January 16, 2015



SIKU ambayo Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), lilijitutumua na kutangaza kuufungia Uwanja wa Karume mjini Musoma kutumika katika mechi za Ligi Daraja la Kwanza, ndiyo siku ambayo wachezaji wa Polisi Tabora walimtwanga mwamuzi.


TFF iliamua kuufungia uwanja huo baada ya vurugu kubwa zilizozuka wakati timu ya Polisi Mara ikicheza na Mwadui FC, wikiendi iliyopita.


Kocha wa Mwadui FC, Jamhuri Kihwelo ‘Julio’, alipigwa jiwe la mgongo, mshambuliaji Bakari Kigodeko kwa kuwa alitoa pasi ya bao la kusawazisha naye alipigwa huku Mwenyekiti wa Chama cha Soka Shinyanga, Kangi Rugola naye akipigwa na kuchaniwa nguo hadi kubaki uchi!

Saa chache zilitofautisha vurugu za Musoma na zile za kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza wakati wachezaji wa Polisi Dodoma walipompiga mwamuzi wa kati na yule wa akiba.

Tena mchezaji mmoja wa Polisi Dodoma yeye alidiriki kumkimbiza mwamuzi hadi jukwaani ambako aliambulia kipigo kutoka kwa mashabiki wa Toto. Jiulize yule mchezaji alijiamini vipi hadi akapanda jukwaani?

Sasa TFF imetoa adhabu, huenda bado inaendelea kuchunguza. Jana wachezaji wa Polisi Tabora nao walimpiga mwamuzi wa kati na msaidizi wake.

Wachezaji hao wa timu ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Tabora, wamempiga mwamuzi huyo baada ya Toto African kusawazisha bao na kufunga la pili. Waliendelea kuwapiga waamuzi na mmoja alipokimbilia jukwaani walijaribu kumfuata.

Mashabiki walionyesha kukasirishwa na kutaka kuwaadhibu, hali iliyosababisha askari polisi waingilie. Baadaye mwamuzi akarudishwa chini ya ulinzi mkali na kumaliza mpira, Polisi Tabora wakiwa wameshatoa timu yao uwanjani!

Kiongozi wa soka kapigwa na mashabiki wa Polisi Mara, wachezaji na kocha wa Mwadui FC wakapigwa na mashabiki wa Polisi Mara.

Siku iliyofuata wachezaji wa Polisi Dodoma wakampiga mwamuzi huku akikimbizwa kama kibaka. Siku moja baadaye waamuzi wamepigwa na wachezaji wa timu ya Polisi Tabora.

Maana yake timu za Polisi ndizo zinazoongoza kwa kujichukua sheria mkononi katika mchezo wa soka. Hii ni sehemu ya picha mbaya kwa jeshi hilo kwa kuwa lina timu zinazoendeshwa au kutumikiwa na watu wasiokuwa waelewa.

Hatuwezi kukwepa kwamba timu za soka zipo kwenye jamii, wanajua kuhusiana na wananchi kukatazwa kuchukua sheria mkononi. Sasa vipi timu za Polisi zinachukua sheria mkononi kwa kuwapiga waamuzi eti kwa kuwa wao ndiyo polisi?

Jeuri hiyo ya kudharau mamlaka husika katika soka kama TFF wanaipata wapi? Wanamtegemea nani? Kwa nini wanafanya hivyo?

Ndiyo maana nasisitiza, uamuzi wa TFF kufungia uwanja pekee bado hautamaliza tatizo hili, badala yake kuwe na juhudi za kuwanasa wahusika na adhabu yao iwe kali kupindukia ili iwe mfano kwa wengine.

Kama kweli kuna mwamuzi anaboronga, basi naye apewe adhabu kali ambayo itakuwa mfano kwa wengine.

Lengo langu si kuwatetea waamuzi wafanye maovu, lakini tukubaliane hatuwezi kuwa na waamuzi wanaofuata sheria kwa kupigwa kama ngoma karibu kila mechi inayohusisha timu za Jeshi la Polisi au jeshi jingine lolote.

Si wanajeshi wala askari walio juu ya sheria, kwa kuwa siku ya mwisho wote ni wananchi. Hivyo lazima wakubali kuna mamlaka zitakazoshughulikia matatizo kama hayo.

Hata mamlaka hizo pia bado zinaweza kukosolewa kama zitachukua uamuzi ambao si sahihi katika mambo ya msingi na haki.

Ndiyo maana nasisitiza, timu za majeshi lazima zionyeshe kuwa zinatokea katika taasisi zinazoheshimika na nidhamu ndiyo uti wa mgongo, badala ya kufanya mambo ya kihuni kama zinavyofanya sasa!



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic