December 2, 2015


Na Saleh Ally
WATANZANIA ni watu wasiopenda kuambiwa ukweli hata kidogo, ni watu wanaofurahia kufanya maovu na kukosolewa kwao linakuwa ni tusi.


Angalia Rais John Magufuli na Serikali yake, wanachokifanya katika kipindi hiki kinaonekana ni kitu kipya kabisa katika ulimwengu wa Watanzania.

Kinakuwa kipya kwa kuwa wengi walifanya mambo kwa ujanjaujanja na upigaji, waliamini kuiba mali ya umma ni haki yao na kitu kibaya zaidi walijijengea wigo, kwamba hakuna wa kuwafanya kitu.

Unaona kiongozi yuko ndani ya TFF, amepewa nafasi ambayo kiuwezo haiwezi na hawezi kuleta matunda, lakini anafurahia kwa kuwa atapata fedha za kuendesha maisha yake.

Angalia ndani ya klabu za Simba na Yanga, viongozi kibao tunawajua, wamediriki kugombea nafasi za uongozi huku wakijua ndani ya nafsi zao kwamba hawana uwezo wa kuongoza Simba.

Viongozi wanaokwenda kugombea Simba au Yanga, hawakuwahi kuongoza hata timu ya mtaa. Hawakuwahi hata kuona namna gani ai kipi kifanyike kusaidia maendeleo ya mpira.

Angalau wangekuwa wamejifunza, angalau wangekuwa wana elimu ya kitu wanachotaka kukiongoza. Pamoja na kujua hawana, lakini wanaamua kuingia kugombea, wakijua watapita njia za mkato na kushinda ili waiongoze klabu.

Kama unakwenda kwenye klabu, Yanga, Simba, Mtibwa Sugar, Azam FC na nyinginezo, unakutaka viongozi wasio sahihi katika uongozi. Halafu unarudi kwenye ngazi ya shirikisho, nako unakuta viongozi wasio sahihi na wasio na malengo ya kuendeleza mchezo wa soka. Unategemea utaendelea vipi?


Asilimia kubwa ya viongozi wa soka huona wanadhalilishwa pale wanaopoambiwa uwezo wao ni mdogo, hakika wanakuwa wanajua wazi kwamba hawana uwezo wa kuisaidia au kuyasaidia maendeleo ya soka hapa nchini.

Viongozi wa soka, wengi wao ni wale wanaoingia katika nafasi nyingi, kwa kuwa tu wana uwezo wa kuweka visingizo, kuanzisha kesi au kufanya chochote kuonyesha wamesingiziwa au kuonewa hasa wanapoelezwa ukweli.

Katika upande wa soka, malalamiko ya maendeleo kuwa duni ni makubwa sana. Viongozi wetu si watu waaminifu na wanaotaka kujifaidisha wao wenyewe. Utaona walivyokuwa wamelala viongozi wa sehemu nyeti nchini kama TRA, Bandari na kwingineko, mambo yakasababisha hasara kwa Watanzania.

Ndivyo ilivyo katika sekta nyeti za soka na michezo mingine. Wengi ni wapigaji, wenye maslahi zaidi na maisha yao na si maisha ya soka na michezo kwa ujumla na kamwe hawataki kuguswa kwa kuwa wanatengeneza uzio wasifikiwe au kuwekwa wazi.

Sidhani kama wadau wa soka wanapaswa kumsubiri Magufuli aje kuondoa uozo huo. Badala yake wale ambao wanajua uwezo wao ni mdogo, huu sasa ndiyo wakati mwafaka wa kuanza kujiondoa taratibu na kupicha nafasi kwa wengine wenye uchungu na lengo la kuendelea.

Kwangu ninaamini huu si wakati wa kuogopa au kuwahofia watu tena. Si wakati wa kuhofia wanaotaka kupunguza kasi ya kusema ukweli kwa vitisho vya kwenda mahakamani, vitisho vya kuwamaliza watu kwa kuondoa roho zao.

Mchezo wa soka na michezo mingine iko hatarini kuporomoka zaidi ya hapa kwa kuwa haina watu sahihi. Huu ni wakati mwafaka wa kuwafichua na kueleza matendo yao, kukumbusha maovu yao na kusisitiza kwa kuwataja kwa majina, kwamba wanapaswa kuondoka ili wawapishe wengine waongoze soka na kuleta maendeleo.

Kiongozi anakasirishwa kabisa kuambiwa hana uwezo, anaamini amedhalilishwa kwa sababu kaelezwa ukweli. Lakini hana chochote cha mafanikio alichokifanya zaidi ya kutumia vibaya fedha za Watanzania zinazopatikana kupitia soka.

Mimi nafunga uoga huo, nitasimama hadi nitakapobaki peke yangu. Lakini nitakuwa niliyesema ukweli, niliyepigania maendeleo ya michezo ambayo inayumba.

Ila safari hii nitakuwa wazi zaidi, ikiwezekana kumzungumzia kiongozi mmoja zaidi ya mara moja na kuweka wazi madudu yake bila ya woga wala kuogopa chochote.

Mlio katika klabu za Simba, Yanga na nyingine, kumbukeni ni mali ya wananchi. Mlio TFF, msianze kuamini ni mali yenu, misifikiri madudu mengi mnayofanya ni siri kubwa. Mimi sitamsubiri Magufuli afike kwenu, nitapambana hadi mwisho na msitegemee uoga kunizimbele ya uso wangu. Mnaweza kuchagua, mbaki na kuwa watendaji wa kweli, au ondokeni muwapishe wenye uwezo wa kuusaidia mpira wetu.

Angalia leo, kila sehemu tunakwama. Angalia hata katika viwango tu vya Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), Tanzania inazidiwa na karibu kila nchi ya ukanda wa Afrika Mashariki na Kati. Halafu, mnajisikia vibaya kuitwa mna uwezo mdogo!




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic