March 23, 2015


Baada ya kuibanjua Mgambo JKT mabao 2-0, Kocha Mkuu wa Yanga, Mdachi, Hans van Der Pluijm, amefunguka kuwa Yanga ndiyo timu bora kwa sasa kutokana na matokeo mazuri wanayoyapata.


 Yanga juzi Jumamosi iliwaadhiri Mgambo JKT kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga kwa kuwafunga mabao 2-0 yaliyofungwa kwa vichwa na Mrundi, Amissi Tambwe pamoja na kiungo mshambuliaji, Simon Msuva.

Yanga chini ya kocha huyo imefanikiwa kushinda michezo yote mitano ya Ligi Kuu Bara iliyocheza nje ya Jiji la Dar es Salaam na kuweka rekodi ya kipekee.

 Ilishinda dhidi ya Mbeya City na Prisons kwenye Uwanja wa Sokoine, Mbeya kabla ya kuitungua Polisi Moro katika Uwanja wa Jamhuri, Morogoro, kisha kuzifunga Mgambo na Coastal kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

Kocha huyo wa zamani wa Berekum Chelsea ya Ghana, ameliambia Championi Jumatatu kuwa, Yanga ndiyo timu bora kwa sasa kutokana na kucheza vizuri katika kila mchezo.

 “Tumecheza vizuri katika mchezo huu, mara zote huwa tunacheza hivyo, ndiyo maana tunapata matokeo chanya, Yanga ndiyo timu bora, sisemi kwa sababu ni timu yangu bali matokeo yanathibitisha hilo.

“Mechi inayokuja tutacheza na Ruvu, ni timu ngumu lakini tunachotaka ni kushinda kila mchezo ili kusafisha njia ya ubingwa mwishoni mwa msimu na kufanya vizuri katika michuano ya kimataifa,” alisema Pluijm.


Yanga ndiyo timu pekee ya Tanzania iliyobaki katika michuano ya kimataifa ambapo inashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho na wikendi ijayo itapambana na FC Platinum nchini Zimbabwe. Awali, Yanga iliifunga timu hiyo mabao 5-1 jijini Dar.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic