December 13, 2014


Inaonekana mshambuliaji nyota wa Yanga, Mrisho Ngassa amepoteza mvuto kutokana na mambo kadhaa.


Kwanza kabisa amekuwa hafungi mabao au kufanya kazi kama ile iliyozoeleka, kwamba anatoa krosi nyingi safi au kufunga mwenyewe.

Wakati kikosi cha Yanga kikitarajiwa kushuka uwanjani leo hii kupambana na Simba katika mechi ya Mtani Jembe 2, kocha mkuu wa timu hiyo, Mbrazili, Marcio Maximo, amekifanyia mabadiliko makubwa kikosi chake huku akimtupa nje kiungo wake, Ngassa.

Katika mechi hiyo inayosubiriwa kwa hamu kubwa na wapenzi wa soka hapa nchini, Ngassa anatarajiwa kuanzia benchi kutokana na kuporomoka kwa kiwango chake katika siku za hivi karibuni.

Huenda Maximo akabadili mambo, lakini kutokana na mazoezi ya Yanga ambayo SALEHJEMBE  iliyafuatilia kwa karibu sana, inaonekana Maximo atamuweka Ngassa nje.

Yaani ataanzia benchi na kama ikiwa hivyo, basi ana kazi kubwa ya kusali, aombe apate ya kucheza.

Kama akiipata, basi ana kila sababu ya kuonyesha kwamba Maximo amesahau kwamba Ngassa anaweza.

Maximo anatarajia kumuanzisha Simoni Msuva ambaye tangu Ligi Kuu Bara ilipoanza msimu huu, amekuwa akianzia benchi na kuingia kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Ngassa au Andrey Coutinho huku akionyesha kiwango kikubwa cha kuwa kikosi cha kwanza.


Tangu kikosi cha Yanga kilipoingia kambini kujiandaa na mechi hiyo, Ngassa amekuwa akipangwa mazoezini katika kikosi cha pili ambacho kinaundwa na wachezaji wengi wa akiba, hali ambayo imekuwa haimfurahishi mshambuliaji huyo.

Inawezekana Maximo alifanya hivyo kumpa ugumu ili leo aanze, kama kweli akianza lazima afanye kazi ya ziada.

Mechi ya leo itakuwa ni sehemu ya uamuzi, kwamba Ngassa bado wamo au ndiyo safari inamkuta, kazi kwake kuonyesha hasi au chanya ingawa hakuna ubishi uwezo anao, je, anautumiaje? tusubiri.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic