March 6, 2015



JUMAPILI saa 10 jioni, watani wa jadi Yanga na Simba wanakutana tena kwa mara nyingine msimu huu. Kwa hesabu za kawaida watakuwa wanakutana kwa mara ya tatu katika msimu mmoja na mara ya kwanza kwa mwaka huu.


Nimesema mara tatu kwa kuwa naunganisha mechi ya kwanza ya Ligi Kuu Bara iliyomalizika kwa sare ya bila mabao, ilipigwa Oktoba 18, 2014.

Katikati kuna mechi moja ni ya kirafiki lakini maarufu kama Nani Mtani Jembe ambayo ilipigwa Desemba 13, 2014 na Simba wakaibuka na ushindi wa mabao 2-0 na kuchukua kikombe.

Sasa wanarudi kwenye ligi na hesabu za kitaalamu zinaonyesha kwa msimu huu hakuna mbabe kwa kuwa mechi ya kwanza ilikuwa na sare ya bila bao. Hivyo kila timu pamoja na kuwa inatafuta pointi tatu muhimu lazima ijue hakuna ambayo imeifunga nyingine au kushinda katika msimu wa 2014-15.

Ndiyo, hakuna ubishi kwamba Yanga na Simba wanasaka pointi tatu muhimu, Simba wanataka kujikomboa kutoka katika hali ya kusuasua na Yanga wanataka kuendeleza hali yao ya kasi ambayo imeanza kuonekana.

Ushindi ndiyo furaha na faraja ya kila upande lakini ukirudi katika hesabu, kila upande unazitaka pointi tatu zake ili kujiongezea katika msimamo. Yanga ndiyo vinara, inajua kila timu yaani 13 zilizobaki Ligi Kuu Bara zinaifukuza, lakini Simba pia inataka kupanda hadi ‘Top 2’ ikitokea nafasi ya nne.

Yanga ina pointi 31 kileleni, Simba ina 23. Ingawa pengo la pointi ni kubwa lakini kila upande unataka kupata pointi hizo tatu ili kujiimarisha kutokana na malengo zilizojiwekea. Yes! Kila upande unataka uzipate pointi tatu tamu kuliko zote za ligi kwa Yanga na Simba.

Wakati Yanga na Simba wanawaza kila wanalotaka, mfano ujiko, furaha, kupoza presha upande wa viongozi, makocha na wachezaji au umuhimu wa pointi tatu, bado tukubaliane mechi hiyo inapaswa kuwa mfano kwa kuwa ndiyo taswira ya soka nchini.

Tunajua kuna Azam FC, Mtibwa Sugar, Kagera Sugar na timu nyingine ambazo zimekuwa mfano wa kuigwa kutokana na mambo kadhaa mazuri zinayofanya, lakini pia tukubaliane, wakongwe hao wanapaswa kupewa nafasi yao na hilo halipingiki hata kidogo.

Wakikutana watani hao, mambo mengi yanasimama kwa lengo la kuwashuhudia wakifanya mambo yao. Sasa wanachofanya nini, hapa ndiyo ninaposisitiza kwamba taswira iwe kweli wakongwe au baba wa mpira wa Tanzania wanakutana.

Kuanzia uwanjani, soka liwe la uhakika, mechi ichezwe kwa kiwango ambacho yeyote awe wa Tanzania au nje, aamini kweli wakongwe wa mpira wa Tanzania wamekutana na si kupaniana, ugomvi, kuzozana au kuchezeana rafu za mchangani.

Wachezaji wanapocheza mechi hizo za watani wamekuwa wakicheza katika kiwango duni kutokana na uoga, kwamba wana hofu ya kuonekana wamehujumu hasa kama wakipoteza mpira.

Hilo si sahihi na kama timu itacheza kwa woga kila mmoja akitaka kumpa mpira mwenzake kioga na si kwa mipango, soka ya Tanzania itakuwa ni kwa ajili ya kuchekesha tu.

Hivyo wachezaji lazima waonyeshe uwezo na kuthibitisha kweli wanastahili kucheza katika timu hizo kongwe zilizobeba mioyo ya watu wengi wanaopenda soka nchini, hivyo kiwango ni jambo namba moja.

Wachezaji na viongozi, kumbukeni Watanzania wengi na hasa mashabiki wa soka hawana kiwango cha juu cha kipato.

Wanapojipinda na kuja kushuhudia mechi yenu, basi wanakuwa wamejichanga kupita kiasi na wengine wanasafiri kutokea mikoa mbalimbali ya Tanzania, basi wapeni burudani wanayostahili na si vituko ambavyo wakivihitaji, wataangalia runinga hasa vipindi vya wachekeshaji kama Kingwendu au King Majuto.




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic