July 14, 2015


Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Charles Boniface Mkwasa ameonyesha kuumizwa na maneno yaliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete.


Wakati akilifunga Bunge la Jamhuri ya Muungano. Kikwete aliamua kuwa wazi na kusema aliamua kuacha kwenda uwanjani kuiunga mkono Taifa Stars kutokana na kupoteza michezo mfululizo.

Kikwete alisema mara kadhaa alipokuwa akienda uwanjani, Stars ilikuwa ikipoteza hadi kufikia kuona watu wanaweza kuona yeye ana bahati mbaya ndiyo maana timu inafungwa kila mara.
Hali hiyo ilimfanya Mkwasa ajitokeze na katika maneno yake alisisitiza kuwa ni wakati mwafaka kwa Kikwete kurudisha imani yake kwa Stars kwa kuwa imebadilika.

Mkwasa anakuwa kati ya Watanzania walioguswa na maneno ya Kikwete ambaye amekuwa mkweli na kujiweka wazi kwamba anakerwa na mwenendo wa Stars.
MKWASA.

Hakika unakera na hata baada ya kuingia kwa Mkwasa, katika mechi yake ya kwanza ambayo ilikuwa dhidi ya Uganda, Stars ilipata sare.

Maana yake, hakuna chochote cha kujivunia hadi sasa. Kama ni mabadiliko anayoyasema Mkwasa, si thabiti au yanayoweza kuonekana na kusema kweli yamepatikana.

Bado, ndiyo safari inaanza. Kikubwa ni kumuunga mkono yeye na kikosi chake na yeye na wenzake wajitume kuwaonyesha Watanzania kwamba hawajakosea kuwaunga mkono.

Kikubwa wakumbuke, mafanikio yatakuwa sehemu ya kurudisha imani yao kwa Watanzania. Lakini kama watafeli katika hilo, basi mwisho uvumilivu utawaisha wale wanaowaunga mkono.

Pamoja na Mkwasa, wadau wengine nao wanapaswa kuumizwa na jambo hilo. Hakika ni gumu kuendelea kulibakiza moyoni huku ukiona timu ya taifa lako ikigeuzwa kichwa cha mwendawazimu.

Kufeli kwa Stars hakujaanzia kwenye kikosi pekee, viongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), lazima wawe kitu kimoja pia.
TAIFA STARS
Huenda wale wa juu wanaweza kuwa wanatamani kuona mafanikio yanapatikana na wakafanya kila linalowezekana.
Lakini wengine ambao wako ndani ya shirikisho hilo kwa ajili ya maslahi yao binafsi wakawa tayari kuiona timu ikifeli ilimradi wao wanafaidika.

Lazima tukubali, Stars si ya TFF, ni ya Watanzania wote wapenda maendeleo wa mchezo wa soka. Lakini haiwezi kupiga hatua kama waliopewa dhamana wako kwa ajili ya matumbo na mioyo yao.

Kuna kila sababu ya kila mmoja kuwa mkweli, kuipigania Taifa Stars na kama tabia za ubinafsi, ujivuni, kujiamini kwa kipuuzi kutaendelea. Basi Stars haitapiga hatua hata kidogo.
Mwisho itakuwa hivi, Rais Kikwete amekuwa wa kwanza kuacha kwenda uwanjani, baadaye atafuatia Saleh Ally, halafu wewe, yule na mwingine na siku moja, timu hiyo itacheza uwanjani bila ya mashabiki!



Kikosi


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic