November 30, 2015



Na Saleh Ally
JANA nilianza kuchambua namna nilivyogundua wachezaji wa Taifa namna ambavyo hawakuwa na nidhamu kwa kiasi kikubwa katika kambi kama vile kuchelewa wakati wa chakula, kupanda basin a hata kuchelewa kulala huku wakichati kupitia mitandao ya Facebook, Instagram na Whatsapp.


Maana yake hawakuwa wakipumzika, huku wakijua wataamkaa asubuhi na mapema kwa ajili ya kifungua kinywa, pia kwenda mazoezini. Sasa watu gani hawa wanataka kuchungwa kama ng’ombe ili waishi katika utaratibu sahihi. Tena wakiwa katika kiwango cha timu ya taifa? Upuuzi kabisa.

Niliishia pale walipokuwa wakisimuliana kuhusiana na akina Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu ambao wanachezea TP Mazembe. Kwamba nidhamu yao, iliwavutia na wengine walitamani kufanya hivyo.

Mimi sikuwahi kuwaona Ulimwengu na Samatta wakifanya hivyo, ila wachezaji na baadhi ya memba wa benchi la ufundi walisema kama saa ya chai ni 1:30 asubuhi, basi wachezaji hao wa TP Mazembe wangekuwa eneo husika saa 1:20 asubuhi wakisubiri kwa dakika 10 nzima, muda ukitimia wanaanza kazi ya kula. Hali kadhalika, hata upandaji basi kwenda mazoezini au kwenye mechi, wangekuwa pale chini dakika 5 hadi 10 wakisubiri kuingia. Wakati wengine wangeingia baada ya muda wa kuondoka kupita!

Sasa wanasimuliana, wanakubali wanachofanya wenzao ni bora lakini kutumiza hawawezi.
Wachezaji walipewa siku mbili za kufanya manunuzi. Siku ya tatu, Mudathir Yahaya alimfuata kiongozi wa msafara, Msafiri Mgoyi akiomba akafanye shopping tena. Akakataliwa, tena akiambiwa huo ni mzaha.

Siku ya safari, tulitakiwa kuwa uwanja wa ndege saa saba. Lakini saa tano tuliondoka hotelini, tukafika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Oliver Tambo saa zima kabla ya desk la Fastjet halijafunguliwa ili tuanze kukatiwa tiketi maalum kwa ajili ya kuingia kwenye ndege.

Kwa pamoja tulisubiri kwa saa zima, walipofungua tulipeleka ombi ili mtu mmoja atuhudumie maana tulikuwa timu nzima, likakubaliwa lakini kijana yule wa Kisauzi, alikuwa anafanya mambo yake taratibu.

Licha ya kuwa nimeishapata tiketi yangu, mimi niliamua kubaki kati ya watu wa mwisho kuhakikisha wenzangu wote wameingia na mwisho baada ya yule kijana wa shirika la ndege kumaliza, nikaongozana na baadhi ya maofisa wa TFF, memba wa benchi la ufundi moja kwa moja, kwenda kwenye ndege.

Ajabu! Wakati tunaingia ndani ya ndege, kila abiria akiwa ameishaingia, wachezaji wa Taifa Stars, hata walimu wao hawakuwa wameingia ndani ya ndege. Mmoja wa maofisa wa TFF tuliokuwa tukisaidiana nao pale kwenye desk kuhakikisha wachezaji na makocha wanakuwa wa kwanza kuingia, akadhani tumekosea ndege.

Kazi ya kuanza kuwapigia simu ikaanza, dakika 10 baadaye walikuwa katika ndege. Walidai walikuwa wanamalizia kula! Tiketi kawaida zinaandikwa muda wa kuingia kwenye ndege, pia muda wa kuondoka, ninaamini wote wanajua kusoma namba!

Baada ya kuona kazi imeisha, wakati maofisa wa Fastjet wanataka kufunga mlango, ikagundulika abiria watano walikuwa hawajaingia ndani ya ndege! Wachezaji waliokuwa ndani ya ndege wakasema John Bocco na Shomari Kapombe ndiyo walikuwa hawajaingia, mbaya zaidi hawakuwa na simu zenye namba za Afrika Kusini na wakati huo hawakuwa na ‘bando’ maana walitumia internet ya hotelini.

Maofisa wa Fastjet walijitahidi kusubiri kwa dakika 15. Wakasema sasa ni muda wa kuondoka kwa kuwa kuendelea kuchelewa, walikuwa wakilipa ushuru wa uwanja zaidi.

Ukiwaacha wachezaji hao itakuwaje? Tena wachezaji wamesema ameongezeka na Himid Mao, sasa ni watatu. Dakika tano baadaye wakasema yumo na Aishi Manula.
Mimi na ofisa mmoja wa TFF tulisimama na kusema ndege haitandoka, kama imeshindikana washushe mizigo ya sisi sote. 

Kwao angalau ikawa mtihani, tukaomba wamruhusu Baraka Kizuguto ashuke kwenda kuwatafuta na mimi nina simu kwa namba ya Afrika Kusini kama ilivyo kwake, ingekuwa lahisi kuwasiliana naye.

Zilishafika dakika 20 na ushee, Kizuguto alipewa dakika 5 za kwenda kuwafuata, jamaa walifanya hivyo huku wakijua walikuwa wakivunja kanuni za mambo ya anga.

Dakika tano zilipita, Kizuguto hakuwa amerudi na wachezaji walikuwa hawajaonekana, nilipompigia akasema hajawapata naye alikuwa njiani anarejea katika ndege.

Maofisa wa Fastjet uvumilivu ulikuwa umewashinda na sasa walisema hata sisi kama tunataka, basi tukashushe mizigo yetu tubaki kwao poa tu maana ‘tuliishawazingua’ vya kutosha.

Dakika tano baadaye, tuliowana wachezaji hao wanakuja wakiwa wamebeba rundo la mifuko baada ya kupiga shopping ya uhakika, tena hawakuwa wanne, walikuwa watano, aliongezeka Mudathir ambaye watu walimsahau.

Ndani ya ndege tayari kulikuwa na tafrani kati yangu na baadhi ya abiria wazungu ambao walikuwa wakilaamini kucheleweshwa na walikuwa na haki. Tena walisisitiza wachezaji wetu hawakuwa na nidhamu kwa kuwa hawajui hata kujali muda.

Wachezaji wakati wanaingia ndani ya ndege walitoa sababu ya kijinga kabisa. Eti walipotea, jambo ambalo lilikuwa haliwezekani kwani walikuwa wanaongozana wakati wanaingia ndani ya ndege, vipi wengine wapotee wakati ni msafara wa watu wengi?

Tena kitu kibaya zaidi, wote watano walikuwa wanatokea klabu moja ya Azam FC ambalo si jambo zuri kwa uongozi wa klabu.
Lazima tukubali wachezaji wetu pia ni sehemu kubwa ya tatizo, kwamba kama wao hawatabadilika hata taifa Stars ikipewa nini haitawezekana.

Tunataka kukuza vijana, ndiyo ni jambo jema. Lakini kuwakuza bila kujadili misingi sahihi na kutumia wataalamu wa uhakika ni kupoteza muda.

Wachezaji wa Stars hasa waliokuwa wakifanya madudu, asilimia 90 ni hao wanaoonekana makinda au vijana kwa kuwa wengi wana miaka 20 hadi 26. Sasa vijana, lakini si wale waliokulia katika mazingira sahihi.


SOMA SEHEMU YA SABA AMBAYO NDIYO YA MWISHO.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic