kuchagua ni wachezaji gani wabaki na nani aondoke kwa ajili ya msimu ujao, kocha mwenyewe ndiyo ataangalia wakina nani watamfaa na nani hamfai kisha yeye atatoa maagizo kulingana na tathimini yake.
“Yeye anatambua kuhusu usajili wa wageni na ndiyo aliyetoa pendekezo la usajili wa Jaja na Coutinho kwa hiyo tayari ana ‘target’ zake, tumwache aamue yeye anaotaka wawepo kwenye mpango wake kisha sisi tutatekeleza, hatuwezi kumpangia,” alisema Njovu.
Tangu Maximo aanze kuinoa Yanga takriban wiki nne zilizopita mpaka sasa Kiiza, Okwi na Niyonzima bado hawajajumuika kwenye mazoezi ya timu hiyo kutokana na majukumu ya timu zao za taifa waliyokuwa nayo  lakini taarifa zinaeleza kuwa tayari Maximo ameshaangalia CD za wachezaji hao kwa ajili ya kuufahamu uwezo wao.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic