January 14, 2015

WACHEZAJI WA POLISI DODOMA WAKIMSHAMBULIA MWAMUZI WA AKIBA KATIKA MECHI YAO YA DARAJA LA KWANZA DHIDI TOTO AFRICAN KWENYE UWANJA WA CCM KIRUMBA, MWANZA. 

Na Saleh Ally
WAKATI mwingine nachelea kusema Watanzania tumekuwa na uoga usiokuwa na sababu za msingi hadi kufikia kuwapa watu nafasi ya kuvunja sheria, pia bila ya sababu za msingi.


Kweli kila mmoja wetu anajua nguvu ya jeshi, maana wanatumia silaha, wana mafunzo ya kupambana, hivyo ni watu ambao wameiva kwa mapambano.

Ninajua majeshi yote, wanapewa elimu hiyo kwa ajili ya usalama wa raia na hakuna ubishi wote ni waajiriwa wa wananchi ambao kodi zao ndizo zinazowalipa mishahara na kuendesha mambo mengi ya majeshi hayo.

Leo nitazungumzia Jeshi la Polisi Tanzania bila ya woga hata chembe, kwa kuwa sasa naona wanataka kugeuka sehemu ya waharibifu wa amani na nidhamu katika mchezo wa soka.


Imekuwa ni hali ya kawaida, timu zinazomilikiwa na Jeshi la Polisi kufanya vurugu bila ya woga wakijua hakuna wa kuwagusa.

Timu hizo zinaundwa na baadhi wakiwa maaskari na wengine raia, lakini wanafanya vurugu waziwazi wakijua wao ndio wenye uwezo wa kuwaadhibu wengine wakifanya hivyo, kwa kuwa ni wao, watalindwa wafanye vurugu.

Mechi lukuki zimetokea hivyo, tokea wakati huo daraja la nne na wakati mwingine hadi Ligi Kuu Bara, mara kadhaa tuliona mambo hayo na tukayakemea kwa nguvu kubwa.

Sasa naona yanaanza kurejea kwa kasi kubwa huku kama ilivyo kawaida, viongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na wengine wa ngazi za mikoa wakiwa kimya kwa ileile hofu kuwa hili ni jeshi, mimi naifuta.


Naona yanayofanyika ni mambo ya kijinga tena hadharani. Angalia namna timu ya Polisi Mara walivyowashambulia kwa mawe kwa kuwapiga na kuwaumiza wachezaji wa Mwadui FC pamoja na Kocha, Jamhuri Kihwelo ‘Julio’.

Mshambuliaji Bakari Kigodeko alipigwa jiwe kwenye goti kwa kuwa alitoa pasi ya kusawazisha bao. Julio alipigwa jiwe la mgongo katika vurugu hizo.

Mwenyekiti wa Chama cha Soka Shinyanga (Shirefa), Kangi Lugola alipigwa na mashabiki hao, akachaniwa nguo, hakika huyu mtu mzima ameaibishwa. Yote haya yametokea mjini Musoma.

Julio alilazimika kupiga simu Dar es Salaam kwa kuwa baadhi ya waliokuwa wakishiriki ni rafiki wa askari na hakuna anayeweza kuwazuia.

Siku hiyohiyo kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza, wachezaji wa Polisi Dodoma licha ya kuwa ugenini, walikuwa ‘busy’ wakipiga waamuzi, wakianza na wa akiba, halafu yule wa katikati.

Mmoja wa wachezaji bila ya aibu, alimkimbiza mwamuzi huyo hadi jukwaani. Kufika huko mashabiki wakamtolea uvivu na kumchakaza makonde na makofi. Lakini hivi karibuni timu nyingine ya Polisi hukO Tabora ilifanya tena vurugu.

Hawa wachezaji na mashabiki wa Polisi, jeuri wanaitoa wapi? Kwa nini wanafanya mambo haya ya kipuuzi na kulichafua jeshi hilo ambalo lina watu wengi makini?

Hata hao makini, hawawezi kukwepa kuchafuka kama watakuwa kwenye dimba la wapuuzi wachache ambao hawaelewi kazi ya polisi ni kudumisha amani na utulivu badala ya kusababisha vurugu za makusudi, huu ni upuuzi wa kupindukia!

Siku moja nikiwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, mwishoni mwa mwaka jana, nilishuhudia shabiki mmoja wa Toto African akishuka jukwaani na kwenda kumuondoa mwandishi wa Championi aliyekuwa akipiga picha karibu na kibendera.

Sababu za msingi, eti mganga wao alisema mtu yeyote asikae eneo hilo. Mwandishi akakimbilia kwa askari waliokuwa pale kushitaki, lakini kwa kuwa askari wale jamaa ni washkaji zao, wakamsisitiza mwandishi aache kupiga picha eti wenye mechi hawataki! Angalia maajabu haya!

Kuna sababu ya Jeshi la Polisi Tanzania pia kuanzisha mafunzo maalum kwa wanaokwenda viwanja vya michezo ili kuondoa hofu ya askari kutojua haki za wahusika walio uwanjani, mpigapicha anatakiwa akae wapi, shabiki ashangilie namna gani na kadhalika.

Msisitizo ni kwamba, timu za soka zilizo chini ya Jeshi la Polisi, zimekuwa zikilipaka matope jeshi hilo kuonyesha kwamba hawana nidhamu.

Ajabu askari polisi wanataka nidhamu na watu wafuate sheria wakati wao wanaonyesha  ni mbumbumbu wa sheria za soka kwani wanaowapiga watu, hawafuati sheria za soka. Wanawaachia rafiki zao wawaonee watu, wawaumize kwa kuwa wanaamini wanatetea timu za polisi!

Hiyo inatokana na kujumuisha watu wasio waelewa, wanaoamini kuwa askari ni kufanya unavyotaka huku wakiwa wamesahau hata mchezo wa soka una sheria na kanuni zake na hakuna hata sehemu moja inayoruhusu kupiga au kumshambulia binadamu badala yake ni kupiga mpira au kushambulia kwa mpira pekee!




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic