January 14, 2015


Na Saleh Ally
MJI wa Freiburg uko Kusini mwa nchi ya Ujerumani, sifa yake ni utulivu na mji wenye watu wataratibu na wanaojiamini kwa kiasi kikubwa.


Mwaka juzi nilihudhuria michuano ya vijana iliyofanyika kwenye mji mdogo wa Hausen ambao uko takribani kilomita sita kutoka Mji wa Freiburg.

Baadhi ya wachezaji waliokuwa kwenye michuano hiyo bila ya kujali walicheza au la ni Said Ndemla (sasa yuko Simba) na Mudathir Yahaya (anaitumikia Azam FC) na Frank Sekule, yuko Majimaji.

Watu wa eneo hilo, wanasapoti kubwa kwa timu yao inayoshiriki Bundesliga. Hiyo ni FC Freiburg ambayo kamwe hawajawahi kuwaza iwe bingwa na hawataki ishuke daraja, shida yao kubwa ibaki Bundesliga ili iwape burudani.


Mmoja wa wachezaji waliowahi kung’ara na timu hiyo ni Papis Cisse ambaye sasa yuko Newcastle. Mmoja wa mashujaa na magwiji wa FC Freiburg ni Joachim Low, pia anatokea eneo hilo na ndipo yalipo makazi yake.

Low ndiye kocha mkuu wa kikosi cha timu ya taifa ya Ujerumani alichokifundisha kwa mafanikio makubwa.

Kocha huyo ni kati ya mashujaa wa eneo hilo, watu wa Freiburg wanajisifia kwa kusema ukweli na wasio na hofu wakitaka jambo. Wanaotaka haki walio tayari kuiomba au kushauri bila ya woga.

Kwa sasa Low ni Kocha Bora wa Dunia 2014. Ameitwaa tuzo hiyo akiwabwaga Muitaliano Carlo Ancelotti na Muargentina Diego Simeone.

Hata kabla ya kutwaa tuzo hiyo juzi, Low alionyesha kweli anatokea Freiburg alipozungumza jambo ambalo litasababisha mapinduzi katika mchezo wa soka.

Substitute ya nne, yaani badala ya timu kufanya mabadiliko ya wachezaji watatu katika mechi moja. Basi Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) lifanye utaratibu wa kuboresha kwa kuiangalia upya sheria hiyo ya mabadiliko.

Alichokisema Low nakiunga mkono kwa asilimia mia moja kwa kuwa ndiyo uboresha mpya wa mambo ya soka.

Soka haliwezi kubaki palepale. Lazima kuna mambo mapya yatakuja kama ambavyo tumeona Rais wa Shirikisho la Soka la Ulaya (Uefa), Michel Platini amependekeza iwepo kadi nyeupe.

Kadi nyeupe inapendekezwa kuwa itakuwa hivi; mchezaji anayelambwa kadi hiyo anaweza kurejea baada ya muda fulani.

Sikuwahi kuunga mkono wazo hilo la Platini kama ambavyo ninaunga hili la Low. Huu ni mtazamo wa kila mmoja lakini ni hatua ya kutengeneza njia sahihi ya mchezo wa soka ambao pia unaihusu Afrika na Tanzania kwa jumla.

Hakuna ubishi Low hajasema kwa maslahi ya Tanzania, Yanga, Simba, Mtibwa au Azam FC, anaangalia timu yake ya taifa ya Ujerumani, klabu za Ujerumani na Ulaya kwa jumla, lakini anajua sheria itagusa dunia nzima kama kweli kutakuwa na mabadiliko.

Ninaunga mkono pendekezo hilo la Low kwa kuwa naona litawapa makocha hata wa hapa nyumbani kubwa na wigo mkubwa wa kuwatumia wachezaji zaidi.

Wachezaji watapata fursa ya kucheza zaidi hasa kama kocha anaona anahitaji kubadilisha wachezaji lakini amekuwa akibanwa na mabadiliko mara tatu tu.

Yote yanawezekana, alichoanzisha Low kinaweza kuwa mjadala lakini hata Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) linaweza kukifanyia tathmini na kuangalia kama kina manufaa, basi nao wamuunge mkono Low.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic