July 20, 2018


 
NA MWANDISHI WETU, SONGEA
SHULE ya Sekondari Londoni iliyopo Lizaboni mjini Songea Mkoa wa Ruvuma imeibuka vinara wa jumla katika mashindano ya Mdahalo ‘Debating’ yaliyoandaliwa na Taasisi isiyo ya Kiserikali ya Songea-Mississippi (SOMI), kupitia tamasha la Majimaji Selebuka.

Shindano hilo lilifanyika kwenye ukumbi wa Chuo cha Ualimu Songea mkoani Ruvuma ambako Mgeni rasmi alikuwa Mbunge wa Songea Mjini, Dk. Damas Ndumbaro na kuhudhuriwa na wawakilishi kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania  (TRA), na Benki ya NMB waliokuwa wadhamini.

Mada shindaniwa ilikuwa ni faida na hasara za ulipaji kodi kwa kutumia mashine za kielektroniki ‘EFD’s’.

Katika kipengele hicho cha Ushindi wa Jumla ‘Best School Over All’, Londoni ilifuatiwa na Sekondari ya Ruhuwiko huku nafasi ya tatu ikishikwa na Songea Boys.

Kipengele cha Uwasilishaji Bora ‘Best Presentation School’ Songea Girls waliibuka washindi wakifuatiwa na Peramiho Girls huku nafasi ya tatu ikinyakuliwa na Daora kutoka jijini Dar es Salaam.

Wawakilishi Bora ‘Top 5 Best Presenters’ waliopenya ni Elda Simwamba kutoka Peramiho Girls ambaye alikuwa kinara, Yusto Mwaiginsya kutoka Sekondari ya De Paul, Faines Msola wa Songea Girls, Nasma Ally wa Daora na Christandus Mhagama kutoka Luwawasi Sekondari.

Pia kulikuwa na shindano la uchoraji vibonzo, ambako Oscar Ngonzi wa Sekondari ya Pehisco aliibuka mshindi akifuatiwa na Mwanaidi Mbunde wa Maposeni huku nafasi ya tatu ikienda kwa Sharifa Makarani wa Sekondari ya Londoni.

Washindi walizawadiwa zawadi mbalimbali ikiwamo tuzo, fedha taslimu, vifaa vya kitaaluma na kimichezo, kufunguliwa akaunti benki ya NMB na kuwekewa kianzio.

Aidha,  walimu waliofanikisha shule zao kufanya vizuri walikabidhiwa zawadi za fedha taslimu.

Akizungumza kabla ya Mgeni rasmi, Mkurugenzi wa Elimu ya Mlipa Kodi TRA, Richard Kayombo, aliwapongeza waandaaji na washiriki, kwani wanatoa mchango mkubwa katika kujenga utamaduni wa kulipa kodi kwa jamii.

“Waandaaji wangeweza kulenga kitu kingine, lakini wameamua kuandaa mada hii, tunawashukuru kwani wanajenga walipa kodi wajao…Wengi wetu tumelikuta hili ukubwani ndio maana unaona kuna ukakasi kwa baadhi ya watu katika kulipa kodi,” alisema na kuongeza.

Lakini jamii ikijengewa uelewa na kuelewa faida za ulipaji kodi itasaidia serikali katika ukusanyaji wa kodi na kufanikisha kuendesha shughuli mbalimbali za kimaendeleo.

Kwa upande wake Mgeni rasmi, Dk. Ndumbaro, mbali na kuwapongeza washiriki na kuwataka kuwa mabalozi wema katika kutoa elimu juu ya faida ya ulipaji kodi.

Dk. Ndumbaro, alibainisha kuwa tofauti kubwa ya nchi zinazoendelea na zilizoendelea na ufanyaji kazi na ulipaji kodi.
“Nchi haiwezi kuendelea bila kufanya kazi, kwenye wanafunzi kazi kubwa ni kusoma kwa bidii na pia kushiriki stadi za mikono…Wenzetu nchi zilizoendelea wanachapa kazi sana na kulipa kodi zinazojenga nchi na nyingine tunazoenda kuomba misaada, lakini sisi ni wavivu na visingizio vingi katika kazi na kutoona umuhimu wa kulipa kodi,” alisema Dk. Ndumbaro.

Aidha, alisisitiza kuwa ulipaji kodi ni uchumi hivyo asiyelipa kodi ni adui wa maendeleo na anapaswa kupigwa vita.

Dk. Ndumbaro ambauye pia ni Mkurugenzi mwenza wa SOMI, aliwapongeza TRA na NMB na kwamba tamasha la mwakani litakalofanyika kuanzia Julai 13-21 kwa upande wa mdahalo mada itaendelea kuwa ulipaji kodi katika maeneo mengine zaidi ya mashine za kielektroniki iliyokuwepo mwaka huu.






0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic