August 22, 2015


AZAM FC na Yanga leo zinacheza mchezo wa Ngao ya Jamii kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, gumzo kubwa katika mchezo huo ni straika Donald Ngoma na beki Pascal Wawa.

Ngoma, raia wa Zimbabwe, anaonekana kuwa ndiye atakayeibeba Yanga katika mchezo huo huku Wawa wa Azam akitabiriwa kuwa mtu atakayeweza kuizuia safu ya ushambuliaji ya wapinzani wao.

Wawa, raia wa Ivory Coast, ana nguvu, anajua kumiliki mpira na ukimuendea vibaya hata chenga anakupiga, hivyo kazi itakuwepo kati yake na Ngoma mwenye nguvu pia na uwezo mkubwa wa kuwalamba chenga mabeki.

Hata hivyo, mchezo huo unaweza kuvurugika zaidi kwani kuna uwezekano wawili hao wakacheza kwa kukamiana zaidi na kutolewa kwa kadi nyekundu au mmoja wao kuumia mapema jambo ambalo Hall na Pluijm wameshalifanyia kazi.

Hata makocha wa timu hizo, Stewart Hall wa Azam na Hans van Der Pluijm wa Yanga, wanafahamu hali hiyo na kila mmoja amemuandaa mchezaji wake kupambana ili kupata ushindi ambao ni lazima upatikane hata kwa njia ya penalti.

REKODI YAO NGAO YA JAMII
Mchezo wa Ngao ya Jamii hukutanisha timu bingwa na iliyoshika nafasi ya pili msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara, Yanga ndiye bingwa na ya pili ilikuwa Azam.

Hii ni mara ya tatu kwa timu hizi kukutana na katika mara mbili walizokutana, Yanga ilishinda mechi hizo. Mwaka juzi Yanga ilishinda bao 1-0 lililofungwa na Salum Telela na mwaka jana katika mchezo huo, Wanajangwani walishinda mabao 3-0 yaliyofungwa na Simon Msuva na Geilson Santos ‘Jaja’ aliyefunga mawili.

Wiki chache zilizopita, katika robo fainali ya Kombe la Kagame, kwenye Uwanja wa Taifa, Yanga ilifungwa kwa penalti 5-3 baada ya kutoka suluhu na Azam. Hadi leo tambo kwa mashabiki wa timu hizo zinatawala mtaani.
Kipigo hicho ni cha pili kwa Yanga ndani ya miezi mwili iliyopita kwani Mei 6, mwaka huu katika mchezo wa Ligi Kuu Bara, Azam ilishinda mabao 2-1.
Mechi ilichezwa katika mvua na ilionekana kama Yanga ‘iliachia’ ili kuiruhusu Azam ipate pointi tatu za kuiwezesha kushika nafasi ya pili badala ya Simba.

BUSUNGU AINGILIA KATI
Wakati mashabiki wengi wakisubiri kutazama ‘sinema’ ya Ngoma na Wawa, Yanga ipo makini kwa kuwapa makali zaidi washambuliaji wake wengine kama Malimi Busungu na Amissi Tambwe.

Busungu ameliambia Championi Jumamosi: “Siogopi lolote katika mchezo huu, nasikia Azam wana beki imara ila na sisi tuna fowadi kali inayoweza kuwapenya.”

Hii inamaanisha kwamba, wakati Ngoma na Wawa wakiwa ‘bize’ na vita yao huku Busungu na Tambwe watakuwa wakifanya vitu vyao wakipambana na mabeki wengine waliobaki ambao ni Aggrey Morris na Said Morad kwani kuna uwezekano Hall akawachezesha mabeki watatu wa kati.

AZAM YAJIFICHA, HALL ATAMBIA ULINZI
Jana asubuhi, Azam ilizuia mtu yeyote kutoingia kwenye uwanja wake wa Azam Complex ili kutobaini mbinu zake za ushindi huku Kocha Hall akionekana kuwa makini na uchezaji wa pasi fupifupi.

 Hall amesema: “Hii ni mechi kubwa, si lazima kila kitu kiwe wazi, lakini niseme tu kuna marekebisho makubwa niliyofanya baada ya Kagame.

“Naiamini safu yangu ya ulinzi, itafanya vizuri na kuweza kuizuia safu yoyote ya ushambuliaji, japokuwa katika soka lolote laweza kutokea, tunachotaka ni kufanya vizuri na kuweka heshima katika mechi zetu za Ngao ya Jamii.”

YANGA YATULIZA PRESHA
Kocha raia wa Uholanzi, Pluijm amesema amejitahidi kwa kiasi kikubwa kupunguza presha kwa wachezaji wake ili waweze kufanya vizuri katika mchezo huo.

Pluijm ambaye pia kikosi chake kimefanya mazoezi ya siri wiki hii kwenye Uwanja wa Chuo Kikuu cha Polisi, Kurasini jijini Dar es Salaam, alisema:

“Hii ni mechi kubwa, ni ngumu kutabiri matokeo yake, mimi nimewaambia wachezaji wangu wapunguze presha ili tushinde mechi hii na kulinda heshima ya ubingwa tunaoushikilia.

“Hatutaki tuwaze sana kuhusu matokeo yaliyopita, makosa yote ya mchezo uliopita na kuwasoma wapinzani wetu ni miongoni mwa vitu tulivyovifanyia kazi.”

ULINZI BOMBA, MAMBO DAKIKA 90 TU
Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Baraka Kizuguto, ameliambia gazeti hili kwamba: “Ulinzi ni wa uhakika, kutakuwa na polisi wengi na walinzi wengine.

“Mchezo huu utaanza saa 10:00 na dakika 90 zikiisha kama timu hazitafungana zitapigwa penalti.”

TFF pia imembadilisha mwamuzi Israel Nkongo na sasa mchezo huo utachezeshwa na Martin Saanya kwani Nkongo anasumbuliwa na maumivu ya misuli.

VIKOSI:
Azam: Aishi Manula, Himid Mao, Erasto Nyoni, Aggrey Morris, Pascal Wawa, Said Morad, Jean Baptiste Mugiraneza ‘Migi’, Shomari Kapombe, John Bocco, Kipre Tchetche na Farid Mussa. 

Yanga: Ali Mustapha ‘Barthez’, Juma Abdul, Haji Mwinyi, Vincent Bossou, Kelvin Yondani, Thabani Kamusoko, Deus Kaseke, Haruna Niyonzima, Donald Ngoma, Amissi Tambwe na Simon Msuva.
Mohammed Mdose, Said Ally na Khadija Mngwai.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic