May 8, 2015



Na Saleh Ally
MSHAMBULIAJI wa Tottenham Hotspur, Emmanuel Adebayor, ameamua kufunguka kupitia mitandao na kueleza matatizo kibao yanayowahusu ndugu zake.


Adebayor ameamua kuweka mambo hadharani baada ya kuchoka kuandamwa mfululizo na ndugu zake akiwemo mama yake mzazi.

Hadithi aliyoitupia mtandaoni inasikitisha kusikia dada yake akiipangisha nyumba ya Adebayor ambayo ameijenga kwa zaidi ya dola milioni 1.5 (Sh bilioni 3). Akamuacha dada yake aishi hapo, siku aliporejea, akakuta wapangaji.

Alipojaribu kumuuliza dada yake, akamporomoshea kashfa. Alipomshitakia kwa mama yake naye akamshushia maneno makali!

Kaka yake aliomba mtaji, alipompa hakuwahi kuanzisha biashara. Sasa anawasomesha watoto wake nchini Ujerumani, kila kukicha amekuwa akimshutumu ikiwemo kumzushia kuwa amechangia kifo cha kaka yake mkubwa, Peter.

Alimpa mama yake mtaji wa kutengeneza biskuti huku akiruhusu watumie jina na picha yake ili waweze kuuza. Wakashindwa.

Akachukua uamuzi wa kumlipia mdogo wake katika ‘academy’ acheze soka nchini Ufaransa. Miezi michache, akawa ameiba simu 21 kati ya wachezaji 27 aliokuwa akicheza nao.

Mwaka 2005, akaitisha kikao cha wanandugu na kutaka wamalize tofauti. Alipoomba ushauri wao, wakamueleza ingekuwa vizuri amnunulie nyumba kila mmoja wao na kuwa anawalipa mshahara!

Adebayor ameamua kufunguka. Ukweli huo ndiyo mfumo wa familia zetu nyingi za Kiafrika, uko hivyo lakini inawezekana ukawa ni tatizo kubwa kiutendaji kwa kuwa sisi wengi wetu ni wazembe na watu wa lawama.

Baada ya ujumbe mzito wa Adebayor alioutupia kwenye Mtandao wa Kijamii wa Facebook, nilizungumza na wasanii na wachezaji mbalimbali ambao walikuwa wakielezea machungu ya kuhusuana na ndugu ambao wanachangia hata wengine kukata tamaa.

Wapo ambao wameacha muziki au kukwama kisoka kutokana na kuanza kuona kazi zao ni kero. Wanaathirika kisaikolojia kwa kuanza kuona mafanikio ni kama sehemu ya kuwaudhi ndugu zao, hivyo bora kuachana nayo.

Wanaofikia uamuzi huo wakati mwingine hawajui kama wamefikia hivyo. Taratibu wanaanza kuonekana wanayumba na kwisha kabisa kimchezo au kimuziki. Ndugu lawama wasiojali mafanikio zaidi ya msaada, wanaweza kuwa kilevi ambacho kinachangia wachezaji au wanamuziki kuporomoka kwa kiwango chao kiutendaji na mwisho kwisha au ‘kufa’ kabisa.

Matatizo ya Adebayor ndiyo matatizo yanayomkuta staa yeyote awe wa muziki au michezo. Mfano kwa hapa nyumbani, Diamond Platinumz angekuwa muwazi, angeweza kukuambia ndugu au watu wa karibu wanavyoweza kuwa tatizo.

Kiungo kinda wa Simba, Jonas Mkude pia anaweza kuwa sehemu ya wale waliowahi kukutana na “ndugu lawama” ambao ni wavivu na waliojaa lawama. Si unakumbuka hivi karibuni aliingia mkataba mpya na Simba na kuingiza mamilioni ikiwa ni pamoja na kupata gari?

Adebayor ni shujaa zaidi, lakini hili liwe somo kwa wanamichezo, wasanii au hata waandishi wa habari kwamba maisha ya Kiafrika yana mengi ambayo yanaweza kuwakwamisha na ndugu wanaweza kuwa sehemu.

Ndugu wa Kiafrika wanaweza kuwa kama kilevi na kumfanya mchezaji kushindwa kufanya kazi yake katika kiwango ambacho ni sahihi.

Inawezekana hata utendaji wa Adebayor umekuwa ukiyumba kutokana na matatizo lundo ambayo yamekuwa yakimtokea. Ndiyo maana Didier Drogba akamshauri kuishi maisha anayoona ni sahihi na kuachana na kila mtu anayeamini anamchanganya au kutaka kumrudisha nyuma.

Kuna rafiki yangu mmoja, amefanya kila juhudi, kawaleta ndugu zake jijini Dar. Amekuwa akifanya juhudi ya kuwahudumia kila kitu. Mwisho anaambulia machungu kila kukicha hali inayomfanya akate tamaa.

Lazima tukubaliane kuwa ndugu wenye tabia ya kivivu na waliojaa lawama ni watu wanaozorotesha maendeleo ya michezo, burudani na hata maisha ya kawaida.

Waathirika wa ndugu wa aina hiyo ni wengi sana, lazima tukubali si Adebayor pekee. Uamuzi wa ujasiri aliouonyesha, basi unapaswa kuigwa na wengi na kuamini wanaoweza kukusaidia wanaweza kuwa wachache sana, hivyo hupaswi kuhofia wengi wasiokuwa na msaada kwako.

Muundo wa mifumo ya Kiafrika kweli ni tatizo, lakini wachezaji wa Kitanzania au Kiafrika ambao wamekuwa na hofu kuu hata kutaja kiwango cha mishahara yao kuwahofia ndugu, sasa wanapaswa kubadilika.

Ndugu wote hawawezi kuwa wabaya, lakini ni vizuri kuepukana na wengi wasiokuwa na faida, waache waishi maisha yao, hata kama kusaidia ni muhimu, ishi wewe kwanza.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic