May 22, 2015

HANS POPPE

Na Saleh Ally
KAMATI ya Usajili ya Simba inaongozwa na wakongwe kabisa katika masuala ya mpira. Mwenyekiti ni Zacharia Hans Poppe na makamu wake Kassim Mohammed Dewji.


Wawili hao wamechanganyiwa vijana ambao nao wana damu changa na wana nafasi ya kuendelea kufanya mambo ya usajili kwa ufasaha kabisa.

Ukiachana na hivyo, kamati hiyo, bado inaweza kufanya vizuri kwa msaada wa kocha. Iwe ni ripoti ya Goran Kopunovic ambayo aliiacha, au kocha mpya atakayekuja.

Kwa kutumia wakongwe hao na vijana ndani ya kamati, pia ujuzi wa kocha, hii ni nafasi nzuri sana kwa Simba kupata kikosi bora zaidi.

Maoni, ni jambo jema katika kila jambo la watu. Iwe Dewji au Hans Poppe, au vijana wao wanaweza pia kupokea maoni na kuyafanyia kazi na mwisho wao ndiyo wenye uwezo wa kuangalia yapi ni sahihi na yapi si sahihi.

Wao ndiyo watafanya kazi ya kuchuja na mwisho watapata vitu ambavyo ni sahihi na kuyafanyia kazi, lakini si kila mwenye nafasi ya uongozi Simba anataka kufanya usajili.
 
DEWJI AKIWA NA DALALI...
Usajili wa Simba una vurugu kubwa. Hili limetokea kwa misimu mitatu sasa. Misimu miwili wakati wa uongozi wa Ismail Aden Rage na msimu mmoja ndani ya uongozi wa Evans Aveva

Misimu miwili ya Rage, usajili wa Simba ulikuwa hovyohovyo, kila mtu alipeleka mtu wake. Kila mmoja aliona anajua zaidi ya kocha ilimradi mtu wake asajiliwe.

Mwisho ikafikia viongozi wakaanza kugombea wakitokea kwenye picha ili mradi waonekane wameshiriki kumsajili mchezaji fulani hivi. Kitu ambacho kilikuwa upuuzi tu, maana mwisho wake Simba haikufanya lolote licha ya rundo la wachezaji waliosajiliwa.

Baada ya misimu hiyo miwili, chini ya uongozi wa Aveva, ikaonekana mambo yatabadilika kwa kuwa watu wengi walio kwenye uongozi ni wale waliokuwa wakijua kusajili, kwamba kama wakimtaka fowadi mkali kama Saleh Ally, basi lazima watampata.

Ajabu! Wao nao wakawa walewale, usajili sasa ukawa haueleweki unafanywa na nani. Badala ya kamati ya usajili kufanya kazi yake, ikaonekana suala la usajili limekuwa la kamati ya utendaji ambayo ina watu wengi mno.

Kamati ya mashindano inasajili, kamati ya fedha nayo inasajili, sasa ikawa ili mradi. Makamu wa Rais naye anasajili, mwenyekiti wa kila kamati naye anafanya usajili.

Dalili za kuonyesha Simba watachemsha zilijionyesha mapema. Nikaandika makala kuwakumbusha kwamba wana kila sababu ya kuheshimu uamuzi wa kocha, pia kuipa nafasi kamati ya usajili ifanye kazi yake na wao ruksa kupeleka maoni yao.

Nawajua walioponda, wakiamini kuiachia kamati pekee haikuwa sahihi. Wakajiamini wanaweza kubadili mambo na kusimamia usajili, mwisho tumeona. Simba imepoteza rundo la fedha kusajili wachezaji watano wa Uganda, mwisho wa msimu imetema wawili na bado mmoja amebaki “kimungu” tu.

Sasa ni wakati mwingine tena ambao Simba inaanza usajili. Viongozi ambao hawahusiki na usajili wangepunguza kiherehere, halafu wawape nafasi kamati ya usajili wafanye kazi yao.

Sehemu ambayo wanaamini wanaweza kuwapa maoni basi wanaweza kufanya hivyo na kuwaachia wafanye kazi yao.

Kuendelea kulazimisha wachezaji fulani wasajiliwe kwa kuwa ni watoto wa wajomba zenu, watu ambao wanawaheshimu sana au mnataka kulipa fadhila kwa kuwa ni watoto wa michepuko yenu, si sahihi, mnaiumiza Simba na mashabiki wake.

Lazima mjue mashabiki na wanachama wa Simba, wameumia sana. Huu ndiyo wakati mwafaka kwa uongozi wenu kurudisha imani kwao kwamba umefika wakati wao pia kubadilika. Acheni longolongo, wapeni wenzenu wafanye kazi yao na kama mna mawazo, wafikishieni si kujidai kila mtu anajua na hili ndiyo jambo linaloikwamisha Simba, mnaamini mnajua sana wakati wengine hamna lolote.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic