October 5, 2015



MWANASIASA mkongwe nchini, Kingunge Ngombale Mwiru, jana alitangaza rasmi kujitoa kwenye Chama Cha Mapinduzi (CCM) na akasisitiza kwamba haendi chama chochote.


Kingunge aliyewahi kutabiri anguko la chama hicho kikongwe nchini, sasa ana umri wa miaka 85 na ameamua kujitoa CCM ambayo ni kati ya walioanza nayo baada ya muungano wa Tanu na ASP uliozaa CCM, Februari 5, 1977.

Kingunge aliwahi kuwa mmoja wa memba wa Bunge la Tanzania kwa vipindi viwili tofauti lakini alikuwa kati ya sehemu kubwa waongoza mapambano ya CCM ingawa si kipindi hiki.

Wakati Kingunge anatangaza kujitoa, kimekuwa kipindi ambacho kampeni za vyama zikiwa zimepamba moto na ndiyo maana unaona leo ni gumzo kuondoka kwa mzee huyo.

Kujitoa kwake, kwetu wanamichezo si ishu sana, kuliko tungesikia timu yetu ya taifa, Taifa Stars imefuzu kucheza Kombe la Mataifa Afrika (Afcon) au lile la dunia.

Ndiyo maana wakati wengi wakiwa wametekwa na suala la kujitoa kwa Kingunge CCM, mimi nikaanza kuwaza miaka yote ile, leo ameondoka bado Taifa Stars haijafuzu tena Afcon, wala haina mpango na Kombe la Dunia.

Angalau ingekuwa inaweza kufuzu, Kingunge bado angeiona akiwa nje ya CCM. Tujiulize kwa sasa Stars ina dalili hata za kufuzu michuano hiyo mikubwa?

Michuano mikubwa kwa timu yetu sasa ni ile ya Chalenji ambayo ni michuano ya kanda na mara nyingi inaendeshwa “kimagumashi tu”. Hatuna kipi hadi tushindwe kufika Afcon au Kombe la Dunia?

Sasa Kingunge ameondoka, anakwenda wapi, anajua mwenyewe, lakini Taifa Stars haina nafasi ya kufuzu, haina uhakika na hakuna dalili yoyote kwamba kuna nguvu za dhati mwaka fulani uwekwe kama mpango madhubuti kwamba iwe isiwe, lazima Stars icheze Afcon au Kombe la Dunia.

Achana na Afcon, Kingunge ameondoka CCM hajawahi kuiona Taifa Stars ikipata nafasi ya kucheza Kombe la Dunia. Ingawa sijui anashabikia timu gani, nafikiri hata kama ataenda Ukawa, bado hatapata nafasi ya kuiona Stars inacheza michuano hiyo mikubwa.

Sina maana Kingunge hataiona Stars ikifika Kombe la Dunia kwa kuwa ana miaka 85, lakini hata mwenye umri kama wangu, kama nitaajaliwa kufikia nusu ya umri wa Kingunge bado inaonekana hakuna matarajio na hatuwezi kuyafikia kwa kuwa kila uongozi unaoingia Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), unaona ni kama jambo gumu sana.

Kama ni jambo gumu sana, haliwezekani, sasa nani atatusaidia kufuzu? Jibu ni kwamba tutakwama na mambo hayatawezekana kabisa.

Angalia wadau wengine, viongozi kibao wa soka wanaingia madarakani lakini wanaonekana wamepania kwelikweli kufanikisha malengo yao binafsi. Najua utaniuliza kwamba viongozi wa klabu ipi na ipi?

Nakukumbusha, nchi yoyote ikiwa na kiwango cha juu kisoka, au ikauza wachezaji wengi, watakuwa msaada mkubwa katika kikosi chake cha timu ya taifa na kitakuwa imara sana.

Viongozi wa klabu kama wangekuwa na mikakati, wakawa na timu bora, zenye ushindani mkubwa Afrika kama ilivyo TP Mazembe, Enyimba enzi hizo, Al Ahly, Zamalek na nyingine, lazima kungekuwa na kikosi bora kabisa cha timu ya taifa.

Tunaona Uganda wanavyosaidiwa na wachezaji wengi wanaocheza nje na angalau wamekuwa na mwelekeo wa ushindani. Hali kadhalika Kenya angalau wanatangaza jina lao hadi katika Ligi ya England ‘Premier’ kutokana na wachezaji wao. Wamebakiza vitu vichache tu, wakivibadili watapiga hatua.

Oktoba 7, Taifa Stars inaanza mbio za kuwania kucheza Kombe la Dunia kwa kuivaa Malawi. Huenda inaweza kuwa nafasi nzuri ya kumuonyesha Kingunge angalau aingie kwenye bahati ya kuiona Stars ikifanya vizuri.

Msisubiri arudi CCM ambako amelia ujana wake wote bila kuinoa Stars ikicheza michuano mikubwa ya kimataifa. Huenda bora kumpa zawadi ya uzeeni akiwa nje ya CCM na hakuna haja ya kusubiri hadi Kingunge aamue tena kurudi CCM!



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic