May 18, 2015


UONGOZI wa Azam FC umeamua kumrejesha kocha Stewart Hall kwa mara nyingine kuongoza benchi la ufundi la kikosi hicho.


Hall anarejea Azam FC, hii itakuwa ni mara ya tatu baada ya kuondoka au kuondolewa mara mbili huko nyuma.

Taarifa nilizozipata ni kwamba, Hall, raia wa England, atasaini mkataba wa kufanya kazi Azam FC, leo na mara moja ataanza kupiga mzigo. Ninaamini hawatabadili hilo.

Kabla ya kufikia makubaliano, Hall ameuomba uongozi wa Azam FC kwamba kama unamtaka afanye nao kazi, basi lazima akubaliane nao kuhusiana na suala la timu ya benchi la ufundi.


Uongozi umekubaliana naye na sasa Hall anatua na kikosi chake kizima, akiwemo kocha bora wa makipa pamoja na mtaalamu wa chakula.

Uhakika wa hayo tutasubiri leo, tutajua kila kitu. Ninataka kuzungumzia ujio wa Hall kwa mara nyingine, maana nililazimika kuuliza ili kupata uhakika.

Kwamba vipi kocha huyo amekubali kurejea tena, lakini anatoa masharti ya kutaka kuwa na wasaidizi wake mwenyewe? Je, hawaamini waliopo?

Jibu nililopewa ni kwamba ilikuwa kazi ngumu kwa kocha huyo kufanya kazi zake kiufasaha na mara kadhaa alikuwa akizozana au kugombana na waliokuwa wakifanya naye kazi.

Rafiki wa kocha huyo alinieleza kwamba kulikuwa na mambo mengi ya “Kiswahili”. Watu walitaka kupeleka mambo ili mradi tu, kitu ambacho Hall hakukubaliana nacho hata kidogo.

Kitendo cha kukataa walichokuwa wakitaka, yaani aliotakiwa kufanya nao kazi, kilisababisha wamuanzishie zengwe na siku ya mwisho uongozi uliamini yeye ni tatizo, mwisho akaondolewa halafu akarudishwa tena.

Sasa amekubali kurejea, tena anarejea akiwa na timu ya watu anaowaamini kwamba watafanya kazi vizuri. Hapa ndiyo nimekuwa nikisema mara kadhaa, ingawa zinafanyika juhudi kubwa za kuyapinga kwa kuwatumia watu walaini wa fikra ambao wanakubali kirahisi kuandika lolote.

Kinachoonekana wanachotaka viongozi wakuu wa Klabu ya Azam FC na wanachokilenga waajiriwa wengi, kinaweza kuwa ni tofauti, hali inayosababisha wao kama timu kushindwa pamoja.

Inaonekana uongozi wa juu wa Azam FC unataka kuwekeza kweli. Unataka mambo yaende kitaalamu na ndoto walizonazo zifikiwe kwa kuifanya Azam FC kuwa mahiri, kubwa, gumzo Tanzania na Afrika nzima.

Wafanyakazi wake wengi wanaweza wakawa na mawazo hayo, lakini shida kubwa yamechanganyika na mengine ya umimi kwa kuwa wapo wanaotaka kufaidika kwa maisha yao binafsi.

Penye rikizi hapakosi fitna. Wafanyakazi wao kwa wao badala ya kuungana kama timu, wamekuwa wakipigana fitina na kusababisha kuifanya Azam FC itumbukie katika mifumo ileile ya Yanga na Simba, maana yake wanakuwa hawana tofauti tena.

Shida nyingine unaiona kwamba viongozi wa juu wa Azam FC, wako tayari kusikiliza maoni, wako tayari kujifunza ili kubadili mambo. Lakini waliopewa majukumu ya kuendesha klabu hawataki lolote kwa kuwa “wanajua sana!”

Kama malengo ni kufanikisha mafanikio ya Azam FC, suala la “hii ni rikizi ya nani” na kila mmoja anaitaka hadi kuingiza “fitna” kila mmoja akimpiga vita mwenzake, basi klabu hiyo itaishia katika umaarufu walionao Yanga na Simba ambao wao wanaweza kusema ni timu au klabu za wananchi.

Azam FC inamilikiwa na familia binafsi, tena wenye fedha na ndoto ya mafanikio, hivyo wanaofanya kazi hapo, lazima pia wajue bosi au mwajiri wao amelenga nini. Kama kweli wanapewa kila kitu kufanikiwa maendeleo, basi lazima wakubali kuachana na tabia zao walizokuwa nazo, halafu wabadilike na kutimiza ndoto hiyo.


Nasisitiza, mara kadhaa nimesema kuhusu hili. Mmepinga sana bila ya hoja ya msingi. Sasa Hall anarudi na kauli ya fitna au chuki inajirudia mara nyingine. Vizuri mkawasaidia hao waajiri wenu kutimiza ndoto zao kuliko kuangalia zaidi ndoto zenu za riziki!

1 COMMENTS:

  1. Unajua lazima tujue dunia inakwenda wapi, ajira ni tatizo duniani na wenzetu wamekuwa tofauti na sisi. Wanajua kitafutiana ajira!! Hall mara ya mwisho abaondoka wasaidizi wake walikuwa ni K. Ongara na muhindi ambao hakuna mswahili hata mmoja japo Kally amewahi cheza bongo na baba yake ni mbongo lakini ametumia muda mwingi uingereza na ni mwingereza. Kama ni viongozi atawakuta wale wale ukiondoa jemedari ambaye yuko TFF. Kwahiyo akisema majungu ni lazima atwambie yalikuwa wapi!! Alikuja maximo na msaidizi na wachezaji bado hakuwa na jipya zaidi ya kuwatafutia ajira ndugu zake. Tuache kuamini fikra za mzungu ni sawa hata kama anakosea, huo ni ukoloni wa akili. Aliondoka Mourinho chelsea na kurudi mara tatu, na yeye kuna majungu!? Kuna wakati ambao club inahitaji mabadiliko hata kama ya muda mfupi ili kurefresh na kuanza upya

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic