October 14, 2015


Na Saleh Ally
RAIS wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amezungumza mambo mengi sana mazuri wakati wa sherehe wa kukabidhiwa tuzo maalum na Chama cha Waandishi wa Habari wa Michezo (Taswa) zilizofanyika kwenye Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam, juzi.


Kikwete alipewa tuzo kutokana na mchango wake mkubwa katika michezo katika kipindi chake cha uongozi kwa miaka 10 ambacho kinafikia tamati mwezi huu.

Hakuna anayeweza kulikataa hilo, hata kama haukuwa mchango wa kutosha, lakini si haba, alijitahidi.

Wakati wa mkutano huo, akitoa hotuba yake, Kikwete aliwavutia watu wengi sana kwa kuwa alizungumza vitu vingi kuhusiana na michezo ndani na nje ya Tanzania. Wengi wakawa wakisema chinichini: “Jamaa mfuatiliaji, kweli anaijua michezo.”

Kikwete ni mwanamichezo hasa, ndiyo maana amekuwa tayari kuwalipia makocha wa timu za taifa za soka, riadha, netiboli na kadhalika na alieleza sababu ya kufanya hivyo kwamba kuwapa watu mwalimu ni zawadi kubwa.

Wakati Kikwete anazungumza kuhusiana na kocha, alieleza namna ambavyo Kocha wa Taifa Stars, Charles Boniface Mkwasa anavyofanya kazi na kusema ameanza vizuri kwa kuing’oa Malawi katika kuwania kucheza Kombe la Dunia 2018.

Pia akasisitiza kwamba Tanzania inakutana na Algeria ambayo ina wachezaji wakali hasa na inahitaji juhudi ya uweledi kupambana nao na kuwang’oa kwa kuwa wakati wa Kombe la Dunia mwaka 2014 nchini Brazil, Algeria ilimaliza michuano hiyo ikiwa timu bora ya Afrika. Kweli Kikwete ni mfuatiliaji.

Lakini akasisitiza kwamba mshahara alioutoa wa kocha wa Taifa Stars, hakuwahi kusema alipwe hadi atakapokuwa mzungu au raia wa kigeni, maana yake hapa, Mkwasa apewe mshahara wake.

Mshahara anaotakiwa kulipwa Mkwasa ni Sh milioni 25 kwa mwezi ndicho alichotoa Kikwete. Sasa vipi inaonekana kumeanza na uzungushwaji wa mambo.

Hata kabla Mkwasa hajaingia mkataba na TFF, kulionekana kuna figisu zinatembea. Nilianza kufanya uchunguzi na kugundua kwamba suala la mshahara wa kocha huyo linakwama katika Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo.

Nilizungumza na ofisa mmoja wa wizara hiyo ambaye alisema kwamba wanashughulikia ingawa hakutaka ifanywe habari. Bado hawakuwa wamekubali kuutoa mshahara huo hadi Kikwete ameamua kuzungumza.

Nafikiri sasa siyo siri tena, wanapaswa kumlipa Mkwasa mshahara wake wa nyuma, wamlipe baada ya kuingia mkataba na pia stahiki kama nyumba wampe.

Kocha Kim Poulse kutoka Denmark, alikuwa akiishi Masaki, hali kadhalika Mart Nooij ambaye alikuja ‘kufanya utalii’ Tanzania. Sasa angalau Mkwasa ameanza kuonyesha njia. Kwa kuwa ni mzalendo ndiyo hastahili kupata lolote?

Watanzania tunapenda kujidharau, huenda kutoka wizarani kwenda kumlipa kocha wa Kizungu kama Poulsen au Nooij ilionekana ni jambo la kawaida na huenda anayehusika  na ulipaji aliona ni jambo zuri sana.

Kwa kuwa sasa ni mzalendo, basi mizunguko inakuwa mingi. Taarifa nyingine za uchunguzi zinaonyesha hata funguo za nyumba zinashikiliwa wizarani. Sasa huu ndiyo wakati mwafaka, nazo apewe kwa kuwa ni haki yake.

Kauli ya Kikwete kwamba alitoa mshahara kwa ajili ya kocha wa Taifa Stars bila ya kujali ni Mtanzania au la inaonyesha kiasi gani yeye anaweza kuwaamini makocha wazalendo.

Mkwasa si Mungu, kama ni binadamu naye siku itafikia atakosea, na hatutasita kumueleza. Lakini kwa sasa, mimi naendelea kusimama mstari wa mbele kwa kuwa nilishaanza, apewe haki zake ili tuonyeshe tunawajali na kuwathamini wanamichezo wazalendo wa hapa nyumbani.

Wanaohusika na malipo ya kocha huyo, watimize hilo kwani hata anayetoa amelipita hilo tena kwa kuonyesha heshima kwa Watanzania. Sasa anayetaka kuzuia ni nani?

Angalizo, si kwa kuwa Kikwete anamaliza muda wake, basi ndiyo iwe nafasi ya kutaka kulizungusha hilo hadi lishindikane. Kama kuna ambaye alikuwa hataki kumlipa, basi amlipe ili iwe sehemu nyingine ya motisha kwake.

Mechi dhidi ya Algeria ni ngumu, msimpe nafasi Mkwasa apate kisingizio. Tafadhari mumlipe fedha yake kwa wakati mwafaka maana aliyejitolea kumlipa, ameshaweka mambo hadharani.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic