May 22, 2015


Na Saleh Ally
NITAPISHANA sana na nyie ndugu zangu, lakini hofu yangu mimi ni hofu yenu, kuwa watu waoga utafikiri hapa kwetu ni sehemu mbaya sana ambayo inahitaji kupambwa na watu fulani.


Watanzania wengi sana hawajui ubora wa nchi yao, ndiyo maana kulaumu kumekuwa dira ya wengi wakiamini huenda kila sehemu ni nzuri kuliko Tanzania.

Wakati mwingine kuna haja ya kujionea wenyewe, acheni kuamini kila kinachozungumzwa na wanasiasa, maana karibu kila mmoja anaponda tu Tanzania, hakuna anayesifia hata kidogo.

Watu kibao wangefurahia kuishi Tanzania bila ya kujali wanatokea wapi, iwe ni Ujerumani, Uholanzi, Japan, Uingereza na kwingine kote.

Sisi Watanzania ndiyo hatupaoni kwetu kama ni nchi nzuri ya kuishi. Kasoro hazitaisha, kila nchi ina kasoro lakini leo niwe mtu mwingine ambaye si mwanasiasa kuwa kwetu pazuri sana na tunapaswa kujiamini waungwana.

Samahani sana, nilianza kama mwanasiasa vile, lakini lengo ni kuwakumbusha kwamba tunaishi katika nchi bora kabisa ambayo unaweza kuishi maisha yako yote bila ya hata kutamani kwenda nje, hivyo tusitoe nafasi kwa wajanjawajanja kutuchezea wanavyotaka wao.
Mfano wa watu wanaotaka kuleta utani nasi ni Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Mart Nooij ambaye anaonekana kabisa anatuona kuwa bado tumelala.

Hizi zimekuwa hisia za watu wengi kutoka Ulaya, wanadhani bado tumelala. Hata Watanzania wanaoishi nje ya Tanzania hudhani sisi tumelala, sasa ni tofauti, wapo walioamka hata kuzidi wanaoishi Ulaya.

Huu ni wakati mwafaka wa Nooij kubeba mabegi yake na kwenda kwao Uholanzi ili Taifa Stars ifanyiwe mchakato mwingine mapema kabisa kabla ya kuingia kwenye kazi ya kuwania kucheza Kombe la Mataifa Afrika na pia Kombe la Dunia.

Stars ni timu ya hovyo, si kwa kuwa tu imepoteza mechi zake za Kombe la Cosafa kwa kufungwa na Swaziland na Madagascar lakini uliiona timu ilivyocheza?

Tungeweza kusema timu ilifungwa tu kutokana na kushindwa kutumia nafasi nyingi ilizopata lakini ilionyesha soka safi na la kuvutia.

Swaziland ilitawala na kuizidi Stars, ikashinda 1-0. Ikaja Madagascar nayo ikashinda mabao 2-0 huku ikitunyanyasa pia, ikiwa na mashambulizi mengi, ilimiliki mpira zaidi yetu.

Madudu haya huenda TFF wanakuwa waoga kwa vile wanataka kuwa watu wa kungoja au kuhofia kwamba wataambiwa walimtoa Kim Poulsen kwa kukurupuka lakini huu ndiyo wakati mwafaka wa kumpa ruhusa yule babu anayependa sana bia aende zake.

Tayari Nooij ameshasema soka letu ni maneno tu. Ameshaeleza namna anavyoondoka mapema kwenda zake kunywa bia. Anaonyesha kiasi gani anavyotudharau, lakini sisi tunataka tuendelee kukaa kimya.

Tukubali, TFF ni mali ya umma. Si binafsi na inawakilisha Watanzania na hata kipato chake kinatokana na Watanzania, iwe wamechangia kupitia viiingilio, wadhamini au hata Fifa kwa kuwa inatoa ikijua ni shirikisho la Watanzania.

Hivyo, TFF inapaswa kuonyesha ujasiri kwa kuwa kila dalili inaonyesha tutafeli mbele na ndiyo imekuwa ndoto ya Watanzania kufuzu kucheza Kombe la Mataifa Afrika. Kwa Nooij, hakuna tutakachopata kwa kuwa anaonyesha wazi hayuko ‘siriaz’.

Tanzania si sehemu ya Wazungu kuja kustaafu, tunahitaji watu wanaoweza kufanya kazi. Kama ingekuwa Stars ni kwa ajili ya kuwapa watu nafasi ya kustaafu, basi angalau tungewaachia wazawa kama akina Abdallah Kibadeni, Boniface Mkwasa na wengine nao wastaafu hapo wakipata huo mshahara.

TFF mnaweza kuwa mnahofia, basi mimi naweza kuwasaidia katika suala la kubeba mabegi ya Nooij ili nimpelekee huko Afrika Kusini. Leo akimaliza mechi ya ‘kirafiki’ dhidi ya Lesotho ambayo hata akishinda ni kazi bure, abebe mabegi akawasalimie kwao.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic