November 13, 2015




Na Saleh Ally
RAIS John Joseph Pombe Magufuli amekuwa na sifa ya kutokuwa shabiki wa michezo lakini mara kadhaa yeye amekuwa akieleza namna ambavyo amekuwa shabiki wa michezo mbalimbali na aliwahi kuwa kipa.


Kila binadamu ana haki ya kuchagua anachotaka, lakini linapofikia suala la majukumu, sasa inakuwa ni uwajibikaji badala ya kufurahisha nafsi kutokana na unachokihitaji.

Bado sijawa na uhakika wa asilimia mia kwamba Magufuli ni shabiki wa mchezo gani, au anaipenda michezo kwa kiasi kipi au kiwango kipi.

Ninaweza kusema kwamba kwa mara ya kwanza ameanza na soka kwa kuonyesha anaipenda michezo au anaithamini na kuipa heshima ya juu kama sehemu ya kipaumbele.

Magufuli amekubali kuwa mgeni rasmi katika mechi ngumu ya kimataifa wakati Taifa Stars itakuwa inakutana na Algeria ambao ni vinara au wababe wa Afrika kisoka.
Timu ambayo michuano ya mwisho ya Kombe la Dunia iliyofanyika nchini Brazil, ilikuwa kinara kwa timu za Afrika.

Timu ambayo ni moja ya zile zilizoshiriki Kombe la Dunia mara nyingi ikitokea barani Afrika. Stars inakwenda kukutana nayo, kupambana nayo na kulenga kuisimamisha. Magufuli ameonyesha si mwoga kama baadhi ya viongozi ambao wamekuwa na hofu kama timu ikifungwa, wao wako itaonekana kama hawakuwa wamesaidia.

Magufuli anajua vijana wa Taifa Stars wanakwenda uwanjani kupambana na Algeria ambayo ni sawa na vita ya Daudi na Goliath. Amekubali kuungana na watoto wake ambao ni kina Daudi kwenda kupambana na mbabe huyo wa Afrika.

Magufuli anaungana na Watanzania watakaokwenda uwanjani, kuwa sehemu ya wapambanaji katika mechi hiyo ngumu kuliko zote ambayo Stars inakutana nayo mwaka huu.

Hata ingekuwa Nigeria, Ghana au Ivory Coast wanakutana na Algeria. Lazima wachezaji wao nyota kama Yaya Toure na wengine, wangelazimika kujiandaa maradufu kwa kuwa wanajua mziki wanaokutana nao, hauchezeki kiulaini.

Magufuli ametoa heshima kubwa sana kwa Taifa Stars, wapenda soka na wapenda michezo kwa ujumla. Kazi itabaki kwao wachezaji, makocha wa timu pamoja na Watanzania wenyewe wanaokwenda uwanjani Jumamosi kuishangilia timu kwa nguvu ili Rais Magufuli aone yuko na watu sahihi na kweli alistahili kuungana nao kupambana.

Kamati ya Taifa Stars ambayo imeshiriki kufanikisha au kuomba Rais Magufuli kujitokeza inastahili pongezi. Kuweza angalau kujaribu na kusahau yaliyokuwa yakisemwa kwamba Magufuli si mwanamichezo ni jambo la kupongeza.

Mwenyekiti wa Kamati ya Stars, Farouk Baghoza, Katibu, Teddy Mapunda na wajumbe wengine wamekuwa wakipambana na ndiyo maana unaona maandalizi yamekuwa ya kiwango cha juu. Vema wakaendelea kupambana hadi mwisho.

Kwa Watanzania wengine, ushindi wa Taifa Stars utakuwa ni wa wote. Hakuna ujanja sasa, itikadi za timu kwa maana ya klabu au vyama vya kisiasa ziwekwe kando na pamoja tuungane kesho kuisaidia timu yetu.

Kila mmoja anajua Stars itakapokuwa uwanjani Novemba 17, wenyeji raia wa Algeria wataizomea ile mbaya kuhakikisha wanaichanganya ili kikosi chao kifanye vema.

Watafanya hivyo kwa kuwa watakuwa wanalipigania taifa lao lifanye vizuri. Nafasi ya Watanzania itakuwa ni kesho Jumamosi na vema kama wataitumia kwa kuwa Waalgeria wao hawatafanya mzaha hata kidogo hiyo Novemba 17.

 Kama ni Mtanzania, unabaki kuwa Mtanzania na moyo wako utakuwa hapa Tanzania. Huu si wakati wa kulumbana na kusema hatuwezi kabla hatujapambana. Twende tukapambane kwanza.

Angalia rais wa nchi yetu naye anakuwa pale, vipi wewe uone haiwezekani au itakuwa vigumu. Umetoa mchango gani au ushauri upi hadi kufikia kesho? Bado una nafasi ya kulipigania taifa lako. Taifa Stars ni yako, yangu na ya wote.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic